Friday, August 7

Rekebisha matumizi ya neno Upinzani

Lugha ya Kiswahili ina utajiri mkubwa wa msamiati na istilahi  anuwai. Msamiati ni jumala ya maneno yote yaliyomo katika lugha fulani, sio kama vile baadhi ya walimu  wa shule za msingi wanavyowakaririsha wanafunzi wao kuwa “ msamiati” ni maneno magumu.
Pamoja na ukweli kwamba  Kiswahili kina heshima kubwa kwa kuwa wazungumzajii wake wengi ni waungwana, wastaarabu na wenye heshima ya kutosha. Lakini  ipo  baadhi ya misamiati kadhaa wa kadhaa bado inayokanganya ikilinganishwa na uhalisia au dhana zinazorejelewa.
Kwa niaba ya familia ya ‘Wafia Kiswahili Tanzania (wakita)’, leo ninaomba kuchokoza mjadala kuhusu misamiati miwili tu katika lugha hii aushi ya Kiswahili.  Kwa hakika misamiati hii si migeni katika masikio yetu. Mara nyingi tunaisikia na kuitumia misamiti hii katika muktadha mbalimbali.  Misamiati yenyewe ni  “ UPINZANI “ na “ USHINDANI “.
Kwa mujibu wa Kamusi ya Kiswahili Sanifu toleo la pili, (TUKI), wameeleza neno upinzani kuwa ni “hali ya kupingana, ubishani au ukinzani, Pia wameeleza kama kuna kundi la upande unaopingana”
Kwa mantiki hii, hatuwezi kukosoa ikisemwa kuwa, upinzani msingi wake ni kupingana. Na huenda haitakuwa kosa ikiongezwa zaidi kwamba, mpingaji mzuri ni yule apingaye mwanzo mwisho na sio kubip kupinga.
Dhana hii  ya  kupinga inafanya kuwe na pande mbili zenye ukinzani wa dawamu hata kwa jambo lenye faida au matokeo bora kwa pande zote.  Muda wa kuwa ni wapinzani, hakuna haja ya kukiri ubora wala ufanisi wa jambo lolote lile la mpinzani wako.
Kwa upande wa neno “ ushindani”. Neno hili limeelezwa katika ukurasa wa 443 wa kamusi tajwa kuwa, ni “ hali ya kushindana” kwa dhana ya kushindana wachache ndio pengine hawataelewa haraka kwamba, katika kushindana lazima  pawapo na mshindi  wa  mashindano fulani. Matokeo ya mashindano hayo ni upande mmoja kushinda na mwingine kushindwa. Waswahili katika  mawanda haya ya mashindano hawakutafuna maneno, Waswahili   husema, “ asiyekubali kushundwa si mshindani” Msemo huu chambilecho kwa wanamichezo wote ulimwenguni.
Kwa msemo huu wa Waswahili, pengine huashiria uungwana na maafakiano yao  katika kuridhia kushinda au kushindwa  katika mashindano yao, hata kama mshindi atapewa zawadi kubwa au mshindwa ataadhibiwa. Kwa hoja na maelezo hayo, sina shaka haiwezi kukuchukua muda mrefu kutanabahi kuwa, kushindana si kupingana. Hata kama upo wakati fulani washindanao huhitajika kupingana , kupingana huko kutakuwa kwa minajili ya  kufanya mashindano yao kuwa hai zaidi. Jambo hili litaingia akilini kwa kueleweka  kama uhai  wa mashindano si uhasama mchezoni.
Dhana hii ya uhai wa mashindano na sio uhasama mchezoni  ndio ilifanya wadau wa michezo kuwa na dhana ya ustaarabu mchezoni “ fair play “ . kushindana bila ya uadui mchezoni.
Hali inakuwa tofauti kabisa tukizibeba dhana hizi mbili kutoka katika lugha ya kimombo kuzifanyia tafsiri sisisi (tafsiri ya moja kwa moja) kuwa katika Kiswahili.
Neno la Kiingereza “oppose “ lenye maana ya Kiswahili kupinga na “compete “ lenye maana ya Kiswahili  shindana .
Katika medani ya kisiasa za nchi yetu, neno moja limekita mizizi zaidi ya jingine.  Na kama kuna kosa tulilolifanya sisi Waswahili katika medani ya siasa zetu hapa nchini, basi ni pale mnamo mwaka  1992  wakati tulivyoridhia mfumo wa vya vingi, na kuviita vyama vipya vyote kwa neno hili la “upinzani” nitafafanua.
Hebu sasa tudodose kidogo uhai na uhalali wa neno“upinzani” katika tasnia ya siasa ya nchi sanjari na ukomavu wa demokrasia na maendeleo shirikishi katika nchi yetu.
Kwa kuwa imeshaelezwa hapo juu maana ya neno “ upinzani” ambalo likinyambuliwa zaidi linaweza kutupa maneno kama : pinga, pingana, pingia,  pingania, pinzana, nk.
Msamiati huu huu mmoja tu, tena kwa haraka unaweza usionekane kama una madhara katika jicho la demokrasia na maendeleo ya taifa lakini ukitazamwa kwa jicho la tatu itabainika kuwa huu msamiati ni shida! Hususan katika siasa za nchi za Afrika.
Kwa mfano, ni mara ngapi walikaririwa hao wanaoitwa wapinzani, wakisema serikali hii iliyo madarakani haijafanya kitu cha maana ( rejea hotuba maarufu ya mchungaji mmoja ndani  Bunge la awamu ya nne), na wakati mwingine kaenda mbali zaidi kiasi cha kusema, serikali haijafanya lolote tangu uhuru. Kwa upande wa chama ambacho kinaona kinapingwa nacho  kinasikika kikieleza mafanikio yao ambayo hata mimi binafsi ninyaona pasi miwani ( kama : mtandao wa barabara nchi nzima, Chuo kikuu cha Dodoama, uhuru wa maoni , nk).
Kwa upande wa pili wa shilingi , ni mara ngapi hao waitwao wapinzani wameishauri serikali kwa namna bora zaidi kuhusu maendeleo ya nchi yetu, lakini serikali inakataa ushauru wao tena bila hoja za msingi. (Rejea ushauri wa kuahirisha uchaguzi mkuu, kutazamwa upya kwa mchakato wa katiba, kutofanya haraka kupitisha baadhi ya  miswaada mbalimbali kama ya  gesi na mafuta, nk).
Ni nani katika chama tawala anaweza kusema hadharani kuhusu ushauri mzuri uliyowahi kutolewa na waitwao wapinzani ambao serikali umeuchukua kwa manufaa ya nchi yetu? Iwapo halipo jambo lililozingatiwa na serikali kutoka upande wa vyama vinavyoitwa vya upinzani wala hakuna wa kulaumiwa.  Kwani haitarajiwi Yanga itoe ushauri mzuri kwa Simba unaohusu mafanikio yao. Yanga ikiwa ina mchezo wa kimataifa, Simba ndio huona hiyo ni fursa nzuri zaidi ya kuikomoa Yanga kwa kushangilia wapinzani wa Yanga ili kuipa fedheha .
Ni mara ngapi, mwanachama mmoja akihama chama kimoja cha siasa na kwenda kingine kama ilivyokuwa hivi kwa mbunge mmoja kutoka NSSR kwenda chama cha ACT , NSSR wanaweza kumuona mbunge huyo  ni msaliti hata kama  alikuwa na sababu nzuri zaidi za kuhama kuliko kubaki katika chama chake cha zamani.  Kwa nini? Bila shaka, ni dhahiri kuwa , mwanachama huyo hutafsiriwa kuwa amekwenda upinzani.
Cha kujiuliza, hapa ni kwamba,  mbona vigogo hawa wa pande mbili za siasa, kwa maana wale wanaoitwa wapinzani na wanaona wanapingwa, nje ya uga wa siasa wanaunganishwa na mambo kadhaa, kama dini, makabila, kanda zao, na timu za michezo, nk. Lakini mara tu wanapokuwa ndani ya majukwaa ya kisiasa huwezi kuamami kama ndio hao hao wakutanao kanisani/misikitini au Jangwani na Msimbazi. Inachekesha kidogo, ukijiuliza unaweza kudhani kwamba, mkataba wa kupingana kwao ni katika siasa pekee.
Kwa vile msamiati huu wa “upinzani”  hauwezi kuwapika wanasiasa katika chungu kimoja , ninatoa hoja kuwa tufikiri msamiati mbadala wa kufanya mijadala ya kiungwana, yenye afya njema kwa nchi yetu ili nchi inufaike na uweledi wa kila mwananchi kutoka upande wowote ule wa siasa aliyopo. Kwa maelezo hayo, sasa hoja yangu ni kwamba, msamiati “ushindani” unafaa zaidi katika mazingira ya hali ya siasa zetu za Kiafrika. Msamiati huu utafanya uwanja wa siasa uwe na upinzani usio na uhasama kuliko ilivyo sasa.  Wasiwasi wangu kama wasemavyo Waswahili “ wasiwasi ndio akili “ likiachiwa zaidi neno hili -upinzani katika ya siasa zetu nchini, hatima yake haitakuwa njema kutokana na uzoefu wa miaka zaidi 20 ndani ya siasa za ushindani. Sina shaka ya kuwa neno ushindani  wa siasa ni  mwafaka zaidi kama tunataka maendeleo shirikishi katika taifa letu.  Ndugu zangu ebu tuone , nchi ikiwa ni bingwa wa uchumi lakini nchi yetu haimtumii ipasavyo  katika mambo ya uchumi …..kisa yeye ni mpinzani……. Kweli ni sawa katika nchi kama hii  au  kuwa na mtaalamu wa mambo ya sheria lakini  hatumiki kikamilifu , maoni  yangu ni kuwa,  uwanja wa sheria ungemhitaji sana mtu wa namna hii   katika maendeleo ya taifa letu,   lakini wapii  na wengine wengi tu…..tunakosa michango yao kikamilifu kwa msamiati wa upinzani!
Nimeshawishika kufikiri mbadala huu baada ya tafakuri ya kina, kwa kuzingatia maslahi mapana ya taifa  Ninafikiri neno ushindani litatuweka pamoja sote na kushiriki kikamilifu katika harakati za maendeleo kama taifa huru.
Dhana hii ya ushindani itafanya wanaoshindana kuwa makini zaidi, kusoma mbinu za mchezo za mshindani wake, kutumia udhaifu wa mshindani,  kuboresha pale penye upungufu, nk.
Kwa dhana hii ya ushindani inaweza kufanya siku moja kuwe hata  na kamati ya pamoja ya kushughulikia namna ya kuendesha, kutathmini na kuboresha mashindano yao. Yaani kuwe na kamati ya mseto ya mashindano . jambo hili si rahisi kwa  ile dhana upinzani kuwa na kamati ya mseto ya upinzani.
Tukifikia hatua hii, inafikiriwa, hapatakuwa na haja ya kukanusha mazuri  yaliyofanywa na mshindani mwenzio. Haitapatikana haja ya kukataa ushauri wa mshindani mwingine.
Hivi ni nani katika hatua hii awezaye kupinga mchango wa Mtanzania mwingine iwapo mchango huo utaonekana una tija kwa jamii nzima ?,  Lakini kwa dhana ile ya upinzani, ni nani hata kwa bahati nasibu atakayechukua mawazo ya anayempinga hata kama ni mazuri ? Ipo wazi kabisa, kama mtu anakupinga itatokeaje siku moja  akupatie mbinu ifaayo? Kama si miujiza nini! Hivi kweli Yanga ipo siku itaamba mbinu ya ushindi Simba au kinyume chake ?
Kwa dhana ya ushindani, ni nani atakayechukia na kuchukiwa kwa kuitwa mshindani ?,
Kwa mantiki ile ile, ni nani atakayekataa kushindwa kama ikitokea bahati mbaya ya kushindwa? Lakini kwa kuwa kwa sasa katika siasa zetu kuna dhana ya upinzani, basi hata pale chama kitapoamua yasiyotarajiwa na wengi pana uwezekano wa kutokea kwa sintofahamu kama ilivyoshuhudiwa hivi karibuni mjini Dodoma. Kwa nini, kwa sababu katika dhana ya upinzani, hakuna ustaarabu wa kukubali kushundwa lakini katika kushindana inasemwa ,“ Asiyekubali kushindwa si mshindani”
Kwa dhana hii ya ushindani inaweza kutoa picha nzuri zaidi hata katika  uwanja wa Bunge. Kwa mfano , anayeitwa kiongozi wa kambi ya upinzani bungeni,  kwa taaluma ya semantiki (elimu maana) angeweza kuitwa mpinzani mkuu bungeni lakini kwa dhana hii ya ushindani, angeweza kujulikana  kama kiongozi wa kambi ya  ushindani bungeni, hivyo ni mshindani mkuu. Ni Mtanzania gani angemuona kiongozi huyu ni mpngaji wa kila jambo ndani ya Bunge kama ilivyo sasa ambapo kiongozi wa kambi rasmi ya upinzani bungeni ndiye pengine huonekana kuwa ni mpinzani mkuu.
Iwapo atatokea mtu akasaili juu ya kitu gani kinashindaniwa. Pamoja na majibu mengine angeweza kujibiwa kuwa , Ikulu ndio inashindaniwa. Mwingine akihoji ni kwa vipi wanashindana, angeweza pia kujibiwa , ni kwa hoja wanashindana,  na hoja zenyewe ni za nguvu, ambapo hoja  za nguvu zaidi  ndizo zitakazo shinda. Kinyume  chake ni kwamba,  hoja za nguvu zaidi ndizo zitakazopingwa kwa dhana ya upinzani.
Mfano hai, ni pale Mheshimwa Hamisi Kigwangwala baada ya kukosa ridhaa ya chama chake kuteuliwa kuwania nafasi ya urais mwaka 2015, mara moja aliandika katika ukurasa wake wa facebook pengine na sehemu nyingine kuwa , amekubali matokeo , hivyo  anatazama mbele zaidi katika siasa kupitia chama chake ( huyu alishindana kisiasa ).
Pia kwa dhana ile ya upinzani, ninakumbuka zaidi maneno ya mchungaji mashuhuri  pale bungeni aliposema ,“ Mimi kama mpinzani sikuja kupongeza  hapa bungeni, ninakukosoa ufanye kazi yako vizuri
Wakati washindani wapo tayari kukiri, kupongeza  na kukubali hata matokeo lakini mpinzani hana cha kupongeza na upo uwezekano hata wa kukataa matokeo.
Ndugu zangu, kama hatuwezi kukubaliana, kuelewana na kuafikiana na kupeana mbinu za mafaniko kwa kigezo tu cha upinzani wa kisiasa. Kwa nini sasa isitafutwe busara ya kufikiri vinginevyo ?
 Ninatoa hoja kuwa  kwa vile upinzani haujatusaidia kwa zaidi miaka 20 hapa nchini, tugeukie katika ushindani. Sina shaka utatoa matokeo chanya kwa maendeleo na mustakabali wa taifa letu.
Upinzani hautakiwa Tanzania, sasa tufikiri ushindani wa siasa.
Mungu ibariki Tanzania,
Mungu ibariki Afrika.
Mwenyekiti wa Wafia KiswahiliTanzania (Wakita)
Majid Mswahili.

Wabunge 51 waanguka kura za maoni


Wafuasi wa CCM 

Dar es Salaam. Wakati vyombo vya juu vya baadhi ya vyama vya siasa vikiwa vimeanza hatua za mwisho za kupitisha wagombea wa ubunge na udiwani tayari kwa Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25, hadi juzi wabunge 51 walikuwa wameanguka kwenye kura za maoni za ndani ya vyama vyao.
Idadi hiyo ni takriban asilimia 14 ya wabunge 357 wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, inayojumuisha waliochaguliwa na wananchi na wa viti maalumu, ambao waliamua kwenda kupambana majimboni.
Miongoni mwa walioanguka ni mawaziri wa Serikali ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, ambao walikuwa wakitetea viti vyao majimboni.
Kati ya wabunge hao walioanguka, wawili wanatoka Chadema, wanne CUF na wengine 45 waliosalia wanatoka CCM.
Matumaini pekee yaliyosalia kwa wabunge hao ambao baadhi yao wamekata rufaa kupinga matokeo ya kura za maoni, ni huruma za vikao hivyo ambavyo vinaweza kubadili matokeo ya baadhi ya majimbo, hasa ambayo taratibu zilikiukwa na ushahidi wa kuwapo matumizi ya rushwa.
Wakati wabunge walioanguka Chadema wanasubiri kwa hamu kikao cha Kamati Kuu kilichoanza juzi kupitia majina hayo, wa CCM wanasubiri mfululizo wa vikao vinavyoanza leo hadi Agosti 13, wakati mchakato kupitisha wagombea wa NCCR-Mageuzi bado.
Kwa wabunge wa CUF, hakuna matumaini kutokana na vikao vya juu vya chama hicho kukamilisha kazi yake hivi karibuni.
Mbali na walioanguka, wabunge waliopita katika kura za maoni lakini vyama vyao vinaunda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), nao watalazimika kusubiri hadi vyombo hivyo vya mchujo vitakapomaliza kazi, kujua kama wamepita.
Hiyo inatokana na makubaliano ndani ya umoja huo ya kusimamisha mgombea mmoja atakayeungwa mkono na vyama vyote.
Kwa mujibu wa makubaliano ya vyama hivyo vinne; Chadema, CUF, NLD na NCCR - Mageuzi- kinachooonekana kina nguvu kwenye jimbo fulani ndicho mgombea wake ataachiwa kupeperusha bendera ya umoja huo, jambo ambalo vyama hivyo vilisema vimekamilisha kazi ya mgawanyo kwa asilimia 95.
Wakati Chadema, CUF, NCCR na NLD wakisubiri utekelezwa wa makubaliano hayo, wabunge wa CCM watakuwa njiapanda baada ya chama hicho kueleza kuwa hakitarudia makosa ya mwaka 2010 ya kupingana na maoni ya wanachama kwa kutengua matokeo ya kura za maoni.
Profesa wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Jamidu Katima alisema kuanguka kwa wabunge hao kunatokana na wengi wao kutoonekana majimboni baada ya kupewa dhamana ya kuongoza wananchi.
“Kama kiongozi umepewa dhamana, lakini huonekani jimboni basi ni dhahiri wananchi watakukataa. Wakikuona unachukua fomu watakushangaa lakini ujue watakukataa kwa sababu huwatatulii kero zao kama ulivyoahidi awali.”
Profesa Katima alisema kwa sasa Watanzania wameamka, hivyo ni vigumu kudanganyika na kwamba kama kiongozi hatumii vyema dhamana aliyopewa, wananchi watamuacha apumzike kwa amani.
Maoni kama hayo yalitolewa na mhadhiri wa sayansi ya siasa wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Alexander Makulilo ambaye alisema zipo sababu chekwa za baadhi ya mawaziri kushindwa kwenye kura za maoni, mojawapo ikiwa ni makundi na kushindwa kutimiza ahadi.
Kujaribu mtu mwingine
Dk Makulilo alisema ni rahisi kwa wananchi kuacha kumchagua kiongozi baada ya kuona hajatimiza kile alichoahidi hivyo wakaona wajaribu kiongozi mwingine pengine atawatatulia kero zao.
Kuhusu kuanguka kwa wanasiasa nguli wa CCM, mhadhiri huyo alisema sababu nyingine ni siasa za makundi ambako kundi moja tu linaweza kufanya juhudi ili mwingine ashindwe.
“Sasa hivi tunazungumzia mtu kuanguka katika chama chake, kwa hiyo siasa za makundi ndani ya chama hicho inaweza kusababisha kuanguka katika kura za maoni,” alisema.
Sababu nyingine aliyoitaja Dk Makulilo ni wimbi la vijana na kuwa inawezekana wananchi wanahamia kwa wanasiasa vijana zaidi baada ya kuona wengine amekaa madarakani kwa muda mrefu.
Pia, aliitaja rushwa kuwa miongoni mwa sababu za kuanguka kwani inawezekana kuwa mgombea mwenzake ametoa fedha au yeye ametoa, lakini mwingine ametoa nyingi zaidi.
“Nadhani umeona jinsi ambavyo Takukuru wamekamata wagombea wengi kwa tuhuma za rushwa kwa hiyo hapana shaka kuwa suala la rushwa lilikuwepo,” alisema.
Utafiti wa Twaweza
Idadi ya wagombea hao walioanguka katika hatua ya awali inaashiria kuanza kutimia kwa matokeo ya utafiti uliofanywa na taasisi ya Twaweza mwishoni mwa mwaka jana ambao ulionyesha kuwa nusu ya wabunge wataanguka kwenye kura za maoni.
Kwa mujibu wa utafiti huo uliotangazwa Novemba 12, 2014, kuanguka kwa wabunge hao kutatokana na kushindwa kutekeleza ahadi zao. Asilimia 47 ya wananchi walioulizwa iwapo watampigia tena kura mbunge wao, walisema “hapana” huku asilimia kama hiyo ikisema “ndiyo”.
Utafiti huo ulieleza kuwa ahadi nyingi zilizotolewa na wabunge kwenye mikutano ya kampeni wakati wa uchaguzi hazijatekelezwa na kwamba asilimia 78 ya wananchi bado wanazikumbuka.
CCM kutorudia makosa
Wakati utafiti wa Twaweza ukizungumzia kutotimizwa kwa ahadi, wabunge waliopita kura za maoni watakuwa wakijifariji na matamshi ya viongozi wao kuwa majina yao hayatakatwa kama ilivyokuwa mwaka 2010.
Akihutubia kwenye mkutano wa hadhara mjini Iringa Oktoba mwaka jana, Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana alisema chama hicho hakitarudia makosa ya kuengua majina ya wagombea wanaopitishwa na wanachama kwenye kura za maoni baada ya Frederick Mwakalebela kuenguliwa na Halmashauri Kuu kugombea ubunge wa Jimbo la Iringa Mjini na baadaye Mchungaji Peter Msigwa wa Chadema akatwaa jimbo hilo.

Mke wa Dk Slaa afunguka


Dar es Salaam. Siku moja baada ya Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa kuzungumza na gazeti hili na kusema yupo salama, mke wake, Josephine Mushumbusi amekanusha tuhuma zilizozagaa kuwa ndiye aliyemshauri kiongozi huyo wa Chadema kujiuzulu na kumzuia kushiriki vikao muhimu vya chama.
Tetesi hizo zilivuma kwenye mitandao ya kijamii na vyombo vya habari baada ya Dk Slaa kutoonekana katika vikao muhimu vya Chadema na Ukawa, kuwa Mushumbusi hakupendezwa na kitendo cha Lowassa kupitishwa kuwania urais chini ya mwavuli wa Ukawa na badala yake alitaka Dk Slaa ndiye awe mpeperusha bendera.
Kwa mujibu wa taarifa hizo ambazo Mushumbusi amezikanusha, aliamua alimfungia ndani Dk Slaa kama moja ya mbinu za kumzuia asishiriki shughuli za kichama, tuhuma ambazo amezikanusha.
“Bosi wako akija kukuomba ushauri utamsaidia, lakini akija akakuambia ameshafanya maamuzi unaweza kupingana naye?” alihoji Mushumbusi akianza kutoa maelezo yake na kuendelea:
“Wakati wa vikao nilikuwa namwona (Dk Slaa) anachelewa kurudi kila siku, siku moja akaja akaniambia uamuzi aliouchukua na mimi sikuwa na la kusema, nikachukua shuka nikajifunika.”
Katika mahojiano yake ya kwanza na Mwananchi baada ya kuzagaa kwa tetesi hizo, Mushumbusi pia alikana kumfungia Dk Slaa ndani ya nyumba, akisema wakati maneno hayo yalipokuwa yanazagaa, alikuwa nje ya nchi na wala hakujua kinachoendelea.
“Mwenyewe najiuliza nini kinaendelea, siwezi kufanya kitu kama hicho. Nyumba yangu ina milango miwili, nawezaje kumfungia mtu, tena mwanamume, hata watoto siwezi kuwafungia. Kuna mambo mengine mwanamke huwezi kuyafanya kwa mwanamume. Mwanamume ni mwanamume tu,” alisema.
Alisema viongozi wa Chadema, ndugu, jamaa na marafiki walikuwa wanafika nyumbani kwake na walikutana na Dk Slaa na kuzungumza naye... “Kama ningekuwa nimemfungia wangezungumza naye vipi?”
Mushumbusi alisema mwanamke anaweza kufanya chochote lakini kuna baadhi ya mambo ambayo mwanamume akiamua ni vigumu kumzuia.
Akifafanua tuhuma za kumshinikiza Dk Slaa kujiuzulu Chadema, Mushumbusi alisema kiongozi huyo wa Chadema ana uamuzi wake na yeye ni msaidizi tu ambaye hana uamuzi wa mwisho kwenye familia.
Hata hivyo, alisema endapo angeamua kumshawishi, uwezo wa kufanya hivyo anao lakini yeye ni mwanamke mwadilifu anayependa mafanikio ya mumewe.
“Kwani unanionaje? Mimi ni ‘strong’ (nina nguvu), ningetaka ningefanya hivyo, nisingeshindwa,” alisema.
Pamoja na hayo, Mushumbusi alilalamika kuwa tuhuma hizo dhidi yake zimesababisha asisikilizwe kama ilivyokuwa awali.
Bila kufafanua kwa undani, alisema kuna kundi linalounda propaganda hizo ili abadili mtazamo kuhusu mumewe lakini jambo hilo haliwezi kutokea.
“Nilisema nitampenda kama alivyo, sitajali chochote wala akiwa katika hali gani au chama gani. Kazi yangu ni kumtia moyo ili kile atakachofanya kifanikiwe,” alisema.
Auza mkaa
Mbali na kukanusha vikali tuhuma hizo, Mushumbusi alisema alikwishajitoa kwenye masuala ya siasa kwa miaka miwili sasa na badala yake ameamua kufanya biashara ya kuuza mkaa.
“Nimenyamaza kimya, nimekaa kando ninaendelea na biashara yangu ya kuuza mkaa, nipo mbali na siasa na sitaki kujua kinachoendelea, kwanza hata mchakato wenyewe siujui,” alisema.
Aliwashauri wanawake kuacha kushabikia masuala yanayotokea ndani ya ndoa yake na kuwataka wavae viatu anavyovivaa na wajue kuwa anapitia wakati mgumu.

Mtikisiko: Ni baada ya Profesa Lipumba kujiengua uenyekiti CUF


Aliyekuwa Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba akiaga waandishi wa habari baada ya kuwatangazia kujivua wadhifa huo katika mkutano alioufanya Dar es Salaam jana. 


Dar es Salaam. Hakuna neno jingine linalofaa kuelezea hali ilivyo ndani ya Ukawa zaidi ya “mtikisiko” baada ya Profesa Ibrahim Lipumba kuamua kujivua uenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF) wakati mkakati wa vyama vya upinzani kushirikiana kutaka kushika dola ukiwa umeshika kasi.
Uamuzi wa Profesa Lipumba, mmoja wa waasisi wanne wa Ukawa-Umoja wa Katiba ya Wananchi unaoundwa na vyama vinne vya Chadema, CUF, NCCR Mageuzi na NLD-,unamaanisha anapoteza wadhifa wake wa mwenyekiti mwenza wa umoja huo ambao umeamua kushirikiana kwenye Uchaguzi Mkuu kwa kusimamisha mgombea mmoja kuanzia ngazi ya urais hadi udiwani atakayeungwa mkono na vyama hivyo.
Wengine walioongoza harakati za kuasisi Ukawa ni Freeman Mbowe, ambaye ni mwenyekiti wa Chadema, James Mbatia wa NCCR-Mageuzi na Emmanuel Makaidi wa NLD.
Profesa Lipumba, mmoja wa wenyeviti wanne wa Ukawa walioeleza sababu za kumkaribisha Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa kwenye umoja huo takribani siku 10 zilizopita, jana alieleza kuwa ameamua kujivua wadhifa huo kutokana na vyama hivyo kukubali kupokea watu walioshiriki kukataa Rasimu ya Katiba iliyopendekezwa na wananchi, kitu ambacho kilikuwa msingi wa kuundwa kwa Ukawa.
“Nimejitahidi sana ndugu zangu kuvumilia, lakini dhamira inanisuta,” alisema Profesa Lipumba mbele ya waandishi wa habari jana kwenye Hoteli ya Peacock baada ya mkutano wa juzi aliopanga kufanyia ofisi za CUF kuzuiwa na wanachama.
“Sisi tumekaa tunaipigia kelele Rasimu ya Katiba ya (Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliyokuwa chini ya Jaji Joseph) Warioba lakini iliyopitishwa ni Katiba Inayopendekezwa sasa tunawachukua waliopitisha ili waje kuisimamia. Hivi inaingia akilini?”
Lipumba aliwaomba radhi wanachama na wananchi waliomuamini wakati wote wa uongozi wake.
Tamko la maneno 900
Katika taarifa yake ya maneno 900 ambayo aliisoma mbele ya waandishi wa habari jana, Profesa Lipumba, ambaye amekuwa akibashiriwa kuchukua uamuzi huo tangu katikati ya wiki hii, alisema pamoja na kujivua uongozi hatahama CUF na kwamba ameshalipia kadi yake hadi mwaka 2020.
“Leo hii nimeikabidhi ofisi ya Katibu Mkuu barua yangu ya kung’atuka nafasi ya mwenyekiti wa taifa, lakini naendelea kuwa mwanachama wa CUF na kadi yangu imelipiwa mpaka mwaka 2020,” alisema Profesa Lipumba aliyekiongoza chama hicho kwa miaka 16.
Huku akionekana kuwa mtulivu, alisema hajashinikizwa wala kushawishiwa na mtu yeyote kujiuzulu na kwamba uamuzi huo ameufanya baada ya kutafakari sana na kushauriana na familia yake ambayo alisema imeridhia.
Mtaalamu huyo wa masuala ya uchumi alisema ameshiriki katika vikao vingi vya Ukawa vilivyowafikisha hapo walipo, lakini dhamira na nafsi vinamsuta kuwa wameshindwa kuenzi na kuzingatia tunu za Taifa za utu, uzalendo, uadilifu, umoja, uwazi na uwajibikaji.
Alipoulizwa sababu za kugeuka wakati yeye alikuwa ni miongoni mwa wenyeviti wa Ukawa waliomkaribisha Lowassa Ukawa, alikiri akisema kuwa suala la rushwa na ufisadi ni mfumo ambao lazima uondolewe lakini kwa sasa “dhamira yangu na nafsi yangu vinanisuta”.
Profesa Lipumba alipotakiwa kueleza iwapo kujiuzulu kwake kunahusiana na tuhuma za kuhongwa mamilioni na CCM ili kuusambaratisha Ukawa, alijibu:
“Yametengwa wapi? mimi sina taarifa hizo. Tulielezwa sisi tumemkaribisha kwa sababu tumepatiwa mamilioni na sasa unasema mamilioni yametengwa kusambaratisha Ukawa. Ila ninalosisitiza ni kwamba linalonipa tatizo ni dhamira na nafsi yangu, si vingine.”
Profesa Lipumba aliyekuwa ameongozana na mdogo wake Shaaban Miraji na rafiki yake Abdallah Shaaban, alisema kama mwanachama wa kawaida atashiriki kampeni za chama lakini ataendelea kuiunga mkono Rasimu ya Katiba ya Warioba.
Ukawa iliundwa mapema mwaka jana na wajumbe wa Bunge la Katiba kutoka vyama hivyo vinne kupinga mwenendo wa chombo hicho cha kuandika Katiba, wakisema kilipuuza maoni yaliyokuwa kwenye Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa na Tume ya Warioba na kuweka maoni yaliyotokana na maagizo ya CCM.
Miongoni mwa mambo yaliyozua mjadala mkubwa ni muundo wa Serikali ya Muungano baada ya Rasimu ya Katiba kupendekeza serikali tatu, na pia suala la Tunu za Taifa ambazo zilipendekezwa kuwa ni pamoja na utu, uzalendo, uadilifu, umoja, uwazi, uwajibikaji na lugha ya Taifa, lakini zikaondolewa.
Kikao cha dharura CUF Zanzibar
Baadaye jana jioni, uongozi wa CUF Zanzibar ulitoa taarifa ya kuitishwa kwa kikao cha dharura, huku ikiwahakikishia wanachama wake kuwa itavuka salama kwenye msukosuko huo kama ilivyofanikiwa dhoruba nyingine.
“Katika historia yake, CUF imepita katika dhoruba na misukosuko mingi lakini mara zote imeonyesha uwezo mkubwa wa kuhimili dhoruba na misukosuko hiyo na kukabiliana na athari zake. Hatuna chembe ya wasiwasi kwamba hata mtihani huu tutauvuka na tunaamini tutaibuka tukiwa chama imara zaidi,” inaeleza taarifa ya CUF Zanzibar.
“Katibu Mkuu ameagiza kuitishwa kwa vikao vya dharura vya Kamati ya Utendaji ya Taifa na Baraza Kuu la Uongozi la Taifa siku ya Jumapili, tarehe 9 Agosti, 2015 ili kujadili hatua hiyo na kufanya uamuzi juu ya hatua muafaka zinazopaswa kuchukuliwa katika kipindi hiki hadi hapo chama kitakapomchagua mwanachama mwingine kujaza nafasi hiyo ya mwenyekiti.”
Kuondoka kwa Lipumba kunaacha nafasi mbili za juu kuwa wazi baada ya aliyekuwa makamu mwenyekiti, Juma Duni Haji kuhamia Chadema na kupitishwa kuwa mgombea mwenza wa Ukawa kutokana na makubaliano ya kimkakati ya vyama vinavyounda umoja huo. Hali hiyo inafanya kiongozi mkuu kwa sasa kuwa Katibu Mkuu, Maalim Seif Sharif Hamad ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
CUF wajibu mapigo Dar
Nusu saa baada ya kutangaza kujivua uenyekiti, uongozi wa CUF jijini Dar es Salaam uliitisha mkutano wa ghafla na wanahabari kwenye ofisi za makao makuu yake zilizoko Buguruni na kueleza kuwa kama kiongozi, Profesa Lipumba ana uhuru na haki kikatiba kujiuzulu na CUF kama taasisi bado ipo imara.
“Tunakubaliana na uamuzi wake, lakini tuwaeleze wanachama wetu na Watanzania kwa ujumla kuwa uongozi wa CUF umebaki imara na unaendelea na shughuli zake kwa kufuata taratibu zote na vikao vyetu vitaendelea kama kawaida. Bado katibu mkuu yupo na viongozi wengine wapo,” alisema mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa CUF, Mustafa Wandwi.
Aliwatoa hofu makada wanaogombea ubunge na udiwani akiwataka waendelee na mikakati yao ya uchaguzi kwa sababu uamuzi wa kugombea umebarikiwa na Baraza Kuu la Uongozi na hakuna mfarakano wowote ndani ya chama.
Alipoulizwa kuhusu kauli ya Profesa Lipumba kuwa Ukawa imevunja misingi na maadili wanayoiamini, alisema:
“Yeye alikuwa kiongozi wetu mkuu na aliridhia mengi kama kiongozi wa chama na yapo maandishi yanayoonyesha tulivyoridhia ndani ya Ukawa na tunaendelea vizuri bila tatizo lolote katika umoja huo.
“Kama amegundua udhaifu huo sasa, anaujua yeye kama kiongozi na mwanachama. Sisi hajatupatia taarifa rasmi katika kikao cha aina yoyote na siwezi kuyazungumzia kwa sababu kama chama hatujajadili hayo na tukijadili tutatoa maelezo.”
CUF bila Lipumba
Wakati uongozi ukieleza hayo, makada waliokuwa makao makuu ya CUF walikuwa katika makundi wakijadili kung’atuka kwa Profesa Lipumba huku wengi wakisema “CUF bila Lipumba inawezekana”.
Ili kuondoa simanzi na taharuki, walianza kushawishiana kuimba nyimbo za hamasa zikiwamo za “tuna imani na Ukawa, hoyaa, hoyaaa…tuna imani na Lowassa hoyaa, hoyaaa” na kuchagiza pia salamu ya maarufu ya CUF ya “CCM kwisha kwisha kwisha kabisa, mlalo wa chali, kifo cha mende, kwisha kabisa”.
“Taarifa za kujiuzulu imetushtua sana, mheshimiwa hakutumia hekima na busara,” alisema katibu wa vijana Kata ya Magomeni, Salim Mzee. Jana (juzi) wazee na viongozi wa dini walimwita kujadiliana lakini inaonekana alikuwa na chuki katika nafsi yake na kama kulikuwa na tatizo ndani ya Ukawa angetuita tukajadiliana lakini kama wana-CUF hatutatoka ndani ya Ukawa na tutajenga chama kuhakisha tunaing’oa CCM,” aliongeza.
Licha ya Profesa Lipumba kueleza kuondoka kwake hakuhusiani na kupatiwa mamilioni ya fedha kuvuruga Ukawa, kada Abdallah Mohamed alisema kuondoka kwa Lipumba siyo bure kuna mkono wa CCM.
“Juzi tu alikuwa akitoa kauli za wazi mbele ya vyombo vya habari kuhusu kuunganisha nguvu ya Lowassa na Ukawa CCM chali, chali, mlalo wa mende, sasa kwa hapa nani kawa mlalo wa mende?
Chadema walonga
Mwanasheria mkuu wa Chadema, Tundu Lissu alisema hatua ya Profesa Lipumba kujiuzulu ni sawa na jenerali wa jeshi aliyeanguka katikati ya mapambano ya kuelekea Ikulu na harakati za mageuzi na mabadiliko alizoanza miaka 20 iliyopita.
Akizungumza nje ya Hoteli ya Ledger Bahari Beach kilipofanyika kikao cha Kamati Kuu ya Chadema jana, Lissu alisema katika mapambano kuna majenarali na askari wa kawaida, lakini Profesa Lipumba ni sawa na jenerali aliyeanguka katikati ya uwanja wa mapambano ya mabadiliko.
Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake la chama hicho (Bawacha), Halima Mdee alisema Profesa Lipumba alikuwa kikwazo katika maamuzi ya Ukawa.
“Sishangai kwa sababu tulikuwa tunajua kuwa yeye ndiyo kikwazo cha Ukawa tangu mwanzo wa vikao vyetu. Alikuwa na sababu nyingi, akimaliza hii anaibua nyingine,” alisema Mdee.
Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa alimfananisha Profesa Lipumba na abiria wa treni anayeamua kushukia njiani kabla hajafika anakokwenda.

Chenge akiri kupokea Sh1.6 bilioni

Dar es Salaam. Mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge amekiri mbele ya Baraza la Maadili kupokea Sh1.6 bilioni kutoka Kampuni ya VIP Enginering and Marketing Limited, zikiwa ni malipo ya kutoa ushauri.
Pia, alihoji kama kuna tatizo kutumia taaluma yake ya sheria kuzishauri kampuni binafsi na kujipatia fedha.
Chenge ambaye alitoa utetezi wake jana saa 7:30 mchana, alisema hakulipwa fedha hizo kwa sababu ni kiongozi wa umma, bali kwa kutoa ushauri.
Alisema aliingia mkataba na kampuni hiyo wa kutoa ushauri wa kisheria dhidi ya Kampuni ya Mechmer ambazo ni kampuni binafsi zilizokuwa na mgogoro.
“Nawashangaa mnalalamika Chenge kulipwa na Kampuni ya VIP au wamewafuata na kulalamika kwamba hayakuwa malipo halali,” alihoji.
Alisema hakuna kufungu cha sheria kinachomzuia kutoa ushauri wa kisheria kwa kampuni binafsi.
Kuhusu malalamiko kwamba akiwa Mwanasheria wa Serikali aliishauri kuingia mkataba wa kuuziana umeme kati ya Kampuni ya IPTL na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), Chenge alisema anawashangaa wanasheria wa sekretarieti kwa malalamiko hayo.
“Sikuishauri Serikali kuingia mkataba na IPTL bali ofisi yangu ndiyo iliyotoa ushauri kisheria. Nakubaliana na walalamikaji kwamba mwaka 1995 nilikuwa mwanasheria wa Serikali, lakini sikubaliani na madai yao.”
Alisema Ofisi ya Mwanasheria wa Serikali ilitoa ushauri huo kwa sababu ndiyo jukumu lake.
“Wanasheria ni lazima wafahamu kwamba ile ni taasisi na siyo mtu kama Chenge,” alisema.
Alisema ofisi yake ilitoa ushauri wa mikataba mitatu ya IPTL na Serikali kwa lengo la kuongeza umeme hasa kutokana na ukame uliolikumba Taifa.
“Naomba baraza lako liyapuuze kwa dharua zote na kuyatupilia mbali malalamiko ya sekretarieti kwa sababu hayawezi kukusaidia kutoa uamuzi ulio sahihi,” alisema.
Kuhusu kutumia taarifa alizozipata akiwa mwanasheria wa Serikali na kuzitumia kwa masilahi binafsi, Chenge alisema: “Naomba wachanganue taarifa hizo ni zipi kwa sababu huwezi kumlalamikia mtu kwa jumla lakini kwenye malalamiko husemi.
Shahidi wa mlalamikaji, Waziri Kipacha alisema Chenge akiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) mwaka 1995, aliishauri Serikali kuingia mkataba wa miaka 20 na IPTL.
Alisema baada ya kustaafu mwaka 2005 aliingia mkataba wa kuwa mshauri mwelekezi wa kampuni hiyo iliyokuwa inamiliki asilimia 30 ya hisa za IPTL.
Alisema kitendo cha kuingia mkataba na VIP ni ukiukwaji wa Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.