Friday, August 7

Chenge akiri kupokea Sh1.6 bilioni

Dar es Salaam. Mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge amekiri mbele ya Baraza la Maadili kupokea Sh1.6 bilioni kutoka Kampuni ya VIP Enginering and Marketing Limited, zikiwa ni malipo ya kutoa ushauri.
Pia, alihoji kama kuna tatizo kutumia taaluma yake ya sheria kuzishauri kampuni binafsi na kujipatia fedha.
Chenge ambaye alitoa utetezi wake jana saa 7:30 mchana, alisema hakulipwa fedha hizo kwa sababu ni kiongozi wa umma, bali kwa kutoa ushauri.
Alisema aliingia mkataba na kampuni hiyo wa kutoa ushauri wa kisheria dhidi ya Kampuni ya Mechmer ambazo ni kampuni binafsi zilizokuwa na mgogoro.
“Nawashangaa mnalalamika Chenge kulipwa na Kampuni ya VIP au wamewafuata na kulalamika kwamba hayakuwa malipo halali,” alihoji.
Alisema hakuna kufungu cha sheria kinachomzuia kutoa ushauri wa kisheria kwa kampuni binafsi.
Kuhusu malalamiko kwamba akiwa Mwanasheria wa Serikali aliishauri kuingia mkataba wa kuuziana umeme kati ya Kampuni ya IPTL na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), Chenge alisema anawashangaa wanasheria wa sekretarieti kwa malalamiko hayo.
“Sikuishauri Serikali kuingia mkataba na IPTL bali ofisi yangu ndiyo iliyotoa ushauri kisheria. Nakubaliana na walalamikaji kwamba mwaka 1995 nilikuwa mwanasheria wa Serikali, lakini sikubaliani na madai yao.”
Alisema Ofisi ya Mwanasheria wa Serikali ilitoa ushauri huo kwa sababu ndiyo jukumu lake.
“Wanasheria ni lazima wafahamu kwamba ile ni taasisi na siyo mtu kama Chenge,” alisema.
Alisema ofisi yake ilitoa ushauri wa mikataba mitatu ya IPTL na Serikali kwa lengo la kuongeza umeme hasa kutokana na ukame uliolikumba Taifa.
“Naomba baraza lako liyapuuze kwa dharua zote na kuyatupilia mbali malalamiko ya sekretarieti kwa sababu hayawezi kukusaidia kutoa uamuzi ulio sahihi,” alisema.
Kuhusu kutumia taarifa alizozipata akiwa mwanasheria wa Serikali na kuzitumia kwa masilahi binafsi, Chenge alisema: “Naomba wachanganue taarifa hizo ni zipi kwa sababu huwezi kumlalamikia mtu kwa jumla lakini kwenye malalamiko husemi.
Shahidi wa mlalamikaji, Waziri Kipacha alisema Chenge akiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) mwaka 1995, aliishauri Serikali kuingia mkataba wa miaka 20 na IPTL.
Alisema baada ya kustaafu mwaka 2005 aliingia mkataba wa kuwa mshauri mwelekezi wa kampuni hiyo iliyokuwa inamiliki asilimia 30 ya hisa za IPTL.
Alisema kitendo cha kuingia mkataba na VIP ni ukiukwaji wa Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.

No comments:

Post a Comment