Friday, October 6

Mpinzani wa Kagame Diane Rwigara afikishwa mahakamani Rwanda

Rwigara alifikishwa mahakamani akiwa amefungwa pingu
Mwanasiasa wa upinzani nchini Rwanda Diane Rwigara, mamake na dadake wamdefikishwa mahakamani mjini Kigali kwa mara ya kwanza wiki mbili baada ya kuzuiliwa na polisi.
Watatu hao wameshitakiwa kuchochea uasi nchini, mashtaka wanayokanusha wakisema yana misingi ya kisiasa.
Diane Rwigara alizuiwa kugombea kiti cha urais katika uchaguzi uliofanyika mwezi wa 8 mwaka huu ambapo Rais Paul Kagame alishinda kwa asilimia 98 ya kura.
Mwandishi wa BBC Yves Bucyana mjini Kigali anasema chumba cha mahakama kilikuwa kimejaa watu wengi miongoni mwao wanadiplomasia wa baadhi ya nchi za Magharibi na Marekani.
Ulinzi ukiwa umeimarishwa, watuhumiwa hao watatu waliingizwa mmoja baada ya mwingine katika chumba cha mahakama huku wakifungwa pingu.
Jaji alifungua kikao kwa kusikiliza hoja ya watuhumiwa, Diane Rwigara na Mamake Adeline Rwigara wamesema wana tatizo la kuwasiliana na mawakili wao.
Rwigara
Wamesema wameweza kuwasiliana mara moja tu kabla ya mawakili kukataliwa kuwaona tena huku Dadake Anne Rwigara yeye akisema kuwa hajapa wakili.
Wote wameomba kesi kuahirishwa ili kupata muda zaidi wa kutayarisha kesi dhidi yao.
Hoja hiyo imekubaliwa kwa kesi kuahirishwa hadi Jumatatu wiki ijayo.
Mashitaka yanayowakabili yalikuwa tayari yamewekwa hadharani na mwendeshamashtaka kabla ya wao kufikishwa mahakamani leo.Wote watatu wameshitakiwa kuchochea uasi miongoni mwa wananchi.
Zaidi ya hayo, Diane Rwigara ameshtakiwa kughushi nyaraka huku Mamake Adeilne Rwigara akishtakiwa pia kosa la kugawa wananchi kwa misingi ya kikabila.
Awali walipokuwa katika ngazi ya upelelezi wa mwanzo walishitakiwa makosa ya kutaka kuiangusha serikali na ulaghai wa kukwepa kulipa kodi, lakini makosa hayo yalifutwa.
Wote wanapinga mashitaka dhidi yao wakisema yana misingi ya kisiasa.Diane Rwigara mwenye umri wa miaka 35 alizuiliwa kugombea kiti cha urais uliofanyika mwezi wa 8 mwaka huu.
Tume ya uchaguzi ya Rwanda ilisema kwamba alifanya ulaghai katika kutafuta saini za wafuasi wake ili kutimiza matakwa ya tume hiyo.
Tangu ulipoanza mchakato huo wa kutaka kuingia ikulu,Diane Rwigara amejitokeza kama mpinzani na mkosoaji mkuu wa chama tawala RPF.
Na baada ya kukataliwa kugomea urais alianzisha vugugugu alilotaja kuwa na lengo la kupinga uonevu na kupigania haki miongoni mwa wananchi.

No comments:

Post a Comment