Saturday, August 1

Kada wa Vijana Chadema Dar auawa kwa risasi


Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Vijana Chadema Tawi la Luis, Mbezi Luis, Dar es Salaam, Dennis Kasanga ameuawa kwa kupigwa risasi shingoni usiku wa kuamkia jana, huku taarifa zilizotolewa na polisi zikitofautiana na mashuhuda wa tukio hilo.
Kasanga, mkazi wa Mbezi Luis alipigwa risasi na watu wanaodaiwa kuwa majambazi waliovamia baa inayojulikana kwa jina la Mtauli iliyopo njiapanda ya Barabara ya Goba na Makabe saa saba usiku. Hata hivyo, polisi wamesema tukio hilo halihusiani na ujambazi na wala halikutokea muda huo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, Camillius Wambura alisema jana kuwa tukio hilo lilitokea saa 10 alfajiri kuamkia jana.
Alisema tukio hilo lilitokea Barabara ya Goba baada ya watu wanne waliokuwa wakisukuma gari bovu kuvamiwa na watu wengine wanne na kuibuka mzozo kati yao.
“Baada ya mzozo, ghafla mmoja aliibuka na kuanza kuwafyatulia risasi iliyowajeruhi watu wawili na kuua  mmoja aliyepigwa risasi shingoni,” alisema Kamanda Wambura.
Kamanda Wambura alisema tukio hilo halihusiani na ujambazi kama watu wanavyodai. “Siyo kila mtu anayefyatua risasi ni jambazi, subiri kwanza tunaendelea na uchunguzi wa tukio.”
Hata hivyo, mashuhuda wa tukio hilo walidai kuwa marehemu aliuawa kwa kupigwa risasi na majambazi, ambao pia waliwajeruhi watu wengine wawili akiwamo mlinzi wa baa hiyo.
Mbali na kujeruhi, watu waliokuwa na bastola, mapanga na marungu pia waliwapora simu na fedha wateja wachache waliokuwapo kwenye baa hiyo.
Kati ya waliojeruhiwa, mmoja ni mlinzi aliyepigwa rungu usoni na mwingine aitwaye Erasmo Basheja, mkazi wa eneo la Basondole aliyepigwa risasi begani.
Mhudumu mmoja wa baa hiyo aliyekataa kutaja jina lake, aliliambia gazeti hili jana kuwa watu kati ya sita au saba walifika kwenye baa hiyo saa saba usiku wakijifanya wateja waliotaka kuhudumiwa vinywaji.
Alisema wakati wakifika, baa ilishafungwa ila kulikuwa na wateja wachache nje na yeye muda huo alikuwa ndani. “Baa ilishafungwa zamani, ila kulikuwa na wateja wachache nje wakimalizia vinywaji,” alisema shuhuda huyo.
Alisema baada ya watu hao kuelezwa kuwa baa imeshafungwa, ghafla walibadilika na kuwataka watu waliokuwa hapo kulala chini na wakaanza kuwapekua mifukoni na kupora simu zao.
“Nilisikia mlio wa risasi na haraka haraka nilifunga mlango wa kuingia kaunta ya vinywaji kisha nikalala uvunguni kwenye chumba kinachotumia mlango mmoja na kaunta,” alisema shuhuda huyo.
Aliongeza: “Niliwasikia wale majambazi wakisema, ‘hawa wanawake wameshafunga geti.’ Nilikaa kimya nikiwa nimejilaza chini ya godoro.”
Alisema majambazi hao wanaijua fika baa hiyo, kwani baada ya kuwalaza watu chini walizunguka nyuma, ambako ndiko kwenye geti la kuingia kaunta na vyumba vya ndani.
Mlinzi wa baa hiyo, ambaye amejeruhiwa usoni kwa kupigwa na rungu aliiambia gazeti hili kuwa majambazi hao walifika kwenye baa hiyo saa saba usiku wakati tayari pameshafungwa.
Alisema alikuwa amekaa kaunta pamoja na marehemu na mtu mwingine ambaye hakumbuki jina lake, ndipo aliposikia mlio wa risasi na wakati akitaharuki, alivamiwa na mmoja wa watu hao na kupigwa rungu usoni huku akisema: “Usiniangalie usoni.”
“Nilidondoka chini na wakaanza kunisachi mifukoni huku wakinitaka kutoa simu na fedha, niliwajibu sina kitu na baada ya kunipiga niliamua kutoa simu na kuwapa,” alisema mlinzi huyo.
Alisema marehemu alipigwa risasi wakati akiondoka alipoketi na kwenda sehemu ambayo alisikia mlio wa risasi. “Alikuwa kaunta na baada ya mlio wa risasi alinyanyuka na kwenda sehemu ya nje ya baa huko ndiko alikopigwa risasi na kufariki dunia papo hapo,” alisema.
Kifo cha kiongozi huyo wa vijana Chadema pia kimethibitishwa na mjumbe wa Serikali ya Mtaa wa Luis, Finna Massawe.
Majirani wa eneo ilipo baa hiyo walidai kuwa baa hiyo imekuwa ikivamiwa na majambazi, mara kwa mara, na kwamba ingawa tukio la kuuawa mtu ni mara ya kwanza kutokea, lakini tayari uhalifu wa kuvamiwa baa hiyo ulishafanyika mara mbili.

No comments:

Post a Comment