Saturday, August 8

NEC: Marufuku kutoa kadi ya kupigia kura

Mwenyekiti wa NEC, Jaji mstaafu Damian Lubuva 

Dar es Salaam. Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), imeonya kwamba mtu yoyote haruhusiwi kutoa kadi yake ya kupigakura au taarifa za kadi hiyo kwa ndugu, jamaa au mwajiri wake.
NEC imetoa onyo hilo wakati tayari kukiwa na tetesi kuwa baadhi ya wafanyakazi wa umma wakiwamo polisi, wanajeshi na askari magereza, wametakiwa kukabidhi kadi zao kwa viongozi wao wa ngazi za juu.
Wakati hayo yakisemwa, Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Bara, John Mnyika jana aliitisha mkutano wa vyombo vya habari akidai kuna tetesi serikali imeviagiza vyombo vya usalama, kupeleka namba za vitambulisho vya askari wote kwa wakuu wa vitengo jambo ambalo ni kunyume na utaratibu
Mkurugenzi wa Uchaguzi wa NEC, Kailima Kombwey alitoa angalizo juu ya hilo na kusema kuwa kwa mujibu wa Sheria ya Uchaguzi ambayo inazungumzia Daftari la Kudumu la Wapigakura, hairuhusiwi na haitakiwi kwa mtu asiyehusika na kadi ya mpigakura kuimiliki kadi hiyo.
Kombwey alisema hakuna sheria yoyote inayomlazimisha mtumishi wa umma kutoa kadi yake ya kupigiakura kwa mwajiri wake.
Akizungumzia suala hilo, Msemaji wa JWTZ, Kanali Ngemela Lubinga alisema taarifa hizo ni za uongo na hazina ukweli wowote kuwa wanajeshi wameombwa nambari za vitambulisho.
Msemaji wa Polisi, Advera Bulimba alipopigiwa simu kuhusu madai hayo, alisema hana hizo taarifa.
Ofisa Mawasiliano wa Magereza, Deodatus Kazinja alisema hizo ni tetesi na wala hazina ukweli wowote.
*Imeandikwa na Hussein Issa na Florid Mapunda, Suzan Mwillo

No comments:

Post a Comment