Saturday, August 8

‘Lipumba angetaka ningemwachia urais’

Profesa Ibrahimu Lipumba 
Dar es Salaam. Mgombea urais kupitia tiketi ya Chama cha Alliance for Democratic Change (ADC) Chifu Lutalosa Yemba, amemkaribisha aliyekuwa Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba kujiunga na chama hicho.
Chama hicho juzi kilifanya mkutano wa kuwatambulisha wagombea wake wa nafasi ya urais, Yemba anayewania urais wa muungano na mgombea mwenza wake Said Miraj Abdullah, pia alitambulishwa Hamad Rashid Mohamed, anayewania urasi wa Zanzibar.
Yemba kwenye mkutano huo alisema anaufahamu uwezo wa Lipumba katika siasa, ujasiri na uvumilivu wake, hivyo hatakuwa na kinyongo kufanya naye kazi ya kusukuma mbele gurudumu la siasa za upinzani.
Alisema hakujiunga na chama hicho kwa ajili ya kuwa rais, amejiunga kwa ajili ya kutengeneza dola ya uongozi itakayoondoa dhiki na mateso wanayopata Watanzania, hivyo kutokana na uzowefu alionao katika siasa anaamini watafanikisha hilo kwa ufanisi.
“Walinifukuza mwezi wa sita , mwezi wa nane Lipumba amejing’atua kwenye uongozi, watafahamu sasa kuwa kwenye chama kile kuna udhalimu, namkaribisha Lipumba na ninampongeza kwa uvumilivu wake, ingawa ninaumia kuona kiongozi shupavu aliyekuwa na uwezo wa kuhakikisha wananchi wanaamini katika vyama vingine vya upinzani kukatishwa tamaa na watu wachache wenye uroho wa madaraka, ”alisema Yemba.
Alisema kuwa anaingia katika kinyang’anyiro cha kuwania urais akipambana na chama kimoja tu, CCM, hivyo vilivyobaki hakuna wa kumtisha kwa sababu wenyewe kwa wenyewe wameanza kuvurugana.
“Sisi ADC kama bahari, tunachukua maovu yao tunameza, baadaye tunayatema, wakati ukifika wa kufanya hivyo tutafanya kwa sasa , nawaomba Watanzania mpime kwa makini na kuchagua kiongozi anayefaa.
“Mchagueni asiyekuwa mwizi, fisadi, mnyang’anyi asiye na kashfa na hakuna unapoweza kumpata kiongozi wa namna hiyo zaidi ya ADC, pimeni sikilizeni sera zetu, ilani yetu mtuunge mkono. ”alisema Yemba.
Jana, Yemba alichukua fomu za kuwania urais wa chama hicho, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), huku akiwasisitiza Watanzania kukipa nafasi chama hicho ili kuifanyia nchi mabadiliko ya haki na kuondokana na ukandamizaji.
Kabla ya kufikia uamuzi wa kuchukua fomu Nec, Yemba alinukuliwa akisema kama Lipumba angejitokeza jana, angemwachia nafasi ya kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano. Hata hivyo kuna taarifa Lipumba alisafiri juzi usiku kwenda nje ya nchi.
Said Miraj Abdulla
Kwa upande wa mgombea mwenza wa chama hicho Said Miraj Abdulla, alisema kuwa anamualika Maalim Seif awaeleze Watanzania anataka nini katika siasa, kwa nini anavuruga utaratibu wa kuwapo kwa upinzani wa kweli.
Alieleza kuwa pamoja na kuunga mkono kilichofanywa na Lipumba kutokana na udhalimu unaofanywa na wanasiasa wachache wanaokatisha tamaa wengine, lakini hafurahi kumuona au kusikia anakaa nje ya ulingo wa siasa.
“Nani asiyejua mchango wa Lipumba katika siasa za upinzani wa nchi, arudi kwenye siasa aje kuendeleza safari aliyoianza mwaka 1995, kukaa kwake nje ya siasa kunapunguza nguvu ya Watanzania kufikia kilele cha mafanikio ya kupata rais atakayejali shida zao, kuwasikiliza, kuwanufaisha na rasilimali zinazopatikana nchini mwao, ”alisema Abdulla.
Hamad Rashid Mohamed
Kwa upande wa mgombea urais wa Zanzibar, Hamad Rashid Mohamed, aliwataka wananchi kuwa makini wanaposhabikia vyama na kuviepuka visivyoheshimu Katiba.
Alisema alipokuwa kwenye Bunge la Katiba alisema hakuna upawa wala Ukawa, matokeo yake ndiyo hayo watu wanalumbana, Wazanzibar wanahitaji mabadiliko wamekaa kwenye umasikini usiowahusu kwa sababu hakuna ajira.
Alieleza kuwa kwa wakazi wa Zanzibar wanaohitaji ajira, akijenga viwanda vitano tu hakutakuwa na kijana atakayekosa kazi na huo ndiyo mkakati wake katika miaka mitano ya uongozi.
“Watanzania shabikieni vyama huku mkiwapima wagombea wana nia gani na nyinyi, maslahi yao binafsi au kuwasaidia, maana “Tumbili akimaliza miti anakuja mwilini” kuweni makini, ”alisema.

No comments:

Post a Comment