Sunday, November 26

Njia mbili za kulea kuku bandani

Mfugaji Saria Munisi wa Bomang’ombe mkoani
Mfugaji Saria Munisi wa Bomang’ombe mkoani Kilimanjaro, akiwahudumia kuku anaowafuga katika mabanda maalumu (cages). Hii ni mojawapo ya njia mbili za kulea kuku wakiwa bandani. Picha na Clement Fumbuka 
Banda la kuku linaweza kulea kuku kwa namna nyingi. Leo tutangalia namna mfugaji anavyoweza kutumia banda kulea kuku kwa namna mbili.
Ukiondoa kanuni za ujenzi wa banda zinazoelekeza sehemu ya kujenga banda na vigezo vyake, ufugaji wa kuku kwa njia ya kisasa unafaa uzingatiwe katika matumizi ya banda.
Katika ufugaji wa kuku kwa njia ya kienyeji, kuku huenda bandani kulala wakati wa usiku, huku wakitumia muda mwingi kuzagaa nje wakitafuta chakula na maji wakati wa mchana.
Lakini ufugaji wa kuku kwa njia ya kisasa, kuku hukaa bandani muda wote wakipatiwa mahitaji yao yote bandani. Ni muhimu kuzingatia ujenzi wa banda na njia utakayotumia kulea kuku wako bandani. Faida ya ufugaji wa kuku kwa njia ya kisasa hutegemea matumizi ya banda lako.
Kulea kwenye sakafu
Njia ya kwanza katika matumizi ya banda kwa ufugaji wa kuku kwa njia ya kisasa ni kulelea kuku kwenye sakafu. Kuku kwa njia hii huishi kwenye sakafu iliyowekwa maranda au pumba ngumu ya mpunga. Kwa muda mrefu njia hii imezoeleka na inatumika mara kwa mara na ni teknolojia ya muda mrefu.
Ufanisi wake hutegemea vigezo bora vya banda kama vile nafasi ya kutosha ndani ya banda ili kuku waishi bila kubanana.
Vingine ni hewa safi na ya kutosha itakayofanya kuku wakue vizuri na kuzuia magonjwa au vifo vya mrundikano na kukosa hewa. Mwanga wa kutosha ili kuku wale na kunywa vizuri bila kuhitaji taa wakati wa mchana.
Pia, kuwapo kwa ukuta, milango, na madirisha imara ili kuzuia wizi na banda kutumika kwa muda mrefu bila kuharibika. Uelekeo sahihi wa madirisha ili kuwakinga dhidi ya mvua, jua na upepo.
Kuwe na sakafu imara iliyonyanyuliwa chini ili kuepuka kuku kuchimba mashimo ndani ya banda na hatimaye vimelea vya magonjwa kuathiri kuku mara kwa mara.
Njia ya mabanda maalumu
Njia ya pili ni ya mabanda maalumu maarufu kwa jina la ‘cages’. Kuku huwekwa kwenye banda wakiwa ndani ya waya uliotengenEzwa kwa vyuma. Waya huo unaweza kubebeshwa juu ya mwingine kitaalamu na kutengeneza mfano wa ghorofa kama makreti ya soda ndani ya banda.
Katika teknolojia hii, kuku huwa wasafi muda wote kutokana na kinyesi chao kudondoka moja kwa moja sakafuni bila kukikanyaga.
Pia, kuku hupewa chakula sehemu safi na kula chakula bila kumwaga. Mayai hutagwa na kujikusanya yenyewe sehemu moja. Njia ni bora zaidi katika kuepuka matatizo ya kuku kula mayai, kudonoana na kupatwa na magonjwa ya mara kwa mara.
Aidha, banda linaweza kulea kuku wengi mara nne hadi tano zaidi ya idadi ya kuku wanalelewa kwa njia ya kulelea kwenye sakafu.
Uzalishaji wa kuku kwa kutumia cages ni nafuu kwani mfugaji akifunga cages zake atazitumia kwa muda mrefu na gharama zake ni za kawaida kuliko kujenga banda.
Kwa mfano, mfugaji akijenga banda la kufugia kuku 100 kwa njia ya kufugia sakafuni, banda hilo hilo anaweza kufugia kuku wa mayai 450 kwa njia ya cages. Kufanya usafi kwenye banda la ‘cages’ ni rahisi kuliko kufanya usafi kwenye banda lililofugiwa kuku kwa njia ya sakafuni na kuwekwa maranda.
Mfugaji anaweza kutathmini kwa kulinganisha njia zote mbili ili kubaini tofauti zake katika gharama na faida kabla hajaamua kutumia njia mojawapo..
Ufugaji wa kuku ni biashara sawa na biashara nyingine zenye kuhitaji bidhaa iliyoboreshwa kuvutia wateja kutengeneza soko na hatimaye kuleta faida.
Katika ufugaji, ubunifu upo katika kutumia vizuri rasilimali kama chakula, maji, eneo, mtaji, utaalamu na nguvu kazi.
Matumizi mabaya au kutotumia ipasavyo rasilimali hizi ni kupoteza mapato katika biashara yako. Jambo lolote linahitaji mazingira fulani ili liende vizuri.
Ufugaji nao unahitaji kuandaliwa mazingira rafiki ili kupata mavuno mengi. Watu wengi huchukua mambo kwa historia kitu ambacho hakipaswi kuwa hivyo. Jambo zuri hutokea kutokana na usimamizi wenye kujali kila kipengele kinachohusiana na kuleta matokeo tarajiwa.
Mambo haya yaliyotajwa katika mwongozo huu wa ufugaji wa kuku ni mambo ya msingi kama tofali katika ujenzi wa nyumba.
Huwezi kujenga nyumba bila kuwa na matofali. Kadhalika huwezi kuzungumzia faida katika biashara ya ufugaji wa kuku bila kuzingatia matumizi bora ya rasilimali unazotumia kuendeshea biashara yako.
Banda la kuku ni sawa na shamba kwa mkulima. Mkulima hawezi kupanda mazao yake hewani lazima atahitaji shamba.
Kwa mfano huo mfugaji hawezi kufuga bila banda; lazima ajenge banda bora lenye vigezo kama ambavyo mkulima atatafuta shamba lenye rutuba nzuri ili kupata mavuno mengi.
Kuna aina nyingi za matumizi ya banda kulingana na mfumo aliojiandalia mfugaji. Banda linaweza kutumika kulingana na ubunifu wa mfugaji. Mabanda mengi hujengwa kulingana na mipango ya mfugaji.
Ramani ya banda na malighafi iliyotumika kujengea vina maana kubwa sana katika uzalishaji wa kuku. Mazingira ni kitu muhimu cha kutazamwa hasa mfugaji anapotaka kuchagua njia ya ufugaji wake.
Kwa kuwa faida ni kipaumbele cha mambo yote, kila kitu kifanyike kwa kulenga faida. Biashara yoyote inalenga kupata faida, ndiyo maana mfugaji anashauriwa kuwa na mazingira yenye kuleta faida katika biashara yake.
Mfugaji ahusishe wataalamu katika kubuni ramani ya mradi wake ili kuepuka gharama zinazoweza kuepukika.

No comments:

Post a Comment