Thursday, November 23

Manispaa Ilala yajipanga kutoa huduma ya afya bure

Dar es Salaam. Ili kukabiliana na changamoto ya msongamano wa watu wanaojitokeza kupata huduma za bure za afya, Halmashauri ya Manispaa ya Ilala mwakani itatenga fedha kwa ajili ya kuziwezesha zahanati kutoa huduma za vipimo bure mara moja kwa mwezi.
Mganga Mkuu wa Manispaa ya Ilala, Victorina Ludovick amesema hayo leo Alhamisi Novemba 23,2017 kwenye mkutano wa baraza la madiwani alipojibu swali la diwani wa Kata ya Mzinga, Isack Job.
Diwani Job alitaka kufahamu mipango ya halmashauri katika kuboresha huduma za afya ili kupunguza idadi ya wanaojitokeza kwenye huduma za bure.
Job ametoa mfano wa upimaji wa afya bure uliofanyika miezi michache iliyopita katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam na unaoendelea sasa katika meli kutoka nchini China.
Dk Ludovick amesema katika utafiti waliofanya imebainika watu wengi wanafuata huduma za bure za afya kwa kuwa wanashindwa kwenda kufanya vipimo  hospitalini kutokana na gharama kubwa.
Akifungua kikao, Naibu Meya wa Manispaa ya Ilala, Omari Kumbilamoto amewaeleza wajumbe kuwa, meya Charles Kuyeko anaugua na amekwenda kupata huduma kwenye meli ya China.

No comments:

Post a Comment