Thursday, November 23

Katambi ataka tuhuma dhidi yake zithibitishwe

Aliyekuwa mwenyekiti wa Baraza la Vijana la
Aliyekuwa mwenyekiti wa Baraza la Vijana la Chadema (Bavicha), Patrobas Katambi 
Dar es Salaam. Aliyekuwa mwenyekiti wa Baraza la Vijana la Chadema (Bavicha), Patrobas Katambi amewataka viongozi wakuu wa Chadema kuthibitisha tuhuma za kununuliwa kwake na CCM la sivyo atatoa sababu za kina za uamuzi wa kuhama chama hicho.
Katambi Jumanne Novemba 21,2017 alitangaza kujiunga CCM katika mkutano wa Halmashauri Kuu ya CCM uliofanyika Ikulu, Dar es Salaam akidai upinzani hauna dhamira ya dhati ya kupambana na ufisadi.
Akizungumza na Mwananchi  leo Alhamisi Novemba 23,2017, Katambi amesema, “Inaniuma kuona nazushiwa uongo, natishwa kwa uamuzi wangu, nilikaa kimya kulinda staha za watu, nimetoa muda  wathibitishe wanachokisema.”
Amesema, “Unajua hekima na busara zangu zilinilazimisha kuondoka Chadema na kuhamia CCM bila kufafanua yaliyonitoa ili kuacha haiba yao waendelee kwa amani na mfumo wao wa siasa mpya, lakini wameshindwa sasa nitasema ukweli kama watashindwa kudhibitisha hadharani.” Katambi amesema hakukurupuka kufikia uamuzi wa kuondoka Chadema na wala hakuwashirikisha wazazi wake, kwa hiyo anayepaswa kulaumiwa au kutishwa ni yeye si wazazi au mke wake.


“Nimekuwa nikipokea vitisho vya kila aina, wazazi wangu na mke wangu, niseme tu kwamba mlinzi wa kwanza wa maisha yangu ni Mungu. Namwachia Mungu maisha yangu niliyoyatoa katika ukweli kwa faida ya Watanzania,” amesema.
Amesema kama watashindwa kutoka hadharani kukanusha taarifa hizo, ataitisha mkutano na waandishi wa habari na kusema ukweli wa kile kilichomfanya akaondoka Chadema.
Jana Jumatano Novemba 22,2017 Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe akizungumza naMwananchi alisema Katambi hakuondoka hivihivi bali kuna hila ilifanyika ambayo ilitumia saa 48 kukamilisha mchakato na kujiondoa.
"Badala ya nguvu na fedha kuzielekeza kujenga viwanda wao nguvu wamezielekeza kushawishi viongozi wetu, wamewashawishi wengi na Katambi ni miongoni ingawa wengine wamekataa."

No comments:

Post a Comment