Friday, April 6

Msukuma ataka la saba warudishwe kazini

Mbunge wa Geita Vijijni, (CCM) Joseph Msukuma ameitaka Serikali kuwarudisha kazini watumishi wa umma waliofukuzwa kwa kuwa wana elimu ya darasa la saba hadi watakapostaafu.
Msukuma ameyasema hayo leo alipokuwa akichangia hotuba ya bajeti ya ofisi ya Waziri Mkuu kwa mwaka wa fedha 2018/19.
“Wabunge wenzangu, tuwatake Serikali wawarudishe kazini hadi hapo watakapostaafu. Hapa bungeni wabunge kama 100 hivi ni darasa la saba, wengine wamefeli, wengine wana vyeti feki,” amesema.
Amesema iwapo hawatawarejesha watumishi hao basi wawafukuze hata wabunge ambao wana elimu hiyo au wabunge hao warejeshwe kuwa wa viti maalum.
Kadhalika Msukuma ameitaka Serikali kuunda tume ya kuchunguza operesheni uvuvi haramu ili kubaini ukiukwaji wa haki za uvuvi unaofanywa kutokana na operesheni hiyo.
Amesema katika operesheni hiyo kuna mtu alitozwa Sh2milioni lakini risiti yake ikaandikwa ni ya mwaka 2015.
“Serikali iunde tume ichunguze hili jambo, operesheni uvuvi haramu? Kuna mvuvi anatozwa Sh2 milioni lakini anaandikiwa risiti ya 2015,” amesema.
Amesema kuna wakurugenzi wamewatumia watumishi katika operesheni hiyo ambao hukusanya fedha na ndiyo maana anaiomba Serikali kuunda tume.

No comments:

Post a Comment