Friday, April 6

Bashe afunguka

Mbunge wa Nzega Mjini (CCM), Hussein Bashe ameiomba Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na Ofisi ya Waziri Mkuu kuanzisha chombo huru cha kuchunguza matukio mbalimbali nchini, yakiwemo ya mauaji.
Bashe ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Aprili 6, 2018 wakati akichangia mjadala wa bajeti ya ofisi ya Waziri Mkuu bungeni mjini Dodoma.
“Yapo mambo yanaanza kutokea katika nchini yetu yanaashiria kuanza kuwepo kwa mgawanyiko. Mambo haya tukiendelea kuyatizama kwa macho, hayaleti taswira njema huko mbele na wala hayataweza kulifanya Taifa hili kuwa moja wala kupambana na adui mkubwa ambaye ni umasikini,”amesema.
“Yanatokea matukio ya kusikitisha katika nchi yetu, ambayo ukitazama huoni any consign ya deliberate effort ambayo itawajengea Watanzania imani kwamba hata mimi mdogo nikikumbwa na dhahama yupo anayenilinda.”
Huku akitolea mfano tukio la kijana Allan Mapunda, aliyefariki dunia hivi karibuni mkoani Mbeya ikidaiwa sababu ni kipigo, Bashe amesema, “Naiomba Serikali kwa heshima kabisa, matukio ya namna hii yakiendelea kujengeka katika nchi yetu na  kuanzisha utamaduni ya kutowajibika yanaharibu amani.”
“Kijana huyu amekufa, ripoti ya daktari mkuu wa Hospitali ya Rufaa Mbeya inasema amefariki kwa majeraha ya ndani ya mwili wake. Familia yake imesema waliompiga ni polisi, RPC wa Mbeya (kamanda wa polisi) amesema hawahusiki, matokeo yake Serikali imeenda kutoa rambirambi ya Sh200,000.”
Amesema ndio maana matukio ya aina hiyo yameendelea kuwepo na kushauri kuwepo kwa chombo huru  kwa ajili ya kufanya uchunguzi wa matukio ya aina hiyo.
“Hatuwezi kuacha hii,  utamaduni wa kutojali kuendelea  katika nchi yetu si nzuri na ni jambo la kusikitisha maana unaharibu taswira na hii ndio inatumika na watu wasiopenda nchi yetu kuendelea kuharibu heshima ya Taifa,”amesema.

No comments:

Post a Comment