Thursday, September 5

Katiba moto, Chadema, CUF watoka nje

Dodoma.Wabunge wa Kambi ya Upinzani Bungeni jana jioni walitoka ndani ya Ukumbi wa Bunge, baada ya kupuuzwa kwa mwongozo wao wa kutaka kuahirishwa kujadiliwa kwa Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, hadi hapo Zanzibar itakaposhirikishwa.
Wabunge waliotoka bungeni jana yapata saa 12.15 ni kutoka vyama vya Chadema, CUF na NCCR- Mageuzi huku Mbunge wa Vunjo na Mwenyekiti wa Taifa wa Tanzania Labour Party (TLP, Augustine Mrema akiendelea kubaki ukumbini.
Kitendo cha wabunge hao wa upinzani kilionekana kuwakera baadhi ya wabunge wa CCM, ambao walisikika wakiwakejeli kwa kupiga meza huku wakisema: “Kwendeni zenu, tumewazoea.”
Wakati wabunge hao wakiondoka, Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai, alikuwa akiwasisitiza wabunge wanaobakia wawe watulivu, maana kuna usalama wa kutosha ndani ya ukumbi huo.
“Mnaotoka nimewaona wote na mnanijua,” alisikika Naibu Spika Ndugai akiwatahadharisha wabunge wa upinzani waliosusa mjadala huo.
Wabunge wa CCM waliendeleza vituko ambapo baada ya wapinzani kutoka, wabunge Juma Nkamia (Kondoa Kusini), Hilary Aeshi ( Sumbawanga Mjini) na Murtaza Mangungu (Kilwa Kaskazini) walikwenda kukaa katika viti vya kambi ya upinzani.
Kabla ya kutoka kwa wabunge hao wabunge wawili kutoka CUF waliomba mwongozo wa Spika, wakitaka muswada huo kuondolewa ili kuwapa nafasi Wanzanzibar kutoa maoni yao.
Mbunge wa Mkanyageni, Habib Mohamed Mnyaa (CUF) aliomba mwongozo akitaka muswada huo uondolewe, hadi hapo Wazanzibar watakaposikilizwa.
Alisema kuwa kwa maoni ya Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala wamesikiliza maoni ya wadau wengi, lakini Zanzibar hawakwenda kuwasikiliza wadau wa eneo hilo.
“Na hili suala zima katika masuala ya katiba linahitaji usawa wa washirika, tunazungumza kitu kinachohusiana na Zanzibar na Tanzania Bara, ili kupata maoni ya nchi nzima kuna uhalali gani wa Bunge hili kuendelea na mjadala huu?” alihoji.
Hata hivyo, alikatizwa na kelele za Mbunge wa Viti Maalumu, Pindi Chana (CCM), ambaye alitoa taarifa kuwa Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala ilialika wajumbe mbalimbali ikiwamo Zanzibar.
“Miongoni wa wajumbe walioalikwa ni pamoja na Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi ya Zanzibar pamoja na wadau mbalimbali ambao walikuja mbele ya Katiba,” alisema Pindi ambaye pia ni Mwenyekiti wa kamati hiyo.
Mbunge wa Konde, Khatibu Said Alli (CUF), alitaka mwongozo wa Spika kuhusiana na ujumbe mfupi wa maneno ambao aliupokea ukimtisha, kutokana na kitendo chao cha kumuunga mkono Msemaji wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Tundu Lissu.
“Unashabikia mambo ya Tundu Lissu leo, endelea ila mtashughulikiwa,” aliunukuu ujumbe huo na kuongeza kuwa hafahamu umetoka kwa mbunge gani ila wahudumu wa Bunge ndio waliompelekea.
Akijibu mwongozo huo, Ndugai alisema kuwa ni miongoni mwa mambo ambayo anayachukua na kuyafanyia kazi ni suala hilo. Pia Ndugai aliomba ujumbe huo apelekewe.
“Hii ni demokrasia mara nyingi imeshatolewa miongozo, jibu linatolewa hapo hapo ama baadaye na kwa hoja zilizotolewa inakilazimu kiti kupata ushauri hapo baadaye,” alisema Ndugai.
Hata hivyo, baada ya Ndugai kutoa majibu hayo, wabunge wa upinzani waliamua kutoka ndani ya ukumbi huo.
Baada ya wabunge hao kutoka Naibu Spika Ndugai aliendelea na ratiba ya Bunge kwa kusema, jambo hilo halikupangwa kumalizika jana na kwamba litaendelea kujadiliwa hata ikibidi hadi keshokutwa.
Hata hivyo, Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, alisimama kabla ya mjadala kuendelea na kutetea hoja kuwa makundi yote yalisikilizwa tofauti na inavyodaiwa na wapinzani.
“Hata katika marekebisho ya sheria mbili hizi, mimi na Mwanasheria Mkuu wa Serikali tumekutana na viongozi wengi na mawaziri na ndiyo maana tumeahirisha Muswada wa Sheria ya Kura ya Maoni,” alisema.
Alisema, yeye (Lukuvi) alikuwa Mwenyekiti wa ujumbe uliotumwa na Rais kuitisha makundi ya siasa ambayo yalijadili muswada huo. Lukuvi alisema kuwa, pande zote zimeshiriki kikamilifu katika kutoa maoni yao, “kama hizi ni sarakasi za kisiasa mimi sijui.”
Baada ya kutoka, wabunge wa vyama vya Chadema, CUF na NCCR-Mageuzi walifanya mkutano wa pamoja kwenye Ukumbi wa Pius Msekwa. Habari kutoka ndani ya kikao hicho zinaeleza kuwa, wabunge hao walikubaliana kufanya kila njia kuhakikisha wanazuia mjadala huo leo.
Pia wabunge wa CCM nao walikutana nao mara baada ya Ndugai kuahirisha kikao cha jioni.
Lissu achafua hali ya hewa
Hotuba ya Lissu ndiyo iliyochafua hali ya hewa baada ya kuituhumu Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala kwa kutohoji watu wa Zanzibar wakati wakikusanya maoni kuhusu muswada huo.
Alisema licha ya kamati hiyo kukusanya maoni ya taasisi za kidini na za kiraia, taasisi za elimu ya juu na za kitaaluma, vyama vya siasa na asasi nyingine, lakini bado haikwenda Zanzibar kukusanya maoni ya watu wa huko.
“Wadau pekee walioshirikishwa kutoa maoni yao juu ya muswada huu ni Watanzania Bara tu. Wazanzibari hawakupatiwa fursa hiyo na hawakushirikishwa kabisa, licha ya sheria yenyewe kuwa na mambo mengi yanayoihusu Zanzibar,” alisema Lissu.
Pamoja na suala hilo, Lissu alitaka pia Rais wa Jamhuri ya Muungano aondolewe madaraka ya kuteua Wajumbe wa Bunge Maalumu wasiokuwa wabunge au wawakilishi kuwa inavuruga au kuondoa kabisa dhana ya uwakilishi wa wananchi na uhalali wa kisiasa katika mchakato wa Katiba Mpya.
Pia alipendekeza kuongezwa kwa idadi ya wajumbe ifikie 792, kwani Tanzania ina idadi ya watu milioni 45 kwa takwimu za Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012.
Lissu pia alitaka wawakilishi wa Zanzibar waongezwe bungeni, kwa Zanzibar itakuwa na wajumbe 219 kwenye Bunge lenye wajumbe 604, sawa na takriban 36% ya wajumbe wote. Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inataka idadi iwe nusu kwa nusu kati ya pande mbili za Muungano.
Wajumbe 166
Kutakuwa na wajumbe 166 wasiotokana na Bunge na Baraza la Wawakilishi watateuliwa na Rais. Kutakuwa na Wabunge 357 na Wawakilishi 81 na kufanya Bunge Maalumu kuwa na jumla ya wajumbe 604.
Chikawe asoma muswada
Mapema akisoma muswada huo, Waziri wa Sheria na Katiba, Mathias Chikawe alisema Rais atakaribisha makundi mbalimbali kuwasilisha majina yasiyozidi matatu kila kundi ambao watateuliwa kama wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba. Alisema pia Kifungu cha 27 (2) kitatoa fursa kwa uhuru wa maoni katika mijadala ya Bunge Maalumu na maoni hayo hayatahojiwa mahakamani au sehemu yoyote nje ya Bunge Maalumu.
Chikawe alisema Bunge Maalumu la Katiba litakaa kwa siku 70 mfululizo jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kujadili rasimu hiyo. Hicho kitakuwa kikao kirefu zaidi cha Bunge kuwahi kukaa nchini Tanzania.
“Kutokana na unyeti wa suala lenyewe muswada huo unampa nguvu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuongeza siku 20 ili kujadili katiba,” aliongeza Chikawe.
Imeandikwa na Daniel Mjema na Sharon Sauwa - mwananchi 

Breaking news: Freeman Mbowe atimuliwa bungeni

Kiongozi wa kambi rasmi ya Upinzani Bungeni Mh Mbowe ametolewa nje ya Bunge, baada ya kukaidi amri ya Naibu spika Mh Ndugai alipomwamuru akae na Mh Mbowe kutokutii amri hiyo. 

Mh ngudai aliamuru askari wa Bunge kumtoa nje, hata hivyo baadaye wabunge karibu wote wa upinzani walitoka pia isipokuwa Mh. Augustin Mrema wa TLP. 

Upinzani Bungeni unadai muswada wa katiba 2013 unamapungufu.

Wednesday, September 4

‘Mvua za Lowassa’ zagonganisha mawaziri

Dodoma.Suala la mvua za kutengeneza kutoka nchi ya Thailand maarufu kwa jina la ‘Mvua za Lowassa’ liliwagonganisha mawaziri wawili wa Serikali bungeni jana.

Ubishi mkali ulizuka baina ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mazingira, Dk Terezya Huvisa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi waliokuwa wakivutana juu ya ukweli kuhusu teknolojia hiyo.

Wakati Waziri Huvisa akisema kwamba hakuna utaalamu wa aina hiyo, Lukuvi alisimamia kumpinga na kusisitiza kuwa jambo hilo lipo.

Suala la mvua hizo lililetwa nchini na aliyekuwa Waziri Mkuu Edward Lowassa mwaka 2007, baada ya kufanya ziara Thailand ambako alivutiwa na utaalamu wa kutengeneza mvua na kuahidi kuuleta nchini.

Kutokana na mvutano wa mawaziri hao, Lowassa ambaye pia ni Mbunge wa Monduli (CCM), alipewa dakika moja na Mwenyekiti wa Bunge, Jenister Mhagama kutoa ufafanuzi ambapo aliunga mkono hoja ya Lukuvi.

Malumbano hayo yalisababishwa na swali la nyongeza la Mbunge wa Viti Maalumu (Chadema), Susan Lyimo ambaye alihoji mpango wa kutengeneza mvua ulipoishia kwa kuwa Serikali imekuwa kimya.

“Sasa ni miaka takriban sita au saba tangu Serikali ilipokuja na mpango wa kutengeneza mvua ambao iliuchukua kutoka nchi za wenzetu, mpango huo umefikia wapi?” aliuliza.

Akijibu swali hilo, Waziri Huvisa alisema: “Mimi ni Rais wa Mazingira wa Afrika, nasema hakuna kitu kama hicho, si Marekani wala Malaysia ambao wanaweza kutengeneza mvua, hayo ni mabadiliko ya tabianchi tu.”

Waziri Lukuvi alionyesha kutokuridhishwa majibu hayo, ndipo aliposimama kutoa ufafanuzi na kusema Lowassa alikwenda Thailand ambako kuna utaalamu huo na kusisitiza kwamba upo na bado unaendelea kutumika hata Ujerumani wanakotumia mitambo ya kijeshi kusambaratisha mawingu.

Alisema kilichokwamisha mpango huo nchini ni ufinyu wa bajeti ya Serikali.

Baada ya majibu hayo, Lowassa alisimama akitaka kutetea wazo lake. Hata hivyo, kabla ya kumruhusu, Mhagama alimwomba akae chini kwanza ili atoe maelekezo.

“Mheshimiwa Lowassa, yeye siyo waziri na hivyo hastahili kutoa majibu ya Serikali, lakini kwa kutumia kanuni zetu bungeni kuhusu kutengeneza utaratibu mzuri wa kuongoza Bunge, naomba Lowassa usimame sasa walau kwa dakika moja au mbili utoe ufafanuzi,” alisema Mhagama.

Aliposimama Lowassa alizungumza kwa ufupi; “Nakushukuru Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka kukazia tu kuwa jibu lililotolewa na Mheshimiwa Lukuvi ndilo jibu sahihi.”

Majibu hayo yalisababisha Bunge kulipuka kwa shangwe.

Mara baada ya majibu ya Lowassa, Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Christopher Chiza naye alisimama akitaka kutoa maelezo. Hata hivyo, Mhagama alisema inatosha na kuwaagiza mawaziri hao kukutana kuliangalia jambo hilo badala ya kuwa na majibu kinzani.

Awali, katika swali la msingi, Mbunge wa Viti Maalumu (Chadema), Rachel Mashishanga alitaka kujua ni kwa nini Serikali isirasimishe utaalamu wa kuleta mvua kutoka kwa waganga wa jadi walioko Mikoa ya Katavi na Rukwa ili maeneo yanayokabiliwa na ukame yapate mvua?

Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Christopher Chiza, alipinga mpango huo na kusema hakuna kitu kama hicho isipokuwa wapo watu wenye utaalamu wa kuangalia mawingu yanayoendana na mvua.

Alisema watu wote wanaosema kuwa wanaweza kutengeneza mvua kwa imani za kishirikina ni waongo na hivyo hawapaswi kuaminiwa.

Alisema siyo wakati mwafaka kwa Serikali kushinikizwa kurasimisha utaalamu huo wa kuleta mvua kwa kuwa hakuna tafiti zozote zilizofanyika na kuthibitisha kuwapo kwake.

Wabunge Z’bar wakwamisha Muswada wa kura za Maoni - mwananchi

Dodoma. Muswada wa Sheria ya Kura ya Maoni wa mwaka 2013 uliokuwa ujadiliwe katika mkutano wa 12 wa Bunge unaoendelea mjini Dodoma, umeondolewa na sasa utajadiliwa Bunge lijalo.

Habari za uhakika zilizopatikana jana, zilisema kwamba kuahirishwa huko kumetokana na wajumbe wa Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala ya Bunge wanaotoka Zanzibar kupinga vikali kura ya maoni kupigwa visiwani humo kwa kuwa tayari huko kuna sheria hiyo.

Muswada huo ulikuwa ujadiliwe na wabunge katika kikao cha Bunge kinachoendelea ukitanguliwa na Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya mabadiliko ya Katiba wa mwaka 2013.

“Ukisoma huu Muswada unasema kura hiyo itapigwa Tanzania Bara na Zanzibar sasa sheria hii ina apply vipi (inatumikaje) Zanzibar wakati kule tuna sheria yetu tayari?” alihoji Mbunge mmoja wa Zanzibar.

Kaimu Katibu wa Bunge, John Joel alipoulizwa jana, alithibitisha kuondolewa kwa muswada huo wa kura ya maoni kusema na utakaojadiliwa ni ule wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba pekee.

“Bunge litaahirishwa Ijumaa (keshokutwa) na ni kweli huo Muswada wa Kura ya Maoni umeondolewa kwa sababu bado uko kwenye ngazi ya kamati,” alisema Joel.

Alipoulizwa sababu za kuondolewa kwa muswada ambao ulishaingizwa kwenye ratiba ya Bunge, alitaka swali hilo aulizwe Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi.

Waziri Lukuvi alithibitisha kuondolewa kwa muswada huo na kusema utajadiliwa katika Mkutano wa Bunge wa Oktoba.

“Ni kweli muswada huu hautajadiliwa na Bunge hili bado kuna mashauriano yanaendelea kati ya SMZ (Serikali ya Mapinduzi Zanzibar) na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” alisema.

Kwa upande wake, Mnadhimu Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Tundu Lissu alisema wabunge wa Zanzibar ndiyo waliokwamisha muswada huo kutokana na mgongano wa sheria.

“Wao wanasema masuala ya kura ya maoni siyo ya Muungano kwa sababu wao tayari wana sheria yao ya kura ya maoni. Sasa wanahoji inakuwaje sheria hii itumike tena hadi Zanzibar? Huu ni mgongano,” alisema.

Lissu ambaye pia ni Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), alisema tangu mwanzo aliliona suala hilo na kuitahadharisha Kamati ya Bunge kwamba mapendekezo hayo yana upungufu.

Muswada pekee uliobaki wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba unatarajiwa kuwasilishwa leo huku ukitarajiwa kuibua mjadala mzito kutokana na misimamo ya baadhi ya wabunge.

Muswada huo unawasilishwa wakati CCM kikiwa kimeweka msimamo wa kupinga baadhi ya mambo katika Rasimu ya Katiba.



Yanayotarajiwa kuzua mjadala

Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe amekiri kupokea mapendekezo kutoka kwa wabunge na hasa kwenye Sheria ya Marekebisho ya Mabadiliko ya Katiba akisema wametaka kuangaliwa upya kwa kipengele cha Kamati ya Uteuzi ya viongozi wa Bunge la Katiba. Alisema sasa wataweka sifa za mwombaji wa nafasi hizo na wasiokuwa nazo hawatagombea.

Muswada wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba unataka wawakilishi kutoka makundi ya jamii kuwa 166 katika Bunge la Katiba, lakini wabunge wanataka idadi iwe 200.

Mbunge wa Muhambwe, Felix Mkosamali (NCCR-Mageuzi) alisema uzoefu katika nchi nyingine unaonyesha kuwa mabunge ya Katiba hushirikisha watu wengi ili kupata uwakilishi mpana tofauti na mapendekezo yaliyotolewa.

Mkosamali ambaye pia ni mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala, alisema ni vyema sheria ikasema wajumbe wa Bunge hilo watatoka katika taasisi zipi.

Kifungu kingine ni kile kinachohusu Kamati ya Uteuzi wa Mwenyekiti na Makamu wake ambao kwa mujibu wa muswada itaundwa na Spika wa Bunge la Jamhuri na Spika wa Baraza la Wawakilishi, Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (AG) na yule wa SMZ, Waziri wa Katiba na Sheria Tanzania Bara na Waziri wa Katiba na Sheria wa Zanzibar na Kiongozi Rasmi wa Kambi ya Upinzani Bungeni.

Mkosamali alisema muswada huo wa Mabadiliko ya Katiba unasema mwenyekiti wa muda atakuwa Spika wa Bunge lakini akataka: “Mwenyekiti wa muda atokane na Chama cha Majaji wastaafu maana wao hawafungamani na upande wowote.”

KASHFA YALIKUMBA JESHI LA POLISI TENA-CCTV ZAZIMWA KURUHUSU UJAMBAZI

SIKU chache baada ya tukio la wizi mkubwa wa fedha katika Benki ya Habibu mjini Dar es Salaam, siri nzito zimeanza kuvuja kuwa polisi wanadaiwa kuhusika katika tukio hilo kwa kuhujumu kamera za usalama za CCTV zinazomilikiwa na jeshi hilo.

Katika tukio hilo, watu wanaodaiwa kuwa majambazi walipora dola za Marekani 20,000 ambazo ni sawa na Sh milioni 32 za Tanzania.

Katika tukio hilo, Polisi Mkoa wa Ilala inamshikilia askari mmoja kwa kosa la kuhusika katika tukio hilo kutokana na kushindwa kuchukua hatua za haraka wakati tukio linatokea.

Habari za uhakika kutokana ndani ya jeshi hilo, zinasema siku ya tukio polisi waliokuwa zamu kuongoza mitambo hiyo, kwa namna moja au nyingine wanadaiwa kufanya hujuma hiyo, kwa lengo la kupoteza mawasiliano na maeneo mengi ya polisi.

Chanzo chetu hicho, kiliongeza kuwa siku ya tukio eneo lote la mzunguko wa barabara ya Uhuru na maeneo ya jirani na Kiwanda cha Bia Tanzania (TBL), sehemu zote hazikuwa na huduma ya kamera za usalama, jambo ambalo si la kawaida kutokea.

“Hatua iliyofikia sasa ni mbaya, huwezi amini siku ya tukio kamera za CCTV zinazotumiwa na polisi zilizimwa kabisa, kitendo hiki kilisababisha polisi makao makuu wasijue nini kinachoendelea pale.

“Ndiyo maana utaona kuna askari mmoja anashikiliwa katika tukio lile, haiwezekani kituo kikuu kishindwe kubaini uwapo wa tukio hili, wakati kuna mawasiliano ya kutosha, umefika muda wa kulisafisha jeshi letu kwa kasi,” kilisema chanzo chetu.

Chanzo hicho, kilisema mitambo ya kamera hizo, ilizinduliwa na Rais mstaafu Benjamin Mkapa mwaka 2004 na imekuwa ikifanya kazi bila matatizo yoyote.

“Nimekuwapo hapa tangu mwaka 2004, kamera hizi zilipozinduliwa rasmi na hazijawahi kuharibika hata siku moja, iwe siku ya tukio zisifanye kazi,” kilihoji chanzo chetu.

Askari aliyekamatwa katika tukio hilo, anadaiwa anafanya kazi katika kituo cha Oysterbay Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Marietha Minangi, alithibitisha kukamatwa kwa askari huyo.

Kamishna wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alipoulizwa na MTANZANIA jana, alisema ameipokea taarifa hiyo na wanaifanyia kazi haraka iwezekanavyo.

“Taarifa hii tumeipokea, tunaifanyia kazi haraka sana ili kupata ukweli, naomba tuwe na subira,” alisema kwa kifupi Kamishna Kova.

Alisema bado polisi wanaendelea na uchunguzi wa tukio hilo na kwamba watu waliokamatwa watafikishwa mbele ya vyombo vya dola.

Monday, September 2

KINGUNGE AMSHANGAA KAGAME



MWANASIASA mkongwe nchini, Kingunge Ngombale Mwiru, amejitosa katika mgogoro wa kidiplomasia uliopo kati ya Rais Jakaya Kikwete na Rais wa Rwanda, Paul Kagame.

Akizungumza na MTANZANIA Jumatatu mwishoni mwa wiki nyumbani kwake Kijitonyama jijini Dar es Salaam, Kingunge alimshangaa Rais Kagame kwa jinsi alivyouchukulia vibaya ushauri wa Rais Jakaya Kikwete, aliompa juu ya waasi wa nchini humo.

Alisema kwamba, kilichotolewa na Rais Kikwete juu ya waasi hao, ulikuwa ni ushauri ambao ulilenga kurejesha amani nchini Rwanda na wala si vinginevyo.

“Kutoelewana baina ya nchi jirani si jambo dogo na jema, hivyo si vizuri hali hiyo ikaachwa iendelee kwa muda mrefu bila kupatiwa suluhu.

“Nashauri jitihada zote zifanyike ili sintofahamu hii baina yetu na Rwanda ipate suluhu haraka iwezekanavyo, kwa sababu sisi ni majirani.

“Ushauri alioutoa Rais Kikwete kwa Rwanda ulikuwa sahihi na nauunga mkono, lakini maadam wenzetu Rwanda hawakuupokea vizuri, jawabu ni kufanya juhudi za kidiplomasia ili mtafaruku huo uishe.

“Hata hivyo, pamoja na mambo mengine, mgogoro huo hauna sababu ya kututoa au kuvunjika kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki, kwa sababu nchi zote tano zinahitajiana na tuna wajibu kwa wananchi wetu kushirikiana kwa faida ya nchi zote husika,” alisema Kingunge kwa kifupi.

Akizungumzia vyama vya upinzani nchini, Kingunge alisema safari yao katika kuchukua dola bado ni ndefu kutokana na kutokuwa na mtandao unaofikika nchi nzima.

Alisema vyama vikubwa vya upinzani vikiwamo Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na Chama cha Wananchi (CUF), bado viongozi wake wana tabia ya kuhutubia na kuondoka badala ya kujenga chama chenye mtandao.

“Tatizo la vyama vyetu vya upinzani nchini, lilianza tangu mwaka 1992 vilipoanzishwa na tangu wakati huo, havijaweza kujirekebisha, viongozi wake wanafikiria kwenda Ikulu tu na hivyo wanajielekeza kwenye kushinda urais na kusahau nafasi nyingine.

“Lakini, ili kufika Ikulu, lazima uwe na watu wa kukufikisha huko na watu hao ni wanachama kutoka kwenye vijiji, kata, wilaya na taifani. Kama kule kwenye watu hao hawajaweza kujizatiti, suala la kwenda Ikulu litawachukua muda mrefu.

“Ili kuwa na nafasi ya kushinda uchaguzi, chama lazima kiwe kimejikita kwa umma wa wananchi na siyo kuzungukazunguka,” alisema Kingunge.

Alisema mikutano ya hadhara kwa vyama ni sahihi kufanyika na kwamba ndiyo kazi ya vyama vya siasa, kwani chama kinapata nafasi ya kueneza sera na kujipima kisiasa kupitia mikutano hiyo.

Pamoja na hayo, alisema mvuto huo wa kisiasa huwa si wa wakati wote kwani inawezekana chama kina tabia ya kuzungumza juu ya masuala ambayo wananchi wanapenda kuyasikia hata kama hawakubaliani nacho.

“Kupata watu wengi kwenye mkutano haimaanishi kwamba vyama vingine havipendwi au havikubaliki, inawezekana vyama vingine vikawa vinapendwa na kukubalika, lakini havina tabia ya kufanya mikutano.

“Lakini, kwa ujumla wake, ni kwamba vyama vyote hivyo vinaweza kushinda urais kama tu vinashinda kwenye majimbo ya ubunge, ila kwa hali jinsi ilivyo hivi sasa, safari yao bado ni ndefu hawawezi kuchukua nchi,” alisema mwanasiasa huyo.

Sakata la Mansour
Akizungumzia kuvuliwa uanachama kwa aliyekuwa Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi Kisiwani Zanzibar, Mansoor Yussuf Himid, Kingunge alisema mwanasiasa huyo alistahili kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa Katiba ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), alistahili adhabu hiyo.

“Chama kina sera ambazo tunazitekeleza na tunaziheshimu, tuna katiba inayotuongoza na kwa mujibu wa katiba yetu, tuna vikao vinavyofuatilia uadilifu wa wanachama wetu.

“Uadilifu huo ni pamoja na kuheshimu Katiba na sera za msingi wa chama na vikao vya mara kwa mara, kwa hiyo, mwanachama anayeonekana kwa kauli na vitendo vyake yuko kinyume na matakwa ya Katiba, Halmashauri Kuu ina madaraka ya kumvua uanachama, uongozi au kumpa adhabu nyingine.

“Kwa hiyo, Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ilikuwa sahihi, hivi ni nani asiyemfahamu Mansour kwamba ni CUF? Hili suala liko wazi familia yao nzima ni wanachama wa CUF, kwa hiyo si ajabu kwake.

“Mimi nastaajabu kwa sababu, kwanza baba yake alikuwa miongoni mwa watu 14 waliotekeleza Mapinduzi ya Zanzibar na hakuwa mkorofi, sijui imekuwaje Mansour naye akabadilika maana ninavyomfahamu hakuwa hivi,” alisema Kingunge.

Agosti 26, mwaka huu, kikao cha NEC, kilimvua uanachama Mansour kwa kushindwa kusimamia malengo ya CCM na kutekeleza masharti ya uanachama.

Msigwa amkalia kooni Waziri Kagasheki



Dodoma. Msemaji wa kambi ya upinzani wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Mchungaji Peter Msigwa amesema kuna ugawaji holela wa maeneo katika Mamlaka ya Uendelezaji Bonde la Ngorongoro (NCAA) kwa kampuni za kitalii na kudai kwamba Waziri wake, Balozi Khamis Kagasheki anahusika.

Msigwa aliwaambia waandishi wa habari katika ofisi za kambi hiyo mjini Dodoma jana kuwa Balozi Kagasheki amerudia makosa yaliyofanywa na mtangulizi wake, Ezekiel Maige.

Hata hivyo, Waziri Kagasheki amejibu tuhuma hizo akisema hana mamlaka kisheria ya kugawa vitalu kama inavyodaiwa na kwamba kilichotolewa ni vibali kwa ajili ya kambi za watalii (tented camps).

“Katika Kamati ya Vitalu tulisema kulikuwa na ukiukwaji mkubwa wa ugawaji na Maige alipata wakati mgumu lakini huyu aliyemrithi hajabadili kitu,” alisema Msigwa, ambaye pia ni Mbunge wa Iringa Mjini (Chadema). Mchungaji Msigwa alisema kampuni mbili za Leopard Tours na Masai Sanctuaries zilipewa vitalu vya utalii ndani ya eneo la NCAA kinyume na mpango wa miaka mitano wa ugawaji wa mamlaka.

Kwa kawaida wataalamu wa uhifadhi na uongozi NCAA hukutana kila baada ya miaka mitano ili kugawa vitalu katika eneo la Ngorongoro. Msigwa alisema Waziri Kagasheki alitakiwa kupata ushauri kutoka uongozi wa Ngorongoro kabla ya kufikia uamuzi wa kutoa vitalu hivyo.

“Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inazo nyaraka zinazoonyesha kuwa kampuni hizo zilipewa vitalu vya utalii vya Ndutu na Oloololo ambavyo havikuwa katika mpango wa ugawaji kama inavyotakiwa kisheria.”

Alidai kuwa katika moja ya barua ambazo kambi hiyo inazo, Waziri Kagasheki aliiandikia Kampuni ya Leopard Tours akiitaarifu kuwa tayari ameiagiza NCAA ipewe kitalu chenye ukubwa wa hekari tano.

“Alielekeza mamlaka kuipa kampuni hiyo ekari tano kwa Dola za Marekani 30,000 (Sh48 milioni) ambacho ni nusu ya kiwango cha kawaida cha Dola 60,000 (Sh95 milioni) kwa ekari 10,” alisema Msigwa.

Barua hiyo ya Julai 17, 2013 yenye kumbukumbu namba CAB.315/319/01B iliyosainiwa na Balozi Kagasheki inauelekeza uongozi wa NCAA kumpa viwango hivyo.

Waziri Kagasheki alisema alitoa punguzo hilo kwa kampuni hiyo ya Leopard si kwa ajili ya kitalu, bali tozo kwa ajili ya kambi yake ya watalii na kueleza kushangazwa na tuhuma zilizoelekezwa kwake akisema sheria haimruhusu kugawa vitalu hadi awasiliane na kamati husika. Alisema aliwapunguzia ada hiyo Leopard kwa kuwa walipewa mita za mraba 29.7 na kudaiwa Dola 60,000. Alisema wangetakiwa kulipa kiasi hicho cha fedha kama wangepewa mita za mraba 60.

“Niliona hawa jamaa hawajatendewa haki kwani walitozwa ada kubwa kwa ajili ya nusu eneo,” alisema na kumtaka Msigwa kutoa ushahidi wa barua kama amegawa vitalu. Balozi Kagasheki alisema ugawaji wa vitalu utafanyika keshokutwa atakapokutana na kamati husika.

Haya hivyo, Mchungaji Msigwa alisema waziri alifanya uamuzi huo bila kuzingatia sheria na kanuni za ugawaji wa vitalu, pia akivunja sheria kwa kufanya uamuzi moja kwa moja na kampuni hiyo na kushusha viwango vilivyowekwa kisheria bila kutoa tangazo la Serikali.

Mke wa Kagasheki atuhumiwa

Mbali na tuhuma hizo, Mchungaji Msigwa pia amemtuhumu Mbunge wa Viti Maalumu (CCM), Catherine Magige akidai kwamba ametumia ushawishi wa mumewe, Balozi Kagasheki kupewa msaada wa Sh10 milioni na NCCA kupitia taasisi yake ya Catherine Foundation Development Ltd kinyume cha kanuni inayotaka isizidi Sh2 milioni.

“Mradi huu ulipewa fedha hizo huku dokezo la maombi ya msaada huo ukionyesha kuwa watendaji wa NCAA walitoa mapendekezo mara mbili kuwa hakuna bajeti ya kusaidia msaada huo,” alisema.

Msigwa alisema Kaimu Mhifadhi wa NCAA alinukuliwa akisema fungu la msaada halina fedha ya kutosha na kwamba Magige ashauriwe kusubiri mpaka mwaka wa fedha ujao 2013/2014... “Dokezo hili lilisainiwa tarehe 14.12.2012 lakini jambo la kushangaza na la kutia walakini... Mhasibu aliagizwa ilipwe kiasi hicho.”

Alisema pamoja na baadhi ya watendaji kueleza kwamba NCAA haikuwa na fedha, Kaimu Mhifadhi Mkuu alitoa agizo Juni 18,2013 la kutoa kiasi cha Sh10 milioni kwa taasisi hiyo.“Katika hili kuna mgongano mkubwa wa masilahi kwa sababu huwezi kumtenganisha Mheshimiwa Kagasheki na kazi zake za uwaziri na hii ya Catherine Foundation ambaye ni mke wake,” alisema.

Akizungumzia suala hilo, Balozi Kagasheki alikanusha vikali tuhuma hizo na kusema hakuwa na mamlaka ya kuishinikiza NCAA... “Nisingependa kuzungumzia masuala ya mke wangu maana kuna mambo mazito ya nchi ya kuzungumzia. Ila siwezi kushinikiza taasisi iliyo chini yangu itoe Sh10 milioni pengine labda ingekuwa Sh1 milioni.”

Kagasheki alisema hamshangai Mchungaji Msigwa kwani amekuwa na tabia ya kumzushia mambo na kukumbusha alivyoshinikiza ajiuzulu katika kikao kilichopita cha bajeti.

Naye Magige alipoulizwa kuhusu fedha hizo, alikiri taasisi yake kupewa lakini akasema walifuata taratibu zote katika kuomba kama wanavyofanya katika taasisi nyingine.

“Sisi tunaomba misaada katika taasisi mbalimbali na katika hili tulifuata taratibu zote na wakaamua watupe Sh10 milioni. Tungekataa wakati wanafunzi hawana madawati?” alihoji Magige.

Alisema kutolewa kwa fedha hizo kulikuwa hakuna shinikizo lolote kutoka kwa Waziri Kagasheki na kwamba kama ingekuwa hivyo, taasisi hiyo ingepewa fedha nyingi zaidi.

Alieleza kushangazwa na kauli za Msigwa dhidi yake na taasisi yake ambayo alisema imekuwa msaada mkubwa kwa shule za msingi Arusha ambazo zimekuwa na upungufu wa madawati.

Nelson Mandela arudishwa nyumbani


Taarifa zaidi zilieleza kwamba Mandela ambaye ni mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, alisafirishwa kutoka Hospitali ya MediClinic, Pretoria na kupelekwa nyumbani kwake Johannesburg.

Saturday, August 31

Serikali yasalimu amri kwa wabunge


Mbunge wa Nkasi Kaskazini, Ali Mohamed Keissy
akichangia bungeni mjadala wa kupitisha muswada wa
sheria ya taifa ya umwagiliaji wa mwaka 2013,
ambapo alikuwa akipinga wawekezaji wa kilimo kwenda kuwekeza mkoani Rukwa, 

Dodoma. Muswada wa Sheria ya Taifa ya Umwagiliaji wa mwaka 2013, jana ulipita kwa mbinde bungeni mjini Dodoma, huku Serikali ikisalimu amri kwa wabunge na kukubali kurekebisha baadhi ya vifungu vyake.

Bila kujali tofauti zao za kisiasa, wabunge jana walisimama kidete na kuonyesha uzalendo wa hali ya juu, wakitaka sheria hiyo imlinde mzawa badala ya mwekezaji.

Moto huo wa wabunge uliwalazimisha Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Christopher Chizza na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Fredrick Werema kusalimu amri na kukubali mapendekezo ya wabunge.

Msimamo wa wabunge hao katika kuibana Serikali, pia ulililazimisha Bunge kutengua kanuni zake na kuendelea na shughuli za kupitia muswada huo hadi saa 7:35 mchana, badala ya kusitishwa saa 7:00 kwa ratiba ya kawaida.

Serikali ilikubali mapendekezo ya wabunge hao na kurekebisha vifungu ambavyo sasa vinampa mmiliki wa ardhi itakayotangazwa eneo la umwagiliaji kuwa mwanahisa na kulipwa fidia.

Awali, wabunge waliowasha moto huo ni pamoja na Mbunge wa Kisesa, Luhaga Mpina na Suleiman Jaffo wa Kisarawe, wote kutoka Chama Cha Mapinduzi(CCM), ambapo walisema baadhi ya vifungu vya muswada huo wa sheria vilikuwa na ajenda ya siri.

Wakichangia mjadala huo wabunge hao walitaka vifungu vinavyotamka kuwa eneo litakalotangazwa kuwa la umwagiliaji litatwaliwa na Tume itakayoundwa na kupewa fidia viboreshwe, ama kama haifai, vifutwe.

Mpina alishikilia msimamo kuwa badala ya kumlipa fidia mwananchi, vifungu hivyo vitamke kuwa atalipwa fidia ama kuwa mwanahisa wa mradi ama alipwe fidia na papo hapo kuwa mwanahisa.

Mbunge wa Kawe, Halima Mdee (Chadema), aliitaka Serikali itunge sheria zinazolinda wazawa na kwamba hatua ya kuacha mianya, ndiyo mwanzo wa wawekezaji kuwanyang’anya ardhi wazalendo.

Mbunge wa Simanjiro, Christopher Ole Sendeka (CCM), alisema kuwa haihitaji kuipitia sheria yote ili kubaini maudhui yenye dhamira ovu dhidi ya Watanzania ndani yake akisisitiza kuwa baadhi ya vifungu vina ajenda ya siri.

“Vifungu hivi vina ajenda ya siri ya kuwapeleka Watanzania kwenye utumwa…Kama msipobadilisha vifungu hivi, mwondoe huu muswada maana hii ni dhambi ya mauti,” alisisitiza Ole Sendeka.

Ole Sendeka alisisitiza sheria itamke kuwa kama ni kutwaa ardhi yoyote, hata kama ni Rais anataka kufanya hivyo ni lazima hilo lifanyike kwa ushirikiano na mmiliki wake, ama na wanakijiji wote kupitia mkutano mkuu.

Mbunge wa Viti Maalumu, Esther Bulaya (CCM), alisema Watanzania wameshindwa kunufaika na rasilimali nyingine na waliyobakia nayo ni ardhi hivyo hawako tayari kurudisha ukoloni mamboleo.

Mbunge wa Peramiho, Jenister Mhagama (CCM), alisema ni lazima sheria hiyo iweke sharti la lazima kwa mwekezaji kuingia ubia na mmiliki wa ardhi na kama hataafiki, ndipo apewe fidia.

IGP aibiwa upanga wa dhahabu - mwananchi newspaper




Jeshi la Polisi limeingia katika kashfa nzito baada ya mkuu wake, Inspekta Jenerali Said Mwema, kuibiwa upanga wa dhahabu ambao ni mali ya Shirikisho la Wakuu wa Majeshi ya Polisi wa nchi za Kusini mwa Afrika (SARPCCO).

Upanga huo wenye uzito wa takriban kilo tatu na wenye thamani ya zaidi ya fedha za Tanzania Sh600 milioni, ni kielelezo kwa nchi inayokabidhiwa uongozi wa SARPCCO.

Mwaka jana Tanzania ilikuwa mwenyekiti wa SARPCCO, ambapo upanga huo ulikabidhiwa kwa IGP Mwema na Jenerali Magwashi Victoria ‘Riah’ Phiyega, ambaye ni Kamishna wa Taifa wa Polisi wa Afrika Kusini aliyekuwa amemaliza muda wake kwa wakati huo.

Hilo ni tukio la pili la wizi la mali zinazohusu ofisi ya IGP, ambapo mwaka jana ndani ya ofisi hiyo kuliibwa kompyuta ndogo (laptop), ikiwa na taarifa muhimu za kipolisi. Hadi sasa hakuna taarifa za kupatikana kwa kompyuta hiyo.

IGP Mwema alikabidhiwa upanga huo Septemba 5, 2012, katika mkutano saba wa SARPCCO uliofanyika Zanzibar na kuhudhuriwa na wakuu wa majeshi ya Polisi kutoka nchi 13, pamoja na mashirika ya kimataifa.

Upanga huo ambao unakwenda sambamba na bendera ya SARPCCO, ni moja ya vielelezo vya nchi iliyochaguliwa kuwa Mwenyekiti wa shirikisho hilo, ambaye moja kwa moja anakuwa ni Mkuu wa Jeshi la Polisi katika nchi husika.

Kwa mujibu wa taratibu za SARPCCO, vielelezo hivyo hutakiwa kuwekwa ofisini kwa kiongozi husika, ikiwa ni alama ya kila mgeni atakayeingia ofisini hapo kutambua uwepo wa wadhifa huo wa kimataifa.

Uchunguzi wa gazeti hili ulibaini kuwa IGP aligundua kutoweka kwa upanga huo wiki iliyopita, wakati akijiandaa kwenda kuukabidhi kwa mwenyekiti mpya wa SARPCCO, ambaye ni IGP wa Namibia.

Taarifa za ndani ya jeshi hilo zilibaini kuwa, IGP alilazimika kuondoka bila upanga huo alipokwenda Namibia wiki iliyopita kuhudhuria mkutano wa nane wa SARPCCO, uliofanyika Jumapili iliyopita mjini Windhoek.

Kwa mujibu wa uchunguzi, IGP Mwema alikabidhi upanga unaofanana na huo ambao siyo wa dhahabu, alioazimwa kutoka kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi la Namibia, Inspekta Jenerali, Luteni Jenerali Sebastian Ndeitunga, na kukabidhiwa kama ishara ya kukabidhiwa uenyekiti wa SARPCCO kwa kipindi cha mwaka mmoja.

Uchunguzi ulibaini kuwa IGP Mwema alitoa ahadi ya kurejesha upanga halisi ndani ya kipindi cha mwezi mmoja, au Serikali ya Tanzania italazimika kutengeneza mwingine kulipa uliopotea.

Uchunguzi wa gazeti hili unaonyesha kuwa kashfa hiyo ametupiwa Mkuu wa Polisi Zanzibar, Kamishna Mussa Ali Mussa pamoja na dereva wake, ikidaiwa kuwa upanga huo baada ya kupokewa na IGP Mwema, Septemba mwaka jana uliwekwa kwenye gari la kamishna huyo.

Kamishna Mussa ndiye alikuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Mkutano wa Saba, na pia ofisa mwenyeji kwa wajumbe wa mkutano huo uliofanyika Zanzibar.

Hata hivyo, taarifa zingine zilidai kuwa IGP Mwema naye analaumiwa kwa kutofuatilia kwa karibu zana za kazi, kwani baada ya kuupokea alitakiwa kuhakikisha unakuwepo ofisini kwake kama alama ya uenyekiti wake.

Gazeti hili lilipowasiliana kwa njia ya simu na Mkuu wa Polisi Zanzibar, Kamishna Mussa Ali Mussa kuhusu madai hayo alisema, kitara (upanga) hicho ni kweli kimepotea, lakini yeye hahusiki kwa kuwa kila kitu kina utaratibu wake.

“Ni kweli kitara kilikabidhiwa kwa afande IGP na mimi nilishuhudia kikikabidhiwa, na ni kweli kitara hakijulikani kiliko, lakini mimi sihusiki na kupotea kwake. Ni kweli mimi nilikuwa ofisa mwenyeji wa mkutano huo, lakini siku hiyo zilitolewa zawadi nyingi, watu walipewa mikoba, kwa hiyo mtu akipoteza mkoba wake niulizwe mimi?” alihoji Kamishna Mussa.

Alisema kila kitu kina utaratibu wake na kwamba taarifa kwamba yeye amehojiwa kutokana na upotevu wa kitara hicho au kuna kamati imeundwa, hazina ukweli.

“Sijawahi kuona kamati hiyo. Kamati hiyo kwanza imeundwa na nani na inatoka wapi? Hayo maneno yanatengenezwa na watu wa nje,” alisema Kamishna Mussa.

Alisema kinachofanyika hivi sasa ni kukitafuta ili kiweze kurejeshwa kunakohusika.

Taarifa zingine zilidai hata bendera ya mezani ya mwenyekiti wa SARPCCO, aliyokabidhiwa sambamba na upanga huo nayo kuna hatihati ilipotea.

Msemaji wa Jeshi la Polisi nchini, Advera Senso alipotakiwa kuzungumzia suala hilo alisema aulizwe kamishina wa polisi Zanzibar.

“Suala hilo muulize Kamishina wa Zanzibar ndiye anayejua,” alisema Senso.

Uchunguzi unaonyesha kuwa maofisa katika ofisi ya IGP na ile ya Kamishna wa Polisi Zanzibar, wamehojiwa akiwamo Kamishna Mussa, na kwamba upelelezi mkubwa umekuwa ukiendelea ndani ya jeshi hilo.

Hata hivyo, juhudi za gazeti hili za kutaka kufahamu uamuzi wa SARPCCO katika ofisi yake ya uratibu iliyopo kwenye ofisi za Makao Makuu ya Kanda ya Polisi wa Kimataifa (INTERPOL), Harare, Zimbabwe, hazikuzaa matunda baada ya baruapepe iliyotumwa kwa ofisa mratibu wa SARPCCO ambaye pia ni mkuu wa ofisi ya Kanda ya INTERPOL, C. Simfukwe kutopata majibu.

SARPCCO ilianzishwa mwaka 1995, Victoria Falls, Zimbabwe, lakini kisheria ilitambulika rasmi mwaka 2006 na lengo lake kuu ni kupambana na uhalifu wa kuvuka mipaka.

Uenyekiti wake ni mwaka mmoja, ambapo kwa sasa mwenyekiti ni Mkuu wa Jeshi la Polisi la Namibia Inspekta Jenerali, Luteni Jenerali Sebastian Ndeitunga, aliyepokea wadhifa huo kutoka kwa IGP Mwema.

Friday, August 30

IGP asafisha vigogo Uwanja wa Ndege


Siku chache baada ya kuibuliwa kwa kashfa ya kupitishwa kiholela kwa dawa za kulevya katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Jeshi la Polisi limemwondoa Kamanda wa Polisi wa Viwanja vya Ndege Kamishna Msaidizi (ACP), Deusdedit Kato pamoja na Mkuu wake wa Upelelezi, David Mwafwimbo.

Mbali ya maofisa hao, pia jeshi hilo limemwondoa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mtwara, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Linus Sinzumwa, naye ikiwa ni miezi michache baada ya kutokea kwa ghasia wakati baadhi ya wakazi wa huko walipokuwa wakipinga mpango wa Serikali wa ujenzi wa bomba la gesi kwenda Dar es Salaam.

Nafasi ya Kamanda Sinzumwa imechukuliwa na Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP), Zelothe Stephen kutoka Makao Makuu ya Polisi.

Taarifa iliyotolewa jana na Msemaji wa Jeshi la Polisi, Advera Senso ilisema Mkuu wa jeshi hilo, Inspekta Jenerali (IGP), Said Mwema amemteua, ACP Selemani Hamisi kuchukua nafasi ya Kato ambaye anahamishiwa makao makuu ya jeshi hilo. Kabla ya uteuzi huo, Kamanda Hamisi alikuwa Makao Makuu Idara ya Upelelezi.

IGP Mwema pia amemteua Mrakibu Mwandamizi wa Polisi (SSP) Hamad Hamad kuchukua nafasi ya Mwafwimbo aliyehamishiwa mkoani Lindi kuwa Mkuu wa Polisi wa Wilaya ya Lindi (OCD).

Taarifa hiyo ya Polisi ilisema uhamisho huo ni wa kawaida kwa mujibu wa kanuni, taratibu na miongozo yake. Hata hivyo, katika siku za karibuni, kumekuwa na malalamiko mengi kuwa vyombo vya usalama katika uwanja huo vimeshindwa kudhibiti biashara hiyo na matokeo yake Tanzania imechafuka katika medani ya kimataifa kutokana na idadi kubwa ya vijana wake kukamatwa sehemu mbalimbali duniani.

Matukio ya karibuni yanahusisha kukamatwa kwa wasanii Agnes Masongange na Melisa Edward waliokamatwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Oliver Tambo, Johannesburg, Afrika Kusini.

Kutokana na kashfa hiyo, Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe aliamua kulivalia njuga suala hilo na kuchukua hatua kadhaa na pia alifichua jinsi wasichana hao walivyosaidiwa kupitisha dawa hizo na mtandao uliohusisha polisi, maofisa usalama wa taifa na baadhi ya wafanyakazi wa JNIA.

RPC Mtwara

Sinzumwa anaondoka Mtwara baada ya ghasia kubwa zilizozuka Mei mwaka huu wakati baadhi ya wakazi wa Mtwara walipokuwa wakipinga gesi kutoka Msimbati kusafirishwa kwa bomba hadi Dar es Salaam.

Katika ghasia hizo, ambazo Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), liliingilia kati, polisi walishutumiwa na wakazi wa huko kwa kutumia nguvu kubwa na kuwasababishia madhara.

RAIS KIKWETE AMUOMBA RAIS WA UGANDA AONGEE NA KAGAME ILI KUMALIZA UGOMVI ULIPO

RAIS Jakaya Kikwete, amewasiliana na Rais wa Uganda, Yoweri Museveni, ili azungumze na Rais wa Rwanda, Paul Kagame kwa nia ya kumaliza mvutano wa maneno kati yao kwa busara.

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, alisema hayo jana bungeni, alipokuwa akijibu swali la Kiongozi wa Upinzani bungeni, Mbunge wa Hai, Freeman Mbowe (Chadema).

“Tunataka suala hili limalizike kwa njia ya busara, ili watu waendelee kuchapa kazi, ninaamini busara zitatumika kumaliza tatizo hilo,” alisema.

Akiuliza swali katika kipindi cha maswali ya Papo kwa Hapo kwa Waziri Mkuu jana, Mbowe alitaka kujua kauli ya Serikali na mikakati iliyopo kupata suluhu katika mvutano wa maneno uliojitokeza kati ya Rais Kikwete na Rais Kagame.

Pia Mbowe alitaka Serikali kuunda jopo la ushawishi wa kimataifa, kutokana na Rwanda kuonekana kushawishi nchi za Uganda na Kenya, jambo ambalo linaashiria kuitenga Tanzania katika shughuli mbalimbali za Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Kwa mujibu wa Mbowe, kitendo cha marais wa Kenya, Uganda na Rwanda kukutana katika mikakati ya kuanza kutumia bandari ya Mombasa ambayo ingekuwa ya nchi za Afrika Mashariki, ni dalili kuwa Tanzania imeanza kutengwa.

Mbowe alisema pamoja na kuanza kutengwa kwa Tanzania katika shughuli za Afrika Mashariki pia kumekuwa na mgogoro uliozuka hivi karibuni wa Bunge la Afrika Mashariki, kutaka vikao vya Bunge hilo vifanyike kwa kupokezana katika nchi wanachama, tofauti na ilivyokuwa awali, ambapo vikao hivyo vilifanyika Arusha.

Hata hivyo, Pinda katika jibu lake, alisisitiza kuwa hakuna sababu ya Serikali kuunda jopo la kutafuta ushawishi wa suluhu na Rwanda kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), kwa kuwa hakuna sababu za kufanya hivyo.

Hakuna uhasama Akifafanua, Pinda alisema Serikali haina sababu ya kujenga uhasama na Rwanda, kwa kuwa nafasi ya Tanzania na mchango wake katika nchi za Ukanda wa Maziwa Makuu na Afrika unajulikana.

Alisisitiza, kuwa ushauri aliotoa Rais Kikwete wa kutaka Rwanda kukaa meza moja na waasi, ulikuwa wa busara na haukuwa na tatizo lolote.

Kutokana na msingi huo, alifafanua kwamba ndiyo maana Tanzania haiangalii mvutano huo wa maneno kama tatizo, ingawa Serikali haitapuuza suala hilo linaloonesha kuwepo kwa dalili ya kutoelewana.

“Ukilitazama suala hili huwezi kuamini kama kweli kauli ya Rais Kikwete ingeleta haya, nadhani wenzetu wanalitazama kwa namna tofauti na sisi tunavyolitazama,” alisema.

Pinda alirejea kiini cha mtafaruku huo, kuwa ni ushauri wa Rais Kikwete kwa nchi ya Rwanda kukaa meza moja na waasi, ili kuacha mapigano kwa maslahi ya wananchi wa Rwanda.

Alisema kauli hiyo iliyotolewa na Rais Kikwete katika mkutano wa Umoja wa Afrika (AU) uliofanyika Ethiopia, ilikuwa na nia njema kwa maslahi ya Rwanda, lakini imechukuliwa tofauti nje ya mkutano huo.


Propaganda za biashara
Katika hatua nyingine, Naibu Waziri wa Uchukuzi, Dk Charles Tizeba, alisema kauli zinazotolewa kuwa mizigo ya Rwanda haitapitishwa kwenye bandari ya Dar es Salaam, ni propaganda za kibiashara kutoka nchi washindani.

Hata hivyo, Dk Tizeba hakuwa tayari kubainisha ni nchi ipi inahusika zaidi kutoa propaganda hizo ingawa aligusia kwamba ni nchi zenye bandari.

Alisema baada ya kukutana na wafanyabiashara wa Rwanda na viongozi wa Serikali ya nchi hiyo, wamebaini kuwa hakuna upande uliozuia mizigo kupita Tanzania.

“Huku wanasema kuna maelekezo kwamba wafanyabiashara wa Rwanda wasipitishe mizigo Tanzania, lakini kwa Rwanda wao wanasema Tanzania imezuia mizigo ya Rwanda kupita Tanzania … tumebaini kuwa kauli hizi hazikuwa na ukweli,” alisema.

Alisema wafanyabiashara wa Rwanda wamesema kama Tanzania wanataka Rwanda ipitishe mizigo mingi, ifanye marekebisho kadhaa, ikiwemo kukabiliana na matatizo kama lililowahi kutokea la kupotea kwa kontena mbili za dhahabu na mbolea, kuangalia tozo za kusafirisha magari yasiyosajiliwa Tanzania na kupunguza wingi wa mizani ambao wanadai unachelewesha usafirishaji.

Pia Tizeba alisema walilalamikia udokozi wa vitu vidogo kwenye magari bandarini, jambo ambalo limefanyiwa kazi na hali hiyo haipo tena, kwani baadhi ya magari vifaa vyao vilikuwa vikiibwa maeneo mengine kabla ya kufika Dar es Salaam.

“Kuna mambo mengi yanafanyiwa kazi ikiwamo kuwa na treni mbili za mizigo hadi Isaka, ambazo zitasafirisha mizigo ya Rwanda, Kongo na Burundi, na pia kuweka ofisa wa bandari Kigali, ambaye atakuwa akishughulikia matatizo na kuanzisha mizani ambayo itapima gari likiwa linatembea na kuwa na mizani maeneo matatu,” alisema.

Kuhusu hatua ya Rais Kagame kuzindua mpango wa nchi yake kutumia bandari ya Mombasa, Tizeba alisema nchi inaweza kuwa na njia nyingi za kupitishia mizigo, na kubainisha kuwa bado Tanzania ndilo eneo pekee zuri kwa kusafirisha mizigo kwa nchi zisizo na bandari.

Thursday, August 29

Dk Ndalichako: Siasa zisipewe nafasi kwenye mitihani yetu


Swali: Unazungumziaje alama za upimaji wa mwanafunzi (continuous assessment) zinazotoka shuleni na nafasi yake katika matokeo ya mwisho?

Jibu: Ni vigumu kujua uhalisia wa alama zinazoletwa kutoka shuleni, wengine wanasema Necta tufuatilie huko shuleni ili kujua uhalisia wake, tutafanya vipi hilo wakati wafanyakazi wote wa Necta ukijumlisha na walinzi tupo 297 na shule za sekondari pekee zipo 430?

Mwaka 2011 wale wanafunzi walioandika vitu visivyoeleweka kwenye mitihani ya mwisho, kwenye alama zao za maendeleo zilizoletwa walikuwa mpaka na 75. Wengine walishindwa kuandika chochote kwenye mtihani wa mwisho lakini kwenye alama zao za maendeleo walikuwa na alama nzuri tu.

Ukiwauliza walimu wengine wanasema hawakuwa na walimu, wanasema walikuwa wanatumia waliomaliza kidato cha sita na hawajui kujaza vizuri hizo alama.

Wengine walisema mitihani ya ndani watoto wanatazamiana majibu na sababu nyingi kama hizo.

Kwa sasa kuna kamati imepewa jukumu la kuangalia hizo alama za maendeleo, kwa hiyo hilo ni eneo ambalo lazima tuliangalie.

Pia nafikiri kwa sababu ya mazingira ya shule zetu, tufike mahali tuwe na uwazi zaidi.

Nafikiri tufike mahali kwenye cheti tuweke alama za mtihani wa Necta na zile zilizotoka shuleni.

Tuseme mathalan huyo mtoto amepata A, lakini kwenye mtihani wa Necta alipata alama hii na ile ya shuleni alipata hivi. Baada ya hapo tukifika kwenye soko la ajira mwajiri achague kama ataangalia alama za shule au za Necta.

Swali: Tangu uanze kuiongoza Necta mpaka sasa unajivunia nini?

Jibu: Nimekaa Necta tangu mwaka 2005, yapo mengi naweza kujivunia, kwanza wakati naingia kila kitu kilikuwa manual (hatukutumia mashine), lakini hivi sasa kila kitu kuhusu mtihani kuanzia usajili tunatumia kompyuta.

Hili limesaidia kupunguza makosa, hasa kwa upande wa watahiniwa wa kujitegemea kwa sababu zamani watu walikuwa wanafanya udanganyifu sana.

Sasa hivi haiwezekani kutumia namba ya mtu mwingine. Usahihishaji kwa darasa la saba sasa hivi pia tunatumia mfumo wa OMR, zamani tulikuwa tunatumia watu 480 kusahihisha mitihani kwa siku 30.

Baada ya kufanya tathimini ya mfumo huu kwa mwaka jana, tumebaini kuwa mashine haikufanya kosa hata moja, baadhi yaliyotokea yalisababishwa na watu na mashine iliwaumbua.

Kwa kidato cha nne na kuendelea, hatujaanza kutumia kompyuta lakini kuna mengi tumefanya, sasa hivi tumeweka mfumo kuweka alama, zikishaingizwa kwenye mfumo kutoka kwenye kituo cha usahihishaji hakuna mtu anayeweza kuzigusa na akigusa anaonekana.

Hata msahihishaji akishaziweka mara moja hawezi kuzigusa tena na akigusa anaonekana. Kwa hiyo kwa mfumo huu, huwezi kumwongezea mwanafunzi alama. Kwa hiyo alama za wanafunzi zinakuwa katika mazingira salama sana.

Databank (benki ya mitihani) tumeiimarisha, maswali ni mengi tofauti na zamani ulikuwa unakuta kwa somo husika kuna mitihani miwili tu.

Kwa sasa maswali ni mengi, ndiyo maana hata kuvuja kwa mitihani hakuna. Kwa mfano, somo kama hisabati kuna maswali kama milioni moja, hata ukimpa mwanafunzi hawezi kuyafanya yote na ajue kwenye mtihani ni lipi litatoka.

Sasa hivi kweli mitihani ni salama sana, lengo letu ni kupunguza mikono kwenye mitihani. Naamini zaidi mifumo kuliko mtu na kwenye mitihani tukileta kuaminiana tunaweza kuwa pabaya.

Swali: Nini ambacho bado unatamani kukifanya ndani ya Necta?

Jibu: Ninachotamani kwa sasa ni kufika mahali tuwe na mashine zinazochapisha mitihani, kuhesabu na kuweka zenyewe kwenye bahasha.

Kwa sasa tunatumia kama siku 40 kuweka mitihani ya shule za msingi kwenye bahasha tu, hii ni kwa sababu lazima watu wanaofanya hii kazi wawe ni wachache na wenye weledi mkubwa. Hawa watu wangetumia hizi siku kufikiri namna ya kuwa na mitihani bora zaidi ingesaidia.

Suala jingine ni kuwajengea uwezo wa wafanyakazi wetu, haswa wa kuandaa maswali. Nina bahati nimesoma nje ya nchi nikasoma kwa undani juu ya mitihani.

Nataka tuwe tunawepeleka watu nje kusomea zaidi juu ya kazi zao, utunzi wa mitihani na masuala mengine, wawe na taaluma nzuri mtu awe na shahada au shahada ya uzamili kwenye eneo la utungaji wa mitihani tu.

Natamani pia jamii ijue majukumu yetu sisi kama baraza, baraza ni kama daktari tu, ukija unapimwa na kuambiwa una vijidudu 10 vya malaria. Daktari akishakupa hayo majibu ni jukumu lako kuangalia kama unatumia neti au mazingira yako vipi na ufanye nini ili usipate tena malaria. Kwa sasa watu wanakuwa na mtizamo hasi sana.

Nimekaa miaka minane baraza, wakati naingia watoto walikuwa hawaandiki madudu lakini sasa hali ni ngumu, wanachora vitu vya ajabu wanaandika matusi, wengine wanaonyesha kabisa hawajui kitu walichokuwa wanafanya.Baada ya hali hiyo, watu wengine wanasema kwa nini mnapeleka mitihani shuleni na hakuna vifaa, wengine wanasema kwa nini mtihani mmoja wakati shule hazifanani, mimi nauliza kwa nini shule isiwe na vitabu.

Wanasema mitihani ilingane na mazingira, Watanzania wote tuko sawa, kama hakuna vifaa shuleni hiyi siyo kazi ya baraza, umma unabidi uelewe hilo. Kwa sasa kitu ambacho naona ni tishio kwa baraza na mitihani ni mitizamo watu. Wengi wanaukataa ukweli, muda wote anatumia nguvu nyingi kuukataa ukweli.

Suala ni la kweli kabisa lakini mtu anakataa mimi naona hiyo ni hatari sana, huwezi kutibu tatizo bila kujua na kuukubali ukweli, ili tuweze kuboresha elimu lazima tukubali ukweli na kukubali kurekebisha, hali ikiendelea ilivyo sasa huko mbele tutakuwa kwenye hali mbaya sana


Ponda asimamisha shughuli Morogoro

Sheikhe Ponda Issa Ponda akiwa chini ya ulinzi wa
askari magereza wakati akielekea katika mahakama ya
hakimu mkazi Morogoro kusikiliza kesi yake inayomkabili. 

Morogoro. Kiongozi wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu, Sheikh Ponda Issa Ponda jana alisababisha kusimama kwa shughuli za Serikali wilayani Morogoro baada ya ofisi kadhaa ikiwamo ya Mkuu wa Wilaya na baadhi ya mitaa kufungwa ili kupisha kusikilizwa kwa kesi inayomkabili katika Mahakama ya Mkoa wa Morogoro.

Tofauti na Agosti 19, mwaka huu wakati aliposafirishwa kwa helikopta, jana Sheikh Ponda alisafirishwa kwa barabara kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro akiwa chini ya ulinzi.

Mbali ya Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Morogoro kufungwa, nyingine ni Hazina Ndogo, Madini, Posta, Vipimo, Ukaguzi na Maktaba ya Mkoa.

Sababu za kufungwa kwa ofisi hizo pamoja na Mtaa wa Stesheni na maeneo ya Posta ni kuwa jirani na Mahakama hiyo. Magari yalizuiwa kutembea katika njia na maeneo ya karibu na ofisi pamoja na Mahakama hiyo huku kukiwa na idadi kubwa ya askari polisi na magereza kwa muda wote wa takriban saa mbili.

Alifikishwa mahakamani hapo saa 4:10 asubuhi akiwa katika basi la Magereza ambalo lilisindikizwa na jingine dogo, huku magari mengine yakisimamishwa kupisha msafara huo. Mahakama hiyo ilifurika umati wa wafuasi wa kiongozi kiasi cha kuwalazimu polisi na wana usalama wengine kuweka utepe kuwazuia wengi wao kufika katika jengo lililokuwa likitumika kuendesha kesi hiyo.

Shughuli katika eneo hilo zilirejea katika hali yake ya kawaida saa 6:25 mchana baada kesi yake kuahirishwa na msafara wa Sheikh Ponda kurejea katika Gereza la Segerea, Dar es Salaam ambako yuko rumande.

Muda wote tangu kuwasili mpaka kusikilizwa kwa kesi hiyo, wafuasi hao walikuwa kimya hadi pale ilipoahirishwa na hasa baada ya Sheikh Ponda kuwapungia mkono alipokuwa akielekea kwenye basi ambako walisikika wakisema: “Takbriir na kuitikia Allahu Akbar – (Mungu Mkubwa).”

Kesi yenyewe

Katika kesi hiyo, Wakili wa Serikali, Benard Kongola alisema mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mkoa wa Morogoro, Richard Kabate kuwa Sheikh Ponda alitenda makosa ya uchochezi Agosti 10, mwaka huu saa 11.45 jioni kwenye maeneo ya Kiwanja cha Ndege, Morogoro.

Alisema siku hiyo, Sheikh Ponda alialikwa kutoa maelezo machache kwenye Kongamano la Eid lililoandaliwa na Umoja wa Wahadhiri Mkoa wa Morogoro (Uwamo) na kwamba akiwa hapo alitamka maneno: “Ndugu Waislamu, msikubali uundwaji wa kamati za ulinzi na usalama za misikiti kwani kamati hizo zimeundwa na Baraza la Waislamu Tanzania (Bakwata), ambao ni vibaraka wa CCM na Serikali na kama watajitokeza kwenu watu hao na kujitambulisha kwamba wao ni kamati za ulinzi na usalama za misikiti, fungeni milango na madirisha ya misikiti yenu na muwapige sana,” huku akijua kutoa maneno hayo ni kosa kisheria.

Alisema kwa kufanya hivyo, Sheikh Ponda anayetetewa na mawakili watatu wanaoongozwa na Juma Nassoro, alivunja masharti ya Mahakama ya kifungo cha nje iliyotolewa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ya Mei 9, mwaka huu iliyokuwa imetamka kuhubiri amani.

Katika shtaka la pili, Sheikh Ponda anadaiwa kuwashawishi wafuasi wake kutenda kosa la jinai kwa kuwaambia: Serikali ilipeleka jeshi Mtwara kushughulikia suala la vurugu iliyotokana na gesi kwa kuwaua, kuwabaka na kuwatesa wananchi kwa sababu asilimia 90 ya wakazi wake ni Waislamu, lakini haikufanya hivyo kwa wananchi wa Loliondo waliokataa Mwarabu asipatiwe kipande cha ardhi ya uwindaji baada ya kudai ni mali yao kwa sababu asilimia 90 ya wakazi wake ni Wakristo.” Shtaka la tatu ni kudaiwa kutamka maneno yaliyoumiza imani ya watu wengine kama yalivyo katika shtaka la pili.

Baada ya kusoma mashtaka hayo, Kongola alisema walikuwa na mashahidi 15 na vielelezo vitatu ambavyo ni DVD mbili na kibali kilichotolewa na Mkuu wa Polisi Wilaya ya Morogoro(OCD), Agosti Mosi, 2013 cha kongamano husika na hati ya hukumu iliyotolewa na Mahakama ya Kisutu, Mei 9, 2013.

Baada ya kusomewa, Sheikh Ponda alikana mashtaka yote matatu huku akikubali kuwemo kwenye kongamano hilo. Alikiri kukamatwa na polisi Agosti 11, Dar es Salaam.

Wakili wa utetezi, Nassor aliwasilisha ombi la dhamana kwa mteja akisema mashtaka hayo yote kisheria yana dhamana. Pia aliwasilisha ombi la kupatiwa hati yenye maelezo ya mlalamikaji ambaye ni Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwani alisema kuwa kutokana na upelelezi upande wa mashtaka kukamilika, wanahitaji maelezo hayo kwa ajili ya kuandaa utetezi.

Hata hivyo, Wakili Kongola aliiomba Mahakama kutompa dhamana mshtakiwa kutokana na cheti kilichotolewa na Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), kupinga dhamana ya mshtakiwa huyo kwa masilahi ya usalama wa nchi.

Akitoa mwongozo wa maombi yaliyowasilishwa na pande zote mbili, Hakimu Kabate aliahirisha kesi hiyo hadi Septemba 11, mwaka huu itakapotajwa tena na kwamba Septemba 17, mwaka huu Mahakama itatoa uamuzi endapo mshtakiwa atapewa dhamana au la wakati itakapoanza kusikilizwa.

MWIGULU NCHEMBA ATAKA MBOWE NA DR. SLAA WAKAMATWE KWA MAUAJI YA RAIA

MBUNGE wa Iramba Magharibi, Mwigulu Nchemba (CCM), amechafua hali ya hewa bungeni kwa kuitaka Serikali kuwachukuliwa hatua viongozi wa juu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA). Mbunge huyo alisema mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe pamoja na Katibu Mkuu wake, Dk. Wilbroad Slaa, wanapaswa kuchukuliwa hatua kwa madai ya kusababisha mauaji ya raia.

Mwigulu, ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Bara, alisema katika kipindi cha miaka miwili tangu nchi ilipotoka kwenye uchaguzi, viongozi hao wamekuwa wakihamasisha maandamano na kusababisha umwagaji wa damu za Watanzania.

“Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha miaka miwili tangu nchi yetu ilipomaliza Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010, Mbowe na Dk. Slaa wamekuwa wakitoa kauli za wazi na hata kusababisha mauaji ya watu bila hatia.

“Kutokana na hali hii, sijui Serikali inafanya nini katika kuwachukulia hatua, kwani viongozi hawa wamekuwa wakitafuta umaarufu wa kisiasa kwa kuchochea chuki na mauaji dhidi ya raia.

“Kwa hali hiyo, tangu kipindi hicho hadi leo hii wanasubiri nini badala ya kwenda kuwaweka jela, kwani huko ndiko wanatakiwa kuwa,” alisema.

Mwigulu, alisema kukosekana kwa maadili kwa baadhi ya viongozi wa siasa, ambao wamekuwa wakitumia majukwaa na kuhubiri umwagaji damu ni hatari kwa taifa.

Alisema viongozi hao wamekuwa wakitumia majukwaa hayo na kusababisha vifo vya wananchi, huku akitaja vurugu zilizotokea katika mikoa ya Morogoro, Iringa, Arusha na Singida.

Akijibu swali hilo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Utawala Bora), George Mkuchika, alisema Serikali inafanya kazi kwa mujibu wa sheria, ikiwa ni pamoja na kukusanya ushahidi na kwamba mahakama ndicho chombo chenye uamuzi wa mwisho dhidi ya adhabu kwa raia au kiongozi yeyote wa kisiasa.

Kauli hiyo ya Mwigulu ilionekana kuchafua hali ya hewa ndani ya Bunge, ambapo Mbunge wa Nyamagana, Ezekiel Wenje (Chadema), alisimama na kuomba mwongozo wa Spika, huku akimtaka Mwigulu kuthibitisha kauli yake, vinginevyo aombe radhi.

Wenje alisema hoja ya Mwigulu imekosa mashiko na ina lengo la kuwadhalilisha viongozi wa Chadema, huku akisahau kuwa baada ya uchaguzi wa Arumeru Mashariki, aliyekuwa Mwenyetiki wa Chadema tawi la Usa River, Omari Mbwambo, aliuawa na watu anaodaiwa kuwa ni wafuasi wa CCM.

Awali katika swali la msingi, Mbunge wa Same Mashariki, Anne Kilango (CCM), alitaka kujua Serikali inachukua hatua gani kwa wanasiasa wanaokiuka maadili na kusababisha uvunjifu wa amani.

“Wanataaluma kama vile madaktari, wahandisi, wahasibu na hata wakandarasi pindi wanapokiuka maadili ya kazi zao huchukuliwa hatua kwa kufutiwa leseni zao.

“Vile vile viongozi wa kisiasa wanayo maadili yanayowaongoza, kwanini pale wanapokiuka maadili ya kazi zao hawachukuliwi hatua kama ilivyo katika makundi hayo? (taaluma),” alisema Kilango.

LUKUVI: WABUNGE WENGI WAMO ORODHA YA DAWA ZA KULEVYA


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi

Dodoma. Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi amesema baadhi ya majina ya wabunge yametajwa miongoni mwa watu wanaoshukiwa kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya lakini Serikali haiwezi kuwataja hadharani kwa haraka.

Majibu hayo ya Waziri Lukuvi yamekuja baada ya wabunge kumbana na wengine wakizomea baada ya kueleza ugumu wa kutaja majina ya washukiwa pasi na ushahidi wa kutosha.

“Serikali haiwezi kutaja majina haraka kiasi hicho kwani inaogopa kukurupuka na kushindwa mahakamani, hivyo lazima tuwe makini sana na jambo hilo. Hatuwezi kukurupuka tu eti ni fulani wakati hatuna vithibitisho.

“Kumbukeni wengine mpo humu ndani ya Bunge na tukianza wengi mtakwisha maana katika orodha hiyo kubwa na ninyi mmo na orodha ni kubwa kweli ambayo wakati mwingine inatakiwa umakini wa hali ya juu,” alisema Lukuvi alipokuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Karatu (Chadema), Mchungaji Israel Natse.

Katika swali lake ambalo lilisababisha kelele za kuzomea, Natse alitaka majina hayo yatajwe hadharani. Hata hivyo, hali ilitulia baada ya Spika wa Bunge, Anne Makinda kuingilia kati na kusema: “Hii tabia ya zomeazomea siitaki humu ndani, acheni tabia hiyo lazima mumsikilize mtu kwa kile anachokisema kwanza lakini mtindo huu si mzuri...”

Patashika hiyo ilitokana na swali la Mbunge wa Viti Maalumu (CCM), Catherine Magige aliyetaka kujua iwapo Serikali inaweza kuwaambia Watanzania ukubwa wa biashara hiyo nchini na kama haioni kama kuna tatizo katika ukaguzi wa abiria na mizigo katika viwanja vya ndege na juhudi za Serikali kumaliza tatizo hilo.

Akijibu swali hilo, Lukuvi alisema ukubwa wa biashara hiyo hapa nchini unadhihirishwa na idadi ya Watanzania 274 waliokamatwa kati ya mwaka 2008 hadi Julai mwaka huu kwa kosa la kujihusisha na dawa za kulevya katika nchi mbalimbali za nje.

Alisema Serikali inafahamu ukubwa wa tatizo la matumizi ya biashara hiyo haramu ya dawa za kulevya nchini na alitaja takwimu za ukamataji wa dawa hizo katika kipindi cha kuanzia mwaka 2000 hadi Machi, 2012.

Alisema pamoja na kukamatwa kwa Watanzania hao nje ya nchi, wageni 31 wanashikiliwa mahabusu katika Magereza ya Keko na Ukonga, Dar es Salaam ambao ni raia wa Iran, Pakistan, Senegal na Afrika Kusini.

Hata hivyo, katika swali lake la nyongeza, Magige alisema uteketezaji wa dawa zinazotajwa kukamatwa umekuwa wa siri kiasi cha kutiliwa shaka kuwa huenda zinachukuliwa na maofisa waliozikamata ndiyo maana hakuna uwazi.

Kuhusu hilo, Waziri Lukuvi alisema suala la uteketezaji wa dawa hizo hauko wazi kutokana na sheria zilizopo kutotoa nafasi ya kuteketezwa mapema kwa kuwa zinatumika kwa ajili ya ushahidi akisema wakati mwingine hukaa zaidi ya miaka 10.

Wednesday, August 28

TAARIFA YA RASMI YA KUREJESHWA URUSHAJI MATANGAZO RADIO IMAAN FM NA KWA NEEMA FM


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

KUREJESHWA KWA URUSHAJI MATANGAZO RADIO IMAAN FM NA KWA NEEMA FM RADIO

1.0 Utangulizi:

Mnamo tarehe 26/02/2013 Kamati ya Maudhui ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania ilitoa uamuzi wa kuvifungia vituo vya utangazaji vya Radio Imaan ya mjini Morogoro na Kwa Neema FM Radio ya jijini Mwanza baada ya kukiuka Sheria na Kanuni za Utangazaji.

Kamati ya Maudhui iliuita uongozi wa vituo hivyo tarehe 11/02/2013 na tarehe 14/02/2013 ili kujitetea na vyote vilikiri kosa. Baada ya kutafakari utetezi wa Radio Imaan na Radio ya Kwa Neema FM na kwa kuzingatia Sheria na Kanuni za Utangazaji, Kamati iliamua kutoa adhabu kwa vituo vyote viliwi kama ifuatavyo:-

a) Vituo vyote vilipewa onyo pamoja na kufungiwa kurusha matangazo kwa kipindi cha miezi sita kuanzia
tarehe 26/02/2013;

b) Vituo vyote vilitakiwa kuithibitishia Mamlaka ya Mawasiliano na Kamati ya Maudhui kwa maandishi kuwa hawatarejea kutenda kosa la aina hiyo au linalofanana na hilo. Ikiwa vitarudia Kamati ya Maudhui haitasita kuvifutia leseni zao za utangazaji.

2.0 Kutekeleza adhabu na hatua zilizochukuliwa na vituo hivyo na Mamlaka ya Mawasiliano:

Baada ya Uamuzi huo kusomwa, vituo vyote viwili vilianza kutekeleza adhabu mara moja kama ilivyotakiwa kwa mujibu wa Sheria na Kanuni za Utangazaji. Mamlaka ya Mawasiliano ilipokea barua ya udhibitisho wa kutofanya kosa tena yaani “Commitment letter” pamoja na sera ya uhariri (Editorial Policy) na ratiba ya vipindi kutoka kwa vituo vyote viwili.

Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania ilifanya ukaguzi kwa vituo vyote viwili ili kujiridhisha na kuzipitia sera za uhariri pamoja na mwongozo wa vipindi kabla ya kuvifungulia.

3.0 Kurejeshwa kwa Matangazo

Kamati ya Maudhui iliandika barua tarehe 27/08/2013 kuhusu kuvifungulia vituo hivyo vya utangazaji vya Radio Imaan ya mjini Morogoro na Kwa Neema FM Radio ya jijini Mwanza baada ya kutumikia adhabu kwa mujibu wa Sheria na Kanuni za Utangazaji. Vituo hivi vimeanza kurusha matangazo yake kuanzia leo tarehe 28/08/2013 baada ya muda wa adhabu kuisha.

Kamati ya Maudhui inapenda kutumia fursa hii kuvionya vyombo vya habari vya utangazaji vya redio na televisheni kuwa makini katika kutekeleza masharti ya leseni pamoja na kufuata Sheria na Kanuni za Utangazaji. Kamati ya Maudhui haitasita kutoa adhabu kali au kuvifungia vituo vitakavyokiuka Masharti ya leseni, Sheria pamoja na Kanuni za Utangazaji au hata kuvifutia leseni zao.

Kamati ya Maudhui inatoa wito kwa vyombo vya habari vya utangazaji kuzingatia Sheria, Kanuni na Masharti ya leseni ilikuboresha Sekta ya Utangazaji na kudumisha amani nchini.

Eng. Margaret Munyagi
Mwenyekiti,
Kamati ya Maudhui Ya TCRA,
S.L.P. 474,
DAR ES SALAAM.
28/08/2013

----

KUHUSU KAMATI YA MAUDHUI:

1.1. Kamati ya Maudhui ni kamati iliyoundwa kwa mujibu wa sehemu ya IV kifungu cha 26 (1) cha Sheria Namba 12 ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania ya mwaka 2003, na marekebisho yake katika kifungu 173 cha Sheria ya Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta (EPOCA) Mwaka 2010

Kwa mujibu wa sheria, majukumu na kazi za Kamati ya Maudhui ni pamoja na:-

(a) Kumshauri Waziri wa Sekta kuhusiana na Sera ya Utangazaji nchini;
(b) Kushughulikia malalamiko kutoka kwa watangazaji na watumiaji wa huduma za utangazaji nchini;
(c) Kusimamia na kuhakikisha kuwa kanuni za utangazaji zinafuatwa.
(d) Kusimamia na kufuatilia maudhui ya vituo vya utangazaji.

1.2. Kamati hii ilianza kazi zake Oktoba 2012 baada ya kuzinduliwa rasmi na Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Dk. Fenella Mukangara (MB) tarehe 4 Desemba, 2012.

1.3. Kamati ya Maudhui inaundwa na wajumbe watano. Wanne ni wateuliwa wa Waziri mwenye dhamana ya Sekta ya Utangazaji na Mwenyekiti ambaye huchaguliwa miongoni mwa wajumbe wa Bodi ya TCRA. Muundo huo umetolewa na sehemu ya 26 (2) ya Sheria ya TCRA ya Mwaka 2003.

Majina ya wajumbe ni kama ifuatavyo:-

i. Mhandisi Margareth Munyagi -Mwenyekiti
ii. Bwana Walter Bgoya -Makamu Mwenyekiti
iii. Bwana Abdul Ngarawa -Mjumbe
iv. Bwana Joseph Mapunda -Mjumbe
v. Bwana Yusuf Nzowa -Mjumbe

Sunday, June 30

LOWASSA AMTAKA OBAMA ASIZUNGUMIE MAMBO YA USHOGA NA NDOA ZA JINSIA MOJA AKIWA TANZANIA

Mwenyekiti wa Kamati ya Mambo yaNje na Ushirikiano wa Kimataifa, Edward Lowassa, amemtahadhalisha kujiepusha na kauli za kuunga mkono ushoga.

Lowassa ambaye pia ni Mbunge wa Monduli, ameliambia NIPASHE Jumapili ofisini kwake jijini hapa jana kuwa ushoga na hai za ndoa kwa watu wa jinsia moja vinaweza `kuiharibu’ ziara yake hapa nchini.

Mapema wiki hii, Rais Obama alikaririwa akizungumzia masuala hayo yanayotajwa kuwa ni moja ya haki za msingi za binadamu, alipokuwa Senegal, lakini akapingwa.

“Watanzania hawatalikubali na wataendelea kushikilia uhuru na heshima walizojengewa tangu awali, kwamba ushoga na ndoa za jinsia moja havikubaliki,” alisema.

Akiwa Senegal, Rais Obama alitaka serikali za Afrika kutoa haki kwa mashoga kama inavyotoa kwa raia wengine.

"Ninachotegemea, I pray and hope (ninasali na kutegemea) kwamba kuhusu mashoga na ndoa za jinsia moja, Rais Obama hatarudia kauli aliyoitoa kule Senegal,” alisema.

Aliongeza, "ninasema hivi kwa sababu Tanzania hatuamini katika ushoga, na endapo utawalazimisha Watanzania, watakukatalia na kushikilia uhuru na heshima waliyojengewa toka awali."

AHIMIZA MAPOKEZI MAZURI
Hata hivyo, Lowassa aliwataka Watanzania kuiheshimu na kuitumiavema fursa ya kutembelewa na Rais Obama, hivyo wajitokeze kumlaki kwa wingi.

"Tutambue mataifa makubwa yanakimbilia maslahi ya karne inayofuata, kwa mfano Rais wa China, Xi Jiping siku moja baada ya kuapishwa kwake alikuja hapa nchini, " alisema.

Hivyo, alitoa wito kwa Watanzania kuhakikisha maslahi na fursa za kiuchumi zinakuwa za kwanza kulindwa, kwa kuwa ziara hiyo itafungua milango zaidi kwa wawekezaji kuja nchini.

Pia, Lowassa alisema ziara ya Rais Obama ni kielelezo cha amani na usalama uliopo, na kwamba itasaidia kuwavutia watalii na wadau wa sekta nyingine za maendeleo kuitembelea Tanzania.

KITUO CHA KIJESHI
Kuhusu hofu na tetesi kuwa ziara hiyo imelenga taifa hilo kuja hapa nchini kufungua kituo cha kujiimarisha kiulinzi, Lowassa alisema Watanzania wanapaswa kufahamu kuwa tayari nchi hiyo ina kituo cha kijeshi nchini Kenya.

"Tuangalie maslahi yetu tuachane na mitazamo hasi, kama ni kituo cha kijeshi tayari kipo Kenya, tujiulize kwa nini marais wa Marekani Bill Clinton na George Bush walivyofanyaziara zao hapa nchini hawakwenda Kenya," alisema.

WALINZI WA NDANI KUWEKWA KANDO
Kuhusu ziara hiyo kutumia ulinzi wa kimataifa huku majeshi ya Tanzania yakiwekwa kando kwa ushiriki wa moja kwa moja, Lowassa alisema Rais wa Marekani ana kiwango cha juu cha ulinzi unaosimamiwa na nchiyake pekee.

"Ni sahihi walinzi wetu kukaa pembeni, huyu ni kama Rais wa dunia, lakini hata majeshi yetu yanafanya kazi ya ulinzi lakini sio kwamba yatakaa nyuma tu," alisema.

SUMAYE: TUMKARIBISHE
Naye, Waziri Mkuu mstaafu, Fredrick Sumaye, alisema ziara ya Rais Obama haina ujumbe zaidi ya kuhimiza watu wajitokeze kumpokea.

Hata hivyo, Sumaye alikwepa kuzungumzia kwa undani hatua ya kuwafukuza wafanyabiashara kutoka kandoni mwa barabara, ili kupisha mapokezi ya Rais Obama.

“Ninachokielewa ni kuwa barabara ambazo wanapita viongozi kama Rais Obama zinatakiwa kuwa katikahali ya usalama na hivyo kutakiwa kuboreshwa,” alisema.

LIPUMBA: MAFANIKIO NI MADOGO KIUCHUMI
Mwenyekiti wa Chama Cha Wananchi (CUF) Profesa Ibrahim Lipumba, alisema mafanikio ya ziaraya Rais Obama yapo katika kujitangaza kimataifa kuliko kiuchumi.

Profesa Lipumba ambaye ni mchumi aliyebobea, alisema changamoto iliyopo ni kwamba bado biashara kati ya nchi mbili hizo siyo kubwa kama ilivyo kwa nchi kama China na Tanzania.

Alitolea mfano, mwaka 2012 bidhaa za hapa nchini zilizouzwa Marekani zilikuwa na thamani ya Dola milioni 66 ikilinganishwa na zile zilizouzwa China ambapo zilikuwa ni zaidi ya Dola milioni 500.

Alisema bidhaa zilizoagizwa kutoka Marekani zilikuwa na thamani ya Dola milioni 230 huku za kutoka China zikiwa na thamani ya zaidi ya Dola milioni 1,100.

"Utakubaliana nami kuwa mahusiano yetu na China ni makubwa kuliko Marekani licha ya nchi hii kutoa fursa kwetu ambazo hatujazitumia ipasavyo," alisema

Profesa Lipumba alisema Marekani kupitia mpango wake wa kusaidia Maendeleo ya Afrika (AGOA), ulitoa fursa kwa bidhaa za Afrika kuuzwa nchini humo bila ushuru, lakini Tanzania haikuitumia.

Pia alisema utawala wa George Bush, uliisaidia Tanzania kupitia Mfuko wa Changamoto za Milenia (Millenium Challenge Compact (MCC) kupewa Dola milioni 700 kwa ajili ya kusaidia miundombinu na ujenzi wa nyaya za umeme kutoka bandarini hadi Zanzibar.

"Pana uwezekano wa mpango wa pili wa MCC, Tanzania ikapata msaada wa kuimarisha miundombinu ya umeme, lakini pia kampuni za Marekani kuja kuwekeza hapa kwetu," alisema.

Alisema uwekezaji wa kampuni hizoutategemeana na wafanyabiashara wa hapa nchini pamoja na serikali kutumia fursa mbalimbali za nchi hiyo.

Katika hatua nyingine, Profesa Lipumba alisema ili nchi iweze kujikwamua na umasikini itatokana na jinsi itakavyotumia sera na juhudina siyo kutegemea msaada kutoka nje.

HOTELI ZIMEJAA
Wingi wa wageni wakiwamo watakaofika kwa ajili ya ziara ya Rais Obama, umesababisha hoteli nyingi za jijini Dar es Salaam `kujaa’.

Uchunguzi wa NIPASHE Jumapili ulibaini kwamba kwa zaidi ya wiki sasa, hoteli nyingi hazikupokea wageni kutokana na kile kilichoelezwa kuwa, nyingine zililipiwa ingawa vyumba havikutumika kwa wakati.

POLISI: WASIO NA KAZI WASIJE MJINI
Kamanda wa Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani, Mohammed Mpinga, amewataka wananchi ambao hawatakuwa na mambo muhimu ya kufanya katikati ya jiji, wasifike huko kupunguza msongamano wa watu na magari baada ya kuwasili kwa Rais Obama.

Alisema, baadhi ya barabara zitafungwa kwa muda kwa ajili ya viongozi kuzitumia, hivyo kusababisha msongamano.

Hekaheka zimetanda jijini Dar es Salaam, ikiwa ni zaidi ya saa 24 kabla ya kuwasili kwa Rais Barack Obama.

Rais Obama, atawasili nchini kesho akitokea Afrika Kusini, ambapo pamoja na mambo mengine, alizungumza katika mkutano wa ‘viongozi vijana wa Afrika’ na kujibu maswali kutoka nchi tofauti.

Mkutano huo ulifanyika jana jioni huko Soweto nchini Afrika Kusini, ambapo alipokewaa na kujibu maswali kutoka Kenya, Uganda, Nigeria na Afrika Kusini kwenyewe.

Jijini Dar es Salaam, shughuli kadhaazikiwamo za ulinzi na usalama, zinafanyika kwa kasi na umakini kuhakikisha ziara ya Rais Obama inafanyika pasipo bughudha. kujibu maswali kutoka Kenya, Uganda, Nigeria na Afrika Kusini kwenyewe.

Jijini Dar es Salaam, shughuli kadhaazikiwamo za ulinzi na usalama, zinafanyika kwa kasi na umakini kuhakikisha ziara ya Rais Obama inafanyika pasipo bughudha.

Hata hivyo, sehemu kubwa inayohusu masuala ya itifaki, ulinzi na usalama yanafanywa na taasisi za Marekani, kwa kuzishirikisha taasisi za ndani kwa kiwango kidogo.

“Hawa jamaa (Wamarekani) wanapoingia nchi yeyote wakiwa naRais wao, shughuli nyingi na uamuzi wanafanya wao, sisi wa ndani inakuwa kushirikishwa kwa kiasi kidogo,” kilieleza chanzo cha NIPASHE Jumapili kutoka moja ya taasisi zinahusika katika ziara hiyo.

Maeneo kadhaa ya jijini humo, yaliendelea kudhibitiwa kwa ulinzi mkali na doria za mara kwa mara, huku kandoni mwa baadhi ya barabara wakionekana askari wa Jeshi la Wananchi (JWTZ).

Mathalani, kandoni mwa barabara ya Morogoro, eneo la Ubungo, walionekana askari wa JWTZ maarufu kama MP.

Shughuli nyingine zimehusisha pia operesheni zinazofanywa na polisi kwa kusaidiana na mgambo wa jiji, kuhakikisha watu na bidhaa zilizopokandoni mwa barabara zitakazotumika kwa ziara ya Rais Obama, vinaondolewa.

Magari yaliyowabeba polisi wenye silaha za moto na mabomu ya machozi, yalionekana katika mitaa kadhaa jijini humu, wakihakikisha operesheni hiyo inafanyika pasipo kikwazo kutoka kwa wahusika.

Kila palipofanyika operesheni hiyo, baadhi ya askari walifanya doria zamu kwa zamu, kuhakikisha kuwa bidhaa na watu walioondolewa, hawarejei.

Hata hivyo, waathirika katika operesheni hiyo walieleza kutofurahia, huku wakihoji ni kwa nini serikali haikuwaandalia mazingira mbadala kabla ya utekelezaji wake.

Walisema miongoni mwao, wamekopa mitaji kutoka kwenye taasisi za kifedha, hivyo kusimamisha biashara zao ili kupisha ujio wa Rais Obama, kutawaweka katika hali ngumu kiuchumi.

“Ikiwa ujio wa Rais Obama unatutesa wafanyabiashara kiasi hiki, ni vigumu kuhimili maisha yetu, kwa sababu hatujui hatma yetu baada ya yeye kuondoka,” alisema mfanyabiashara Zena Rashidi wa Kariakoo.

Hata hivyo, wamachinga walionekana jana katika kituo cha mabasi cha Mwenge walipofukuzwa, wakiwa wanaendelea na biashara zao.

Lakini walifanya hivyo kwa tahadhali ikiwamo kushika bidhaa chache mikononi, huku wakitumia 'janja' ya kupiga kelele za 'kumsifia' Rais Obama.

Walisikika miongoni mwao wakisema, 'praise to Obama' na wengine wakaitikia 'aaamen'. Walifanya hivyo zamu kwa zamu, lakini haikujulisha waliashiria nini.


BARABARA ZAPAMBWA
Aidha, barabara zote atakazopita Obama wakati wa ziara yake zimepambwa kwa bendera za Marekani na Tanzania; huku zikinakshiwa kwa picha yake ambayo imeandikwa 'President Barack Obama' karibu Tanzania.

Barabara hizo ni ile ya Nyerere kuanzia uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius K. Nyerere, Ali Hassan Mwinyi, Mwai Kibaki na Bagamoyo.

Imeshuhudia pichana bendera hizo zikiwa zimewekwa kwenye mabango yote yaliyo barabarani kuanzia Ikulu hadi kwenye barabara hizo huku usafi wa jiji ukionekana kuimarika zaidi.

Jana ilishuhudiwa karibu barabara zote, vijana wanaofanyakazi ya kuweka bendera na picha ya Obama wakifanyakazi hiyo.

Friday, June 21

"POLISI WATAENDELEA KUWAPIGA WALETA VURUGU HAPA NCHINI NA NINASEMA WAWAPIGE ZAIDA NA ZAIDA"... WAZIRI MKUU

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ameagiza vyombo vya dola kuwashughulikia kwa kuwapiga wale watakaokataa kutii amri wakati wakifanya vitendo vya uvunjifu wa amani.

Akizungumza katika Kipindi cha Maswali ya Papo kwa Hapo kwa Waziri Mkuu, bungeni Dodoma jana, Pinda alisema watu wanapokaidi wanajitakia matatizo na vyombo vya dola.

Alisema hayo alipokuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Kilwa Kaskazini (CCM), Murtaza Mangungu aliyeuliza: “Serikali ipo tayari kiasi gani kubainisha na kuchukua hatua stahiki, badala ya kusakama makundi fulani, tujue chanzo halisi cha vurugu hizi na matatizo haya na jinsi gani vyombo vya dola vinavyoshughulikia kwa sababu yapo malalamiko katika baadhi ya maeneo kama Mtwara kwamba wananchi wanapigwa na vyombo vya dola?”

Waziri Mkuu alijibu: “Ni lilelile nililosema... mwishowe unaona anasema vyombo vya dola vinapiga watu. Ukifanya fujo, umeambiwa usifanye hiki, ukaamua kukaidi, utapigwa tu... hamna namna nyingine, maana wote tukubaliane kwamba nchi hii tunaiendesha kwa misingi ya kisheria.

“Sasa kama wewe umekaidi, hutaki unaona kwamba ni imara zaidi... wewe ndiyo jeuri zaidi watakupiga tu.... Mimi nasema muwapige tu, kwa sababu hakuna namna nyingine... maana tumechoka.”

Pinda alisema Serikali imedhamiria kurejesha amani nchini ikiwamo mkoani Mtwara na kuwataka Watanzania waiache Serikali ifanye kazi hiyo. Alisema Serikali ina orodha ya watu wanaosemekana kuwa ni vyanzo vya vurugu na matatizo yaliyotokea Mtwara na kushangaa wale wanaopinga kukamatwa kwao.

“Lazima tuwakamate na kama katika kuwakamata watafanya jeuri, jeuri, watapigwa tu kabla ya kupelekwa tunapotakiwa kuwapeleka, kwa sababu hatuwezi kuendelea na hali hii, mkadhani kwamba tutafika tunapokwenda. Nami nasema vyombo vya dola vijipange imara vihakikishe vinadhibiti hali hii,” alisema.

Hata hivyo, jibu hilo lilipata upinzani wakati Mbunge wa Konde (CUF), Khatibu Said Haji alipomwuliza Waziri Mkuu: “Hapo awali umetoa kauli nzito ya kuliambia taifa hili kwamba wale raia wote, ambao watakaokuwa wakaidi wapigwe tu na watapigwa tu; naomba ninukuu Katika Ibara ya 13 na Kifungu cha 6B cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano.

“Ni marufuku kwa mtu yeyote aliyeshtakiwa kwa kosa la jinai kuteswa kama mtu mwenye kosa, mpaka itakapothibitika anayo hatia kwa kutenda kosa hilo.

“Pia ibara hiyohiyo Kifungu cha 6 E; kinasema ni marufuku kwa mtu yoyote, kuteswa, kuadhibiwa kinyama au kupewa adhabu zinazoweza kumdhalilisha. Kwa kauli yako uliyoitoa huoni kwamba umevunja Katiba?” Akijibu swali hilo, Pinda alisema ni lazima kutofautisha kati ya mtu aliyekwishakamatwa na kufikishwa mbele ya vyombo vya sheria... “Mimi ninayemzungumza hapa ni mtu yule ambaye ameamua kufanya vitendo hajakamatwa na ndiyo maana nilikwambia usiandamane... hapa mahali hutakiwi kwenda wewe ukaamua kutumia mabavu kwa sababu mko wengi, ndiyo maana nikasema, hawa watu tutashughulika nao hivyohivyo.”

Mbunge huyo hakuridhishwa na majibu hayo na kumtaka Waziri Mkuu kuyafuta.

Hata hivyo, Spika wa Bunge, Anne Makinda aliingilia katika na kumweleza mbunge huyo kuwa kila mtu alikuwa amemwelewa Waziri Mkuu na hakukuwa na haja ya kuendelea na hoja hiyo.

Kabla ya swali lake la nyongeza, Mangungu aliuliza: “Ukisikiliza nyimbo nyingi za taifa katika Afrika zinasema hekima, umoja na amani ndiyo ngao zetu. Je, hali ambayo imejitokeza katika nchi yetu na matatizo yaliyojitokeza Arusha na maeneo mengine kama Mtwara. Nini tamko la Serikali?

Waziri Mkuu alijibu: “Swali lililoulizwa na Mheshimiwa Mangungu ni jambo linalotugusa sisi wote. Suala la amani, ulinzi, utulivu ndiyo hasa tunu ya kila nchi ingependa kuwa nayo. Ni kweli hivi karibuni kumejitokeza vurugu za hapa na pale kwa hiyo angependa tuwaeleze Watanzania kama Serikali tunafikiria tufanye nini.

Alisema ipo haja ya jukumu hilo kuachwa kwa viongozi wa kisiasa bila ya kujali itikadi zao... “Yako mambo ambayo lazima tukubali kwamba ni jukumu letu sisi wote na kila mmoja lazima azungumze lugha moja.

Ninyi wote ni mashahidi. Chadema waliposhinda hapa, wao walikuja waziwazi, wakasema tutahakikisha nchi hii haitawaliki. Sasa, inawezekana pengine ndiyo mwendelezo wa utekelezaji wa kauli hizo.

“La pili ni upande wa Serikali, lazima tuhakikishe kwamba wale wote ambao kwa kweli wanajaribu kuvunja amani kwa namna yoyote ile, kazi kubwa tuliyonayo ni kubanana, kupambana kwelikweli kwa njia zozote zile zinazoonekana zinastahili.

“Sasa mimi ninaomba sana Watanzania, maana kila juhudi zinapoonekana zinaelekea huko, unapata watu wengine wanajitokeza, unajua...unajua. Acheni Serikali itimize wajibu wake kwa sababu jambo hili ni la msingi, lazima tulilinde kwa nguvu zetu zote.

“Rai yangu kwa Watanzania kila mmoja ajue kwamba siku tukiingia katika vurugu, hakuna mshindi. Wote tutaumia, sasa wote tuhakikishe hili jambo tunalisimamia vizuri.”

Chadema waja juu

Akizungumzia kauli hiyo, Mkurugenzi Habari na Uenezi wa Chadema, John Mnyika alisema: “Kauli ya Pinda inakiuka Katiba ya nchi na imethibitisha kwamba matumizi mabaya ya vyombo vya dola na kusababisha mauaji ya raia yana baraka za Serikali.”

Alisema kauli ya Pinda kama ilivyokuwa ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi zinatoa mwelekeo kwamba mauaji ya Arusha yana baraka za Serikali.

Wanasheria wakerwa

Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk Hellen Kijo-Bisimba alisema Waziri Mkuu hakustahili kutoa kauli kama hiyo.

Alisema Pinda hapaswi kuwa na jazba, bali anatakiwa kuwa na busara na kuzungumza kwa kuzingatia sheria za nchi badala ya kutoa matamshi ambayo siyo mwafaka kwa nchi inayoongozwa kwa kufuata sheria na taratibu.

Rais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), Francis Stola alisema kauli hiyo ya Waziri Mkuu, mbali ya kwenda kinyume cha Katiba na sheria ya nchi, inaweza kuhatarisha amani.

Stola alisema matumizi ya nguvu kupita kiasi kudhibiti hali yoyote korofi hayaruhusiwi.

Mbowe, Lema wahojiwa polisi,watoa msimamo

Arusha. Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema jana, walijisalimisha Makao Makuu ya Polisi ya Mkoa wa Arusha na kuhojiwa kwa zaidi ya saa nne kabla ya kuachiwa kwa kujidhamini wenyewe huku wakitakiwa kurejea kituoni hapo, Julai 22, mwaka huu.

Pia Mbowe na Lema wamemtaka Rais Jakaya Kikwete kuunda tume huru ya uchunguzi wa kimahakama ili kuchunguza vurugu za Arusha zilizoanza Jumamosi iliyopita baada ya bomu kurushwa kwenye mkutano wa Chadema na kusababisha vifo pamoja na zile zilizofuatia wakati polisi ilipowasambaratisha wafuasi wa chama hicho kwa mabomu walipokusanyika kwenye Viwanja vya Soweto kwa lengo la kutoa heshima za mwisho kwa marehemu.

Wakiongozwa na mawakili watatu, Mbowe na Lema waliwasili polisi saa 3.50 asubuhi na kuhojiwa hadi saa 9.10.

Viongozi hao walipokewa na Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Arusha, Diwani Nyanda kabla ya kutenganishwa kwenye vyumba viwili tofauti kwa mahojiano.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, Mbowe, Lema na wakili Albert Msando walitaja mambo mawili ambayo polisi waliwahoji kwanza ikiwa ni ushiriki wao katika mkusanyiko usio halali kwenye Viwanja vya Soweto, Jumanne iliyopita ambao ulisambaratishwa na polisi.

Jambo jingine ambalo polisi iliwahoji ni kauli yao ya kuwa na ushahidi unaohusisha polisi na tukio la bomu lililorushwa kwenye mkutano wa Chadema na kusababisha vifo vya watu wanne huku zaidi ya 60 wakijeruhiwa.

Mbowe alisema kwa pamoja wamewaeleza polisi kuwa hawaamini kama mkusanyiko wa Jumanne iliyopita haukuwa halali kwa sababu waliruhusiwa kuzungumza na wananchi waliokusanyika ili kuwashawishi watawanyike.

“Mkuu wa Polisi Wilaya (OCD) wa Arusha, Gilles Mroto ndiye aliyeturuhusu kuzungumza na wananchi wale kuwataka watawanyike na ndicho tulichofanya, lakini tukashangaa kuanza kupigwa mabomu mara baada ya kuwataka watu wanaotaka kutoa heshima za mwisho kwa marehemu kwenda Hospitali ya Mount Meru,” alisema Mbowe.

Alisema Mkuu wa Operesheni wa Polisi, Kamishna Paul Chagonja kuwa naye aliyewaomba viongozi wa Chadema kuwatawanya wafuasi wa chama hicho baada ya kuzuiwa kutoa heshima za mwisho katika viwanja hivyo vinavyomilikiwa na Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Arusha (AICC).

Msimamo wa Mbowe

Kuhusu ushahidi anaodai unawahusisha polisi na tukio la bomu, Mbowe alisisitiza kuwa Chadema kina ushahidi wa kutosha kuthibitisha hilo lakini alisema hakitaukabidhi mikononi mwa polisi.

Alisema hakitafanya hivyo kwa kuwa jeshi hilo ni watuhumiwa wakuu hivyo hawawezi kuwa na dhamira na nia njema katika upelelezi wao. Alisema ndiyo maana badala polisi kuwaona ni msaada, kimeanza kutoa vitisho kwa wote wanaosema waliwashuhudia askari wakishambulia watu kwa risasi kabla ya kuondoka na aliyerusha bomu kwenye gari lao.

“Chadema tuko tayari kukabidhi ushahidi huu kwa tume huru ya uchunguzi ya Mahakama. Rais Kikwete atumie mamlaka yake ya kikatiba kuunda tume kuchunguza tukio la bomu Arusha ili ukweli ujulikane. Polisi ni watuhumiwa katika jambo hili, hivyo hawana dhamira safi na ushahidi wetu,” alisema Mbowe.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas alisema polisi inawasiliana na wanasheria kutafuta ushauri wa hatua za kuchukua... “Polisi ndiyo wenye jukumu la kuchunguza na kukusanya ushahidi wote kuhusiana na matukio ya uhalifu. Hili ni jukumu la kisheria la polisi. Chadema wakabidhi ushahidi wao badala ya kupiga danadana ya kutaka tume huru ya uchunguzi ya kimahakama.”

Alisema hata ikiundwa tume, bado jukumu la kuchunguza na kukusanya ushahidi litarejeshwa mikononi mwa polisi, hivyo Chadema wanapaswa kutimiza wajibu wa kusaidia uchunguzi kwa kuwasilisha ushahidi wao wa polisi kuhusika katika tukio la bomu.



Askofu alia na dola

Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Jimbo la Arusha Mashariki, Isaac Kisir ameitaka Serikali kuchukua hatua kali kulinda usalama huku akivitaka vyombo vya ulinzi na usalama kujitathmini kiutendaji.

Akizungumza katika ibada ya mazishi ya aliyekuwa kada wa Chadema, Judith Moshi iliyofanyika katika Usharika wa Sokoni One, Askofu Kisir alisema mlipuko wa bomu haukuwa mapenzi ya Mungu, bali ni ugaidi.

“Tunapomzika mwenzetu lazima tuseme ukweli, tusimung’unye maneno, ukweli utatuweka huru. Nchi yetu sasa haina usalama ule tuliokuwa nao. Kumekuwa na utekaji nyara watu wanaosema ukweli. Kumekuwa na matumizi ya nguvu kupita kiasi kwa vyombo vya usalama, uchomaji wa makanisa na milipuko ya mabomu.

“Tulitegemea Serikali itatoa adhabu kwa wanaohusika lakini tunasikia maneno ya kejeli… mara tuko mbioni, mara tuko imara, huku watu wanauawa na kupata vilema.”

Judith ni mmoja wa watu wanne waliouawa katika shambulio la bomu lililolipuka wakati wa kuhitimisha kampeni za udiwani za Chadema katika Viwanja wa Soweto Juni 15 mwaka huu, huku watu wengine zaidi ya 60 wakijeruhiwa.

"EDWARD LOWASSA ANAHUSIKA NA KUTEKWA KWANGU PAMOJA NI KIPIGO NILICHOPEWA"...NASSARI


Mbunge wa Arumeru Mashariki (Chadema), Joshua Nassari amemtuhumu Mbunge wa Monduli Edward Lowassa kwamba anahusika na kipigo alichokipata kutokana na chuki aliyonayo kwake.

Aidha amemtuhumu Spika wa Bunge, Anne Makinda kwamba naye ni miongoni mwa watu wanaomchukia pamoja na viongozi wengine wa Bunge, kwa kuwa hakuna kati yao aliyempigia simu au kumtumia ujumbe wa kumjulia hali kutokana na kipigo alichopata ambacho kimemsababishia maumivu makali.

Akizungumza jana akiwa kwenye chumba alicholazwa katika Taasisi ya Tiba ya Magonjwa ya Mifupa na Ufahamu Muhimbili (Moi), Nassari alidai Lowassa ambaye amewahi kuwa waziri mkuu kabla ya kujiuzulu, amemchukia tangu alipomshinda mkwewe Sioi Sumari, kwenye uchaguzi mdogo wa ubunge uliofanyika Aprili mwaka jana.


Nassari aliyekuwa amelazwa katika Hospitali ya Selian ya jijini Arusha kabla ya kuhamishiwa MOI, alidai kupigwa na kuchaniwa nguo na Green Guard wakati alipokuwa katika jitihada zake za kuhesabu kura kwenye uchaguzi wa udiwani wa Kata ya Makuyuni-Monduli.

“Kipigo nilichopata Lowassa anahusika ananichukia, anataka urais lakini hawezi kuupata kwa kuuumiza watu kama hivi, alifikiri kwamba nitakufa sitakufa hadi kwa mapenzi ya Mungu,” alisema.

Alisema kuna jambo ambalo wananchi wanapaswa kulifikiria ni jinsi ambavyo kumekuwa na matukio ya kutekwa na kuvamiwa, lakini hakuna yanayohusisha kiongozi wa CCM, badala yake ni raia wa kawaida na viongozi wa dini na siasa. Nassari alidai akiwa kama wakala mkuu wa Chadema katika kata hiyo, alikumbana na mambo kadhaa yaliyomshangaza, ikiwa ni pamoja na kufanyiwa jaribio la kutekwa mara mbili, kabla ya kushambuliwa kwa kipigo.

Alisema pia anashukuru kwamba askari wawili waliokuwepo katika eneo hilo walijitahidi kutaka kumnusuru, lakini walizidiwa nguvu na vijana hao, hasa kutokana na kutokuwa na bunduki, ambapo yeye alipofanikiwa kuchoropoka alikimbilia bastola yake na kuwanyoshea vijana hao bila kufyatua.

Akizungumzia kuhusu hali yake, Nassari alisema amepimwa kipimo cha X-ray ambapo imeonyesha kuwa pingili za mgongo wake zipo sawa, lakini daktari ameshauri afanyiwe kipimo kingine kiitwacho MRI ili kuangalia hali ya mishipa kutokana na maumivu makali anayoendelea kuyapata.

Aidha alitumia fursa hiyo kumshukuru Mbunge wa Kuteuliwa, Joseph Mbatia kuwa ndiye aliyemsaidia kufanya mipango kuwasiliana na uongozi wa Bunge na kumwezesha kuhamishiwa Moi, baada ya wabunge wote wa Chadema kwenda Arusha kushughulikia waliofariki kwa bomu.

Hata hivyo, Lowassa alipotafutwa kuhusiana na tuhuma hizo alikataa kuzungumzia suala hilo na kusema hilo aulizwe Msimamizi wa Uchaguzi, Paulo Kitaleki.

Mwananchi ilimtafuta Kitaleki ambaye pia ni katibu tarafa, alikanusha kuhusika kwa Lowassa akielezea kuwa siku ya tukio hilo alikuwa Geita.

“Huyu Nassari ni mwigizaji na anafaa kuwa msanii kwa kuwa anaigiza tu hata hakupigwa, bali yeye ndiyo aliyempiga Wakala wa CCM, Hussein Osama ambaye ni mlemavu, kisha akatimua mbio baada ya vijana kutaka kumkamata, nashangaa kumwona yupo hospitali akidai kupigwa, siyo kweli,” alisema Kitaleki.

Mwananchi

Wednesday, June 19

SABABU ZA JESHI LA POLISI KUTUMIA NGUVU YA MABOMU JIJINI ARUSHA MUDA HUU


Jeshi la polisi limekipiga marufuku chama cha demokrasia na maendelo(CHADEMA)kufanya shughuli zozote za kuaga miili ya marehemu kwenye viwanja vya Soweto kwani zoezi la uchunguzi bado linaendelea kwenye viwanja hivyo .

Akizungumza ofisini kwake kamanda wa polisi mkoani Arusha, Liberatus Sabas amesema kutokana na uchunguzi unaoendelea wa tukio la bomu kwenye viwanja hivyo imeonelea kuwa si busara kuweka mkusanyiko wa watu kwani kutaharibu upelelezi.


Kamanda Sabas amedai  kuwa  jeshi la polisi  liliwataka viongozi wa chama hicho kuwaeleza wafuasi wao mahali sahihi watakapoweza kufanyia shughuli hiyo lakini si kwenye viwanja hivyo.

Hali kwenye viwanja hivyo imekuwa ya pilika pilika tangu juzi kwa wafuasi wa chama hicho kujikusanya tokea asubuhi hadi jioni kwa madai ya kuomboleza ..

Hata hivyo viongozi wa chama cha demokrasia na maendeleo walikaidi agizo hilo na  kuanza  kujikusanya uwanjani hapo pamoja na wafuasi wa CHADEMA , hali iliyoleta  mvutano kati ya viongozi  wa jeshi la polisi na  wafuasi hao.

Wakati mabishano hayo yakiendelea, Askari Polisi mmoja  alijichanganya na kuingia katikati ya wafuasi wa Chadema pembeni mwa uwanja huo ambao walikua wanasubiri kujua utaratibu wa kuaga miili ya Marehemu waliolipuliwa na bomu June 15 2013.

Baada ya hapo,Wafuasi hao hawakupenda kitendo cha Polisi kujichanganya nao hivyo ikazuka ugomvi huku wakitaka atoke, baada ya dakika kadhaa  mabumu yalianza kusikika.

Baadhi ya viongozi wa juu wa chama hicho waliokuwepo uwanjani haponi mbunge wa jimbo la ubungo John Mnyika,Ezekia Wenje,Tundu lissu, Halima Mdee...