Wednesday, September 4

Wabunge Z’bar wakwamisha Muswada wa kura za Maoni - mwananchi

Dodoma. Muswada wa Sheria ya Kura ya Maoni wa mwaka 2013 uliokuwa ujadiliwe katika mkutano wa 12 wa Bunge unaoendelea mjini Dodoma, umeondolewa na sasa utajadiliwa Bunge lijalo.

Habari za uhakika zilizopatikana jana, zilisema kwamba kuahirishwa huko kumetokana na wajumbe wa Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala ya Bunge wanaotoka Zanzibar kupinga vikali kura ya maoni kupigwa visiwani humo kwa kuwa tayari huko kuna sheria hiyo.

Muswada huo ulikuwa ujadiliwe na wabunge katika kikao cha Bunge kinachoendelea ukitanguliwa na Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya mabadiliko ya Katiba wa mwaka 2013.

“Ukisoma huu Muswada unasema kura hiyo itapigwa Tanzania Bara na Zanzibar sasa sheria hii ina apply vipi (inatumikaje) Zanzibar wakati kule tuna sheria yetu tayari?” alihoji Mbunge mmoja wa Zanzibar.

Kaimu Katibu wa Bunge, John Joel alipoulizwa jana, alithibitisha kuondolewa kwa muswada huo wa kura ya maoni kusema na utakaojadiliwa ni ule wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba pekee.

“Bunge litaahirishwa Ijumaa (keshokutwa) na ni kweli huo Muswada wa Kura ya Maoni umeondolewa kwa sababu bado uko kwenye ngazi ya kamati,” alisema Joel.

Alipoulizwa sababu za kuondolewa kwa muswada ambao ulishaingizwa kwenye ratiba ya Bunge, alitaka swali hilo aulizwe Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi.

Waziri Lukuvi alithibitisha kuondolewa kwa muswada huo na kusema utajadiliwa katika Mkutano wa Bunge wa Oktoba.

“Ni kweli muswada huu hautajadiliwa na Bunge hili bado kuna mashauriano yanaendelea kati ya SMZ (Serikali ya Mapinduzi Zanzibar) na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” alisema.

Kwa upande wake, Mnadhimu Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Tundu Lissu alisema wabunge wa Zanzibar ndiyo waliokwamisha muswada huo kutokana na mgongano wa sheria.

“Wao wanasema masuala ya kura ya maoni siyo ya Muungano kwa sababu wao tayari wana sheria yao ya kura ya maoni. Sasa wanahoji inakuwaje sheria hii itumike tena hadi Zanzibar? Huu ni mgongano,” alisema.

Lissu ambaye pia ni Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), alisema tangu mwanzo aliliona suala hilo na kuitahadharisha Kamati ya Bunge kwamba mapendekezo hayo yana upungufu.

Muswada pekee uliobaki wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba unatarajiwa kuwasilishwa leo huku ukitarajiwa kuibua mjadala mzito kutokana na misimamo ya baadhi ya wabunge.

Muswada huo unawasilishwa wakati CCM kikiwa kimeweka msimamo wa kupinga baadhi ya mambo katika Rasimu ya Katiba.



Yanayotarajiwa kuzua mjadala

Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe amekiri kupokea mapendekezo kutoka kwa wabunge na hasa kwenye Sheria ya Marekebisho ya Mabadiliko ya Katiba akisema wametaka kuangaliwa upya kwa kipengele cha Kamati ya Uteuzi ya viongozi wa Bunge la Katiba. Alisema sasa wataweka sifa za mwombaji wa nafasi hizo na wasiokuwa nazo hawatagombea.

Muswada wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba unataka wawakilishi kutoka makundi ya jamii kuwa 166 katika Bunge la Katiba, lakini wabunge wanataka idadi iwe 200.

Mbunge wa Muhambwe, Felix Mkosamali (NCCR-Mageuzi) alisema uzoefu katika nchi nyingine unaonyesha kuwa mabunge ya Katiba hushirikisha watu wengi ili kupata uwakilishi mpana tofauti na mapendekezo yaliyotolewa.

Mkosamali ambaye pia ni mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala, alisema ni vyema sheria ikasema wajumbe wa Bunge hilo watatoka katika taasisi zipi.

Kifungu kingine ni kile kinachohusu Kamati ya Uteuzi wa Mwenyekiti na Makamu wake ambao kwa mujibu wa muswada itaundwa na Spika wa Bunge la Jamhuri na Spika wa Baraza la Wawakilishi, Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (AG) na yule wa SMZ, Waziri wa Katiba na Sheria Tanzania Bara na Waziri wa Katiba na Sheria wa Zanzibar na Kiongozi Rasmi wa Kambi ya Upinzani Bungeni.

Mkosamali alisema muswada huo wa Mabadiliko ya Katiba unasema mwenyekiti wa muda atakuwa Spika wa Bunge lakini akataka: “Mwenyekiti wa muda atokane na Chama cha Majaji wastaafu maana wao hawafungamani na upande wowote.”

No comments:

Post a Comment