Saturday, December 24

Serikali yapiga marufuku shule binafsi kufanya mitihani ya kuchuja wanafunzi

Serikali imepiga marufuku utaratibu wa shule binafsi kuendesha mitihani ya mchujo kwa wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya kitaifa ili shule zao ziweze kuongoza kwa kubaki ma wanafunzi wazuri(walio na uwezo mzuri darasani)

Agizo hilo pia linapiga marufuku kuwafukuza shule wanafunzi wanaoshindwa mitihani ya mchujo,kuwasajili kama private candidate wale wanafunzi wanaofeli mitihani hiyo,kuwahamisha shule au kuwakaririsha madarasa.

========

Kibano kipya chaja kwa shule binafsi
Hiyo ni baada ya kutangaza kupiga marufuku utaratibu wa kuwachuja wanafunzi wanaotakiwa kufanya mitihani ya taifa uliokuwa unaofanywa na baadhi yao kwa lengo la kuonekana shule zao zinafaulisha vizuri.

Hivi karibuni, Nipashe iliripoti kuhusu hofu ya baadhi ya shule hizo; za msingi na sekondari ziko hatarini kubadilishwa matumizi kutokana na kukosa wanafunzi wa kutosha baada ya Serikali kuboresha shule zake na kutoa elimu bure, huku hali ya kiuchumi ikiwaumiza wananchi.

Huku udahili kwenye shule za serikali ukiongezeka na kuonekana kuwa tishio kwa ustawi wa shule za watu na taasisi binafsi, imewabana tena wamiliki wa shule binafsi kwa kuwazuia kufanya mchujo wa wanafunzi wanaoingia kwenye madarasa au vidato vyenye mitihani ya taifa.

Mmoja wa wazazi aliliambia Nipashe kuwa mwanawe anayesoma kidato cha tatu katika shule moja ya binafsi jijini Dar es Salaam, amepangiwa kuhamishiwa shule nyingine ya mmiliki huyo huyo kutokana na kufaulu kwa daraja la tatu.

Kwa mujibu wa mzazi huyo, kuna wanafunzi takribani 70 wa kidato cha tatu, wanatarajiwa kuhamishwa katika shule hiyo waliyosajiliwa tangu kidato cha kwanza, watahamishwa shule hiyo na kubaki wale waliofaulu kwa viwango vya madaraja ya kwanza na pili tu.

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dk. Leonard Akwilapo, akizungumza na Nipashe jijini Dar es Salaam juzi, alisema ni marufuku shule kumkaririsha darasa, kumfukuza, kumhamishia shule nyingine au kumsajili kama mtahiniwa binafsi (PC) mwanafunzi kwa kigezo cha kutofanya vizuri katika mitihani ya shule husika.

"Ni marufuku kabisa kufanya hivyo. Mitihani tulionayo sisi (Wizara ya Elimu) ndiyo mchujo sahihi. Na mtihani ambao unamkaririsha mwanafunzi ni mtihani wa taifa wa kidato cha pili na mtihani wa darasa la nne tu," alisema.

"Wala siyo mtihani wa shule na madarasa mengine hayana mtihani wa kumkaririsha mtoto au kumfanya aondolewe shuleni au ahamishiwe shule nyingine, hatuna utaratibu huo na serikali haiwezi kukubaliana nao," aliongeza Dk. Akwilapo.

Katibu Mkuu wa Chama cha Wamiliki wa Shule na Vyuo Binafsi (Tamongosco), Benjamin Nkonye, aliiambia Nipashe jana kuwa utaratibu wanaoutumia ni kushauriana na wazazi wa wanafunzi wanaoshindwa kufanya vizuri shuleni ikiwamo kuwapeleka katika vyuo vya ufundi (Veta).

Alisema shule binafsi zinapaswa kupongezwa kwa kudahili hata wanafunzi hasa wa sekondari ambao shule za serikali huwa haziwachukui kutokana na kushindwa kufanya vizuri katika mitihani ya shule za msingi.

“Hakuna shule ambazo zinapaswa kupongezwa kama za binafsi, serikali yenyewe imekuwa ikichagua wanafunzi wote. Inatuachia ‘vilaza’, lakini sisi kwa kujitoa kuwasaidia watoto wa Kitanzania, tunakubali kuwachukua hao hao wanaoonekana wabaya, tunawafundisha na mwisho wa siku wanakuwa wazuri kuliko hata hao wanaokuwa wamethaminiwa na serikali,” alisema Nkonya.

“Na sisi hatuchuji wala kumfukuza mwanafunzi, isipokuwa kinachofanyika kwa kuwa tunapokea wakati mwingine wanafunzi ambao ni ‘vilaza’ kabisa, huwa tunawagawanya katika makundi kulingana na uelewa wao, wenye uelewa wa kwanza, wa kati na wa mwisho. Na mwisho na tunawafundisha kulingana na ‘speed’ (kasi) ya uelewa wao na wanajikuta wanafanya vizuri.

“Lakini kwa sababu sisi tunakuwa na wanafunzi ambao ni wagumu sana, inapoonekana wakatokea wachache hawawezi kabisa huwa tunashauriana na wazazi wao, kuwapeleka Veta ili kule wanapokuwa wanaendelea kujifunza, wengine wanafanya vizuri hadi wanafika vyuo vikuu, hatuwaachi kama ilivyo katika shule za serikali na vyuo vya serikali, haya maneno mengine yanayozungumzwa ni ya kisiasa tu."

HALI ILIVYO

Uchunguzi wa Nipashe uliofanyika hivi karibuni katika baadhi ya mikoa, ulibaini baadhi ya wamiliki wa shule binafsi wamekuwa na utaratibu wa kuchuja wanafunzi kila mwaka kwa lengo la kupata wenye uwezo mkubwa darasani.

Ilibainika kuwa utaratibu huo umekuwa ukifanywa kwa nia ya kuwa na wanafunzi wenye uwezo mkubwa ili shule hizo zifanye vizuri katika mitihani ya taifa, hivyo kuvutia wazazi wengi zaidi kupeleka watoto wao.

Gazeti hili lilibaini kuwa, baadhi ya shule binafsi zimekuwa zikiendesha utaratibu huo kipindi cha mitihani ya mwishoni mwa mwaka kwa kuwafukuza, kuwakaririsha darasa au kuwahamishia shule nyingine wanafunzi wanaoshindwa kufikia kiwango kinachowekwa na shule husika kwenye mitihani ya kufunga mwaka.

Nipashe pia ilibaini baadhi ya shule hizo zimekuwa na utaratibu wa kuwachuja kwa kuwasajili kama watahiniwa binafsi (Private Candidates) kwenye mitihani ya taifa wanafunzi wake wanaoshindwa kiwango kilichowekwa wanapofanya mitihani ya shule husika.

MTOTO WA PROFESA AKACHA KULA

Akizungumzia suala hilo katika mahojiano maalumu na gazeti hili jijini Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Masomo ya Shahada ya Kwanza Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Prof. Allen Mushi, alisema haungi mkono utaratibu wa baadhi ya shule binafsi kuwafukuza wanafunzi wanaoshindwa kufikia kiwango cha alama zilizojiwekea.

Alisema: "Ni makosa kumfukuza shule mwanafunzi aliyekuwa amedahiliwa, anasoma halafu unamsitishia, unamwambia nenda katafute shule nyingine.

"Na ni kweli wana tabia hiyo. “Nina kijana wangu yuko ‘Form One’ (Kidato cha Kwanza) anasoma shule ... (anataja eneo ilipo shule hiyo), yaani anasoma kupindukia. Nilikuwa na wasiwasi hata akija likizo hawezi kula vizuri, anasoma tu."

Alisema kuwa katika shule hiyo ya jijini Dar es Salaam anayosoma mtoto wake, wameambiwa ni lazima awe na wastani wa kuanzia alama 50 katika mitihani ya shule ili aruhusiwe kuingia kidato kinachofuata, vinginevyo wakatafute shule nyingine.

"Katika utaratibu wa elimu, siyo sahihi kufanya hivyo, wewe kama wanafunzi wameshindwa, wewe siyo ndiyo mwalimu, ndiyo kazi yako ya kufanya wanafunzi waelewe," alisema na kufafanua zaidi:

“Sasa ukiwa unafanya hivyo, mwisho wa siku utakuwa unafelisha darasa zima na kujitamba kwamba unafaulisha kwa sababu umefukuza wengi na kubaki na wazuri wachache. Sasa hiyo ni biashara, siyo elimu tena. Wewe kama ni mwalimu, unatakiwa kufundisha wanafunzi wote.

“Kwa hiyo, wanasema shule za ‘private’ (binafsi) zinafaulisha wanafunzi wote, kumbe wengine mliowachuja. Mimi binafsi sikubaliani na hali hiyo kabisa."

Alisema ni muhimu wizara yenye dhamana ya elimu nchini iweke masharti kwamba ukishadahili wanafunzi, wasiondolewe shuleni kwa utaratibu wa viwango vya ufaulu katika mitihani ya shule husika isipokuwa kwa sababu za tabia mbaya na zisizofaa kwa mwanafunzi kwa mujibu wa sheria za nchi.

MAKUNDI YA UELEWA

Msomi huyo alisema wanafunzi wamegawanyika katika madaraja mawili kiuelewa darasani, la kwanza likiwa la wenye uelewa wa haraka (fast learners) na jingine likiwa la wenye uelewa hafifu (‘slow learners).

"Wote hao wanapaswa wazingatiwe katika elimu. Sasa hawa (shule binafsi) wenyewe wanaangalia 'fast learners' tu. Ni vema wote wakachukuliwa katika vigezo sawa, siyo unawachuja wengine halafu unasema unafaulisha wote," alisema Prof. Mushi.

BIASHARA

Aliyekuwa Rais wa Chama cha Walimu (CWT), Gratian Mukoba, akizungumza na Nipashe jana kuhusu changamoto hiyo, alisema si vyema kumfukuza, kumkaririsha darasa au kumhamisha mwanafunzi aliyefanya vibaya katika mitihani ya shule.

"Mtihani wa Kidato cha Pili ni mchujo sahihi tu. Shule binafsi wanakosea. Ufundishaji wa kawaida huwezi kuwa na wanafunzi wanaopata daraja la kwanza na la pili tu," alisema.

"Hao shule binafsi kuna muda wanateleza kidogo, kwa sababu hakuna mwanafunzi asiyefundishika labda kwa sababu wao wanataka suala la biashara. Ni kuonea wanafunzi, bahati mbaya akishaanza shule ya 'private' (binafsi) kidato cha kwanza, hawezi kurudi kwenye mfumo wa serikali, kwa hiyo wanafunzi wanahangaika," alisema zaidi Mukoba.

Tuesday, December 20

Trump aadhinishwa rasmi Rais wa Marekani


Washington, Marekani. Wajumbe wa Jopo la Kuamua Mshindi wa Urais nchini Marekani wamemuidhinisha Donald Trump kuwa mshindi wa uchaguzi wa urais uliofanyika Novemba. Wajumbe hao walikutana katika majimbo yao kupiga kura.
Awali, kulikuwa na juhudi za kutaka kumzuia bilionea huyo kuingia ikulu kwa madai amekuwa akiendesha siasa za kibaguzi.
Hata hivyo, Trump amesema atakuwa rais wa Marekani wote na atafanya kila liwezekanalo kuwaunganisha wananchi.
Wajumbe walikuwa wametumiwa ujumbe kupitia baruapepe na pia kupigiwa simu wakihimizwa kutomuunga mkono bilionea huyo kabla yao kukutana kupiga kura.
Shughuli yao ya kupiga kura kwa kawaida huwa kama shughuli ya kutimiza wajibu kwani mara zote  huwa wanamuidhinisha mshindi.
Kumekuwa na lawama kuwa uchaguzi wa mwaka huu ulitawaliwa na hila ikiwamo vitendo vya udukuzi kutoka Urusi. Madai hayo yamepuuzwa na Urusi iliyosema hayana msingi wowote.
Jimbo la Texas hatimaye lilimuwezesha kufikisha idadi ya kura 270 za wajumbe alizohitaji,, licha ya wajumbe wawili wake kugeuka na kupiga kura kumpinga.
Matokeo ya kura hiyo yatatangazwa rasmi 6 Januari 6 kwenye kikao maalum cha pamoja cha Bunge la Congress.
"Nawashukuru Wamarekani kwa kunipigia kura kwa wingi kuwa rais wa Marekani," alisema Trump kupitia taarifa baada ya matokeo kutangazwa.
"Kwa hatua hii ya kihistoria tunaweza sasa kutazama mbele na kutarajia maisha ya kufana siku za usoni. Nitafanya kazi kwa bidii kuunganisha nchi yetu na kuwa rais wa Wamarekani wote," alisema.

Baba wa msaidizi wa Mbowe kukagua maiti iliyowekwa kwenye kiroba


Moshi. Wakati polisi wakisema kuwa wanaufanyia mchakato wa vipimo vya vinasaba (DNA), mwili wa mtu anayedaiwa kuuawa nje kidogo ya mji wa Moshi na kuwekwa kwenye kiroba na kuchomwa moto, familia ya Ben Saanane, msaidizi wa Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe ambaye hajulikani aliko imesema inaenda kuuangalia mwili huyo.
Hatua hiyo ya polisi kupima DNA ilielezwa na Kamanda wa Polisi Mkoa Kilimanjaro, Wilbroad Mutafungwa baada ya hadi jana, mwili huo kutotambuliwa.
Mauaji hayo yaligunduliwa Ijumaa iliyopita, baada ya watu waliokuwa na gari ndogo ambao hawajafahamika, kumchoma moto mtu huyo katika Kijiji cha Ongoma na kisha kutoweka kusikojulikana.
Kamanda Mutafungwa aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa mtu huyo hajafahamika na wala hakuna mtu aliyejitokeza kuutambua mwili huo hivyo kulilazimu jeshi kufanya uchunguzi huo wa kisayansi.

Wahifadhi wamwambia Majaliwa, hakuna kaburi la Faru John


Arusha. Sakata na kifo cha Faru John (38), limechukua sura mpya baada ya wahifadhi wa eneo la Sasakwa Singita Grumet kueleza kuwa hakuna kaburi lake kwa kuwa hakuzikwa.
Wamesema hayo siku moja baada ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kutangaza kuunda timu mpya kuchunguza mazingira ya kifo cha faru huyo huku akihoji mambo manne yaliyozua utata.
Mambo aliyohoji wakati akifanya majumuisho ya ziara yake mkoani Arusha ni juzi, Faru John aliumwa lini, aliumwa nini, daktari gani aliyemtibu na zilipo taarifa za matibabu yake.
Pia aliagiza mwili wa faru huyo kufukuliwa na kutazama kama vinasaba vyake vinaendana na watoto wake 26 ambao bado wapo katika Creta ya Ngorongoro.
Akizungumza na mwandishi wetu jana, mmoja wawahifadhi wa Sasakwa Grumet aliyeomba kutotajwa jina ili kutoathiri uchunguzi wa tukio hilo, alisema kitaalamu wanyama ambao wanakufa bila kuwa na magonjwa ya mlipuko katika maeneo ya hifadhi hawazikwi.
“Faru John baada ya kufa aliondolewa pembe zake na kutupwa ili kiwe chakula cha wanyama wengine wanaotegemea mizoga, lakini kuna mifupa yake,” alisema.
Alisema faru huyo aliombwa na Grumet kwenda kupanda faru waliopo katika eneo hilo, hasa baada ya dume aliyekuwapo huko kuuliwa na tembo.
“Baada ya kuonekana kuna haja ya kutafuta dume, ndipo tuliomba kupata faru dume na tukaletewa na baadaye alikufa,” alisema.
Eneo hilo la Sasakwa Singita Grumet ni mali ya mfanyabiashara mkubwa raia ya Marekani, bilionea Tudor Jones ambaye amewekeza katika maeneo kadhaa ya uhifadhi.
Akifafanua hatua zinazochukuliwa baada ya mnyama kufa katika hifadhi, mhifadhi Peter Isango alisema kwa kawaida huzikwa au kuchomwa moto pale tu wanapobainika kuwa na magonjwa kama kimeta.
“Kama mnyama ana magonjwa ambayo yanaweza kuambukiza, basi anachomwa moto au kufukiwa lakini kama anakufa kawaida na magonjwa ya kawaida huwa anatupwa ili fisi, bweha na wanyama wengine wanaokula mizoga wale na hii ndiyo ikolojia,” alisema.
Kauli hiyo iliungwa mkono na mkurugenzi mkazi wa shirika la uhifadhi la kimataifa la Frankfurt Zoological Society, Gerald Bigurube ambaye alisema kwa kawaida wanyama wanaokufa hifadhini huwa hawazikwi.
Bigurube ambaye aliwahi kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Hifadhi za Taifa (Tanapa) alisema kwenye kanuni za uhifadhi kitu chochote, kinachokufa ndani ya hifadhi huachwa kwa ajili ya kulinda ikolojia na bionuwai.
“Mnyama ambaye anakufa kwa kifo cha kawaida mzoga wake unapaswa kuachwa kuoza na kutumiwa na wanyama wengine,” alisema.
Alisema hata wanyama wa kawaida kama swala na wengine wanapoumwa huwa hawatibiwi tofauti na wanyama kama tembo, faru na wengine wakubwa ambao hutibiwa.
Hata hivyo, alipoulizwa kuhusu Faru John, Bigurube alisema taasisi yake haikuwahi kushiriki katika suala hilo.
Wapata dhamana
Katika hatua nyingine, Polisi imewaachia kwa dhamana maofisa watano wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) na Tanapa waliokuwa wanashikiliwa kwa tuhuma za kumhamisha Faru John kutoka Creta ya Ngorongoro na kumpeleka Sasakwa Grumet.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Charles Mkumbo alisema jana kuwa licha ya dhamana hiyo, uchunguzi unaendelea.
Watuhumiwa hao ni Israel Naman ambaye alikuwa kaimu mkuu wa idara ya hifadhi wakati faru huyo akiondolewa, Cuthbert Lemanya aliyekuwa mkuu kanda ya Creta, Dk Athanas Nyaki ambaye ni daktari wa mifugo wa mamlaka hiyo.
Wengine ni aliyekuwa kaimu mkuu idara ya maendeleo ya jamii, Kuya Sayaleli na kaimu mkuu idara ya ikolojia, Patrice Mattey.
Kabla ya kukamatwa, maofisa hawa walikiri kushiriki kumhamisha Faru John kutoka Creta ya Ngorongoro hadi Sasakwa kwa maelezo kuwa ilikuwa ni kuendeleza uhifadhi wa faru na pia kutokana na ukorofi wa Faru John kuhodhi majike yote ndani ya Creta kuua madume wengine waliozaliwa.
Akiwa katika ziara ya kikazi mkoani Arusha, Waziri Mkuu alitoa taarifa za kifo cha faru John huku akiwatuhumu baadhi ya watendaji wa NCAA kuhusika na njama za kumuuza kwa Sh200 milioni ambazo alisema walishapokea malipo ya awali ya Sh100 milioni.
Baada ya maelezo hayo, Waziri Mkuu alitaka kupewa taarifa kamili za tukio hilo, pamoja na pembe za faru huyo, ambazo alikabidhiwa Desemba 8 na Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe na kaimu mkurugenzi wa msaidizi kitengo cha kupambana na ujangili, Robert Mande ambaye alimweleza kuwa taratibu zilifuatwa katika kumhamisha.

Aliyebadili dini afariki baada ya kubatizwa


Moshi. Mkazi wa Mailisita wilayani Hai, Paulo (35) amekufa maji baada ya kuzama katika mto Kikafu, dakika chache baada ya kubadili dini na kubatizwa na maji ya mto huo kwa imani ya dini ya Kikristo.
Paulo ambaye jina lake la awali lilikuwa Issa Juma kabla hajabadili dini, alifariki Jumapili iliyopita katika mto huo, wakati shamrashamra za kubatizwa kwake zikiendelea pembeni ya mto.
Hata hivyo, Jeshi la Polisi lililazimika kuwakamata wachungaji wawili wa kanisa la Efatha waliombatiza lakini waliachiliwa baada ya Polisi kujiridhisha kuwa Paulo alikufa maji baada ya kubatizwa.
Habari zilizothibitishwa na Polisi, zimeeleza baada ya kubatizwa saa 8:30 mchana na wakati waumini wakiimba kwa ajili ya kurudi kanisani, ndipo Paulo na mwenzake waliamua kurudi kuogelea.

Thursday, December 8

Kardinali Pengo akerwa na matanuzi


Pwani. Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo amewataka waumini wa madhehebu hayo kutotumia muda na mali zao kufanya sherehe kubwa, badala yake wajikite katika ujenzi wa makanisa.
Alitoa rai hiyo juzi alipokuwa mgeni rasmi kwenye harambee ya kuchangia Sh50 milioni kwa ajili ya ujenzi wa Kanisa Katoliki Tumbi, Kibaha mkoani hapa.
Kanisa hilo litakuwa na uwezo wa kuhudumia waumini 1,232 kwa wakati mmoja.
Kardinali Pengo alisema ili wanadamu waishi kwa furaha, upendo na amani wanapaswa kupewa ujumbe wa neno la Mungu wakiwa kwenye mazingira bora, hivyo ni vyema jitihada za dhati zikafanyika kujenga makanisa zaidi.
“Nakushukuru Padri Beno (Kikudo) wa kanisa hili ambaye uliona ni vyema utumie siku ya maadhimisho ya miaka yako 50 ya kuzaliwa kufanya harambee hii kukusanya fedha za kukamilisha ujenzi wa kanisa, kuliko wengine ambao wamekuwa wakitumia sherehe hizo maeneo ya fukwe za bahari,” alisema. Alisema makusudi ya Mungu siyo kufuja mali ambazo anawajalia wanadamu, bali kutumia mapato yao kwenye mambo ya maendeleo.
Padri Kikudo aliwashukuru waumini kwa kuonyesha juhudi na moyo wa michango ya hali na mali tangu ujenzi wa kanisa hilo ulipoanza.
Alisema ujenzi wa kanisa hilo umefanyika kwa njia tofauti, ikiwa ni pamoja na waumini kuuza kuku na kujitolea kwa nguvukazi kulingana na vipawa na ujuzi walionao ili kufanikisha ujenzi huo.

Serikali yaombwa kuisadia Dangote

Mtwara. Serikali imetakiwa kukaa na mmiliki wa Kiwanda cha Saruji cha Dangote, Aliko Dangote kutafuta ufumbuzi wa changamoto zinazokikabili kiwanda hicho kwa kuwa anaweza kuwa balozi wa wawekezaji nchini.
Katibu wa CCM Mkoa wa Mtwara, Shaibu Akwilombe  ametoa ombi hilo jana akisema Dangote ana jina kubwa, iwapo kungekuwa na mazingira mazuri ya uwekezaji angesaidia kuwavutia wengine.
 “Siku za hivi karibuni kumekuwa na taarifa kadhaa katika vyombo mbalimbali vya habari zinazohusiana na kiwanda cha Dangote, kutozalisha kwa kile kinachoelezwa ni kutokana na hitilafu za ufundi.  Kwa kuwa tatizo la ufundi limejitokeza kipindi ambacho tayari kulikuwa na malalamiko kutoka kwa wamiliki juu ya gharama za uzalishaji, inasababisha kuwapo mkanganyiko kujua kiini cha tatizo,” amesema Akwilombe.