Thursday, December 8

Kardinali Pengo akerwa na matanuzi


Pwani. Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo amewataka waumini wa madhehebu hayo kutotumia muda na mali zao kufanya sherehe kubwa, badala yake wajikite katika ujenzi wa makanisa.
Alitoa rai hiyo juzi alipokuwa mgeni rasmi kwenye harambee ya kuchangia Sh50 milioni kwa ajili ya ujenzi wa Kanisa Katoliki Tumbi, Kibaha mkoani hapa.
Kanisa hilo litakuwa na uwezo wa kuhudumia waumini 1,232 kwa wakati mmoja.
Kardinali Pengo alisema ili wanadamu waishi kwa furaha, upendo na amani wanapaswa kupewa ujumbe wa neno la Mungu wakiwa kwenye mazingira bora, hivyo ni vyema jitihada za dhati zikafanyika kujenga makanisa zaidi.
“Nakushukuru Padri Beno (Kikudo) wa kanisa hili ambaye uliona ni vyema utumie siku ya maadhimisho ya miaka yako 50 ya kuzaliwa kufanya harambee hii kukusanya fedha za kukamilisha ujenzi wa kanisa, kuliko wengine ambao wamekuwa wakitumia sherehe hizo maeneo ya fukwe za bahari,” alisema. Alisema makusudi ya Mungu siyo kufuja mali ambazo anawajalia wanadamu, bali kutumia mapato yao kwenye mambo ya maendeleo.
Padri Kikudo aliwashukuru waumini kwa kuonyesha juhudi na moyo wa michango ya hali na mali tangu ujenzi wa kanisa hilo ulipoanza.
Alisema ujenzi wa kanisa hilo umefanyika kwa njia tofauti, ikiwa ni pamoja na waumini kuuza kuku na kujitolea kwa nguvukazi kulingana na vipawa na ujuzi walionao ili kufanikisha ujenzi huo.

No comments:

Post a Comment