Tuesday, May 19

UZALISHAJI WA VAZI KINGA (PPE) MUHIMBILI WAONGEZEKA KWA 400% HUKU MAMLAKA YA DAWA NA VIFAA TIBA (TMDA) IKIRIDHIA NA KULITAMBUA


Mafundi wa kitengo cha Ushonaji MNH wakiendelea na ushonaji wa vazi la PPE 
Vazi la PPE likiwa tayari kupelekwa kwa wateja .
Mafundi wa Kitengo cha Ushonaji MNH wakiwa katika maandalizi ya awali ya ushonaji wa vazi la PPE
Muonekano wa vazi la PPE linaloshonwa na Hospitali ya Taifa Muhimbili.
*******************************
  Dar es Salaam, Jumanne Mei 19, 2020.
  Uzalishaji wa vazi kinga linalovaliwa na watoa huduma ili kuhudumia wagonjwa walioambukizwa Covid 19 umeongezeka kutoka mavazi 120 hadi kufikia 600 kwa siku sawa na ongezeko la 400% katika kipindi cha mwezi mmoja tangu lilipozinduliwa na Hospitali ya Taifa Muhimbili Aprili 17, 2020.
 
 Mpaka sasa Hospitali imezalisha PPE 10,553 kati ya hizo 5,000 zimesambazwa MSD na nyingine katika baadhi ya Hospitali za Rufaa za Kanda, Hospitali za Rufaa za Mikoa, Vituo vya Afya, Taasisi zisizo za kiserikali, Hospitali binafsi, makampuni, Halmashauri za Wilaya na Manispaa nchini. Tunaendelea kupokea mahitaji mbalimbali kwani sasa uwezo wa kuzalisha tunao. Bei ya PPE moja ni TZS. 50,000.
 
 Katika hatua nyingine, Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) ilitambua vazi hili kupitia barua yenye Kumb. Na. BC.248/383/01/13 ya tarehe 23 Aprili, 2020 hivyo kuiruhusu Hospitali kuendelea kushona na kufanya usambazaji kote nchini.
 
 “Tunapenda kukufahamisha kuwa Mamlaka imepitia na kuridhia ombi lako la utambuzi wa nguo za kujikinga na maambukizi (coverall, shoe cover na apron) zinazotengenezwa na Muhimbili Tailoring Unit kwa kutumia malighafi ya nylon” inaeleza sehemu ya barua hiyo.
 
 Kwa hiyo utengenezaji na usambazaji wa vifaa hivi unazingatia matumizi na uhifadhi unaofuata kanuni za udhibiti wa vifaa tiba nchini, The Tanzania Food, Drugs and Cosmetics (Control of Medical Devices) Regulation, 2015 kama ambavyo tulivyoelekezwa na TMDA.  Pia vazi hili linafanyiwa utasishaji kabla ya kwenda kwa mtumiaji.

No comments:

Post a Comment