Sunday, December 3

Dk Shein: CCM ina uwezo mkubwa


Rais wa Zanzibar Dk Ali Mohamed Shein amesema Chama cha Mapinduzi (CCM) kina uzoefu wa kufanya mageuzi ya kifikra, itikadi, sera na mabadiliko ya kimaendeleo kwa kufuata misingi imara iliyoachwa na waasisi wa Taifa hili.
Dk Shein alisema hayo jana katika Mkutano Mkuu wa CCM Mkoa wa Kusini Unguja uliokwenda sambamba na uchaguzi wa viongozi chama kimkoa.
Alisema CCM si chama cha mtu mmoja kama vilivyo vyama vingine vya siasa vinavyoendelea kupoteza mwelekeo na kusambaratika kwa kukosa uzoefu wa kihistoria.
Dk Shein ambaye mkoa huo ndiyo wake kichama alisema ni vyema kwa wajumbe wa mkutano huo kuhakikisha viongozi watakaowachagua wanaielewa itikadi ya chama hicho na sera zake na wapo tayari kuzilinda, kuzisimamia na kuzitekeleza kwa vitendo.
Aliwataka viongozi watakaochaguliwa wawe makini, kama ilivyo kawaida kwa viongozi wa CCM.
“Chama chetu kinapendwa, kinawavutia wananchi na kina uwezo mkubwa na wa kipekee wa kurejesha na kujenga matumaini mapya kwa wanachama wake na wananchi wote hivyo hapana shaka tuna nafasi nzuri ya kuendelea kushika dola kwa pande zote mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” alisisitiza Dk Shein.
Pia, alisema ushindi wa kishindo ambao CCM imeupata katika uchaguzi mdogo wa madiwani uliofanyika Novemba 26 kwenye kata 43 nchini ni ishara kwamba ilipitisha viongozi wenye sifa, uwezo, nia njema na waliokubalika kwa wananchi kugombea nafasi hizo.
Alisema ushindi mkubwa uliopatikana katika maeneo ambayo wapinzani walidhani ni ngome yao ni uthibitisho kuwa wananchi wanaendelea kuiamini CCM.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ambaye pia ni mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, alisema wajumbe wanapaswa kuchagua viongozi wa kukiimarisha chama hicho ili kiendelee kupata ushindi katika chaguzi zijazo.

No comments:

Post a Comment