Sunday, December 3

Bibi aeleza sababu za kumfanyia ‘unyama’ mjukuu wake Moshi


Bibi wa mwanafunzi wa darasa la tano anayesoma Shule ya Msingi Kilimanjaro wilayani Moshi, Costansia Lyimo amesema si mara ya kwanza kuwaadhibu wajukuu zake.
Bibi huyo aliagiza mjukuu wake kufungwa kwenye mti na kupigwa jambo ambalo lilisababisha maumivu makali kwa mwanafunzi huyo (jina tunalihifadhi kimaadili).
Akizungumza na Mwananchi jana baada ya juzi picha kusambaa zikionyesha mwanafunzi huyo akiwa amefungwa kwenye mti, Costantina alisema amekuwa akiwaadhibu wajukuu zake kwa namna hiyo ya kufungwa kamba na kutwishwa tofali kichwani huku akiwa amefungwa miguu na kunyanyua mikono juu ili liwe fundisho.
Alisema adhabu ambayo mwanafunzi huyo alipewa juzi ni kutokana na ukorofi wake kiasi ambacho wameshindwa kuvumilia na kwamba mara kwa mara akienda kuogolea huwa anakaa kuanzia asubuhi mpaka jioni.
“Yaani huyu mtoto anaweza kuondoka nyumbani asubuhi hadi jioni ndio anaonekana, kwa kweli baada ya kaka yake kufunga shule na kurudi nyumbani nilimwomba anisaidie kumwadhibu maana ameshindikana,” alisema bibi huyo
Hata hivyo, mama mzazi wa mwanafunzi huyo, Grace Mushi aliyekamatwa juzi jioni na kufikishwa katika kituo kidogo cha Polisi Majengo alisema mtoto huyo amekuwa akimsumbua kila mara kutokana na ukorofi wake.
Alisema mwanaye huyo amekuwa akimsababishia matatizo mengi (hakuyataja) kutokana na tabia chafu aliyonayo.
“Huyu mtoto anaweza kwenda Mto Karanga na kukaa huko kuanzia asubuhi hadi jioni hata shule haendi, kwa kweli huyu mtoto ananiumiza kichwa,” alisema mama huyo.
Mwanafunzi huyo, alikiri kuwa huwa anapigwa na bibi yake huyo kila mara na kudai kuwa juzi ilikuwa si mara ya kwanza kupigwa ila kipigo kilizidi siku nyingine.
“Napigwa kila mara, lakini jana (juzi) nimepigwa zaidi, siku nyingine napigwa tu kawaida,” alisema mtoto huyo.
Jirani aliyeshuhudia tukio hilo, Emmanuel Shirima alisema mtoto huyo alifungwa zaidi ya saa tano huku akiadhibiwa vibaya.
Alisema kitendo ambacho mtoto huyo anafanyiwa kila mara si kizuri hata kidogo katika jamii maana ni unyama.
Aliongeza kuwa hata kama ni adhabu asingestahili kupewa kipigo hicho kutokana na umri wake kuwa bado mdogo.
“Kitendo cha kupigwa kwa mtoto huyo tulishindwa kuvumilia ilibidi twende kutoa taarifa katika kituo kidogo cha Polisi Longuo KCMC, ndipo baada ya muda kidogo askari kutoka kituo cha polisi Majengo walikuja kumchukua mtoto huyo pamoja na mama yake,” alisema shuhuda huyo.
Hata hivyo baada ya askari kumchukua mama wa mwanafunzi huyo kumpeleka kituo cha polisi alikaa muda kidogo na kuachiwa.

No comments:

Post a Comment