Sunday, December 3

Wahitimu Veta kupata fursa mradi bomba la mafuta Tanga


Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Ujerumani (GIZ) linafanya utafiti wa kujua namna ya kuwatumia wanafunzi wanaohitimu katika Chuo cha Mafunzo ya Ufundi Stadi (Veta) mkoani Tanga katika mashirika yatakayowekeza kwenye miradi mbalimbali ikiwamo bomba la mafuta, imeelezwa.
Kaimu mkuu wa Veta mkoa wa Tanga, Amenya Ntibai alitoa taarifa hiyo jana katika mahafali ya 22 ya wahitimu 246 wa fani mbalimbali katika chuo hicho yaliyofanyika jijini hapa.
Alisema kupitia utafiti huo, Veta inaamini kuwa wanafunzi wanaosoma na kuhitimu chuoni hapo watapata ajira na kuongeza ujuzi zaidi kupitia miradi hiyo ya uwekezaji.
Ntibai alisema wanafunzi wanaopita chuoni hapo wanatoka wakiwa wameiva kiufundi na wanaweza kumudu ushindani wa soko la ajira la nchi za Afrika Mashariki, hivyo hakutakuwa na haja ya wawekezaji kuleta mafundi wa fani mbalimbali kutoka nje ya nchi.
“Mbali ya kuwapika ili wajiajiri, lakini Veta tunawaandaa vijana kumudu ushindani wa soko la ajira la nchi za Afrika Mashariki na tunaamini wanatoka hapa wakiwa na ujuzi mkubwa,” alisema Ntibai.
Kaimu mkuu wa wilaya ya Tanga, Selemani Zumo aliutaka uongozi wa Veta kuweka kumbukumbu sahihi za wanafunzi waliofanya vizuri kwenye mafunzo kwa vitendo katika kila fani ikiwamo kujua wapi waliko ili itakapopatikana fursa iwe rahisi kuwatafuta.
“Moja ya sifa za fundi kuchukuliwa na mradi wowote wa uwekezaji naamini itakuwa ni cheti cha Veta. Hivyo ni vyema kuwa na kumbukumbu za wanafunzi waliofanya vizuri na kujua wapi waliko, Serikali itahakikisha wanapewa kipaumbele,” alisema Zumo.
Mwanafunzi aliyehitimu mafunzo ya ufundi umeme wa magari katika chuo hicho, Yusuph Idd alisema katika miaka miwili aliyosoma amepata ujuzi utakaomuwezesha kujiajiri na kuajiri vijana wengine.
Veta mkoa wa Tanga ilianzishwa mwaka 1977 na hadi mwaka huu imeshatoa mafunzo kwa vijana 13,987.

No comments:

Post a Comment