Sunday, December 3

Dk Mahanga aeleza kushawishiwa kurejea CCM


Naibu Waziri wa Kazi na Ajira, katika Serikali ya Awamu ya Nne, Dk Makongoro Mahanga ambaye ni mwanachama wa Chadema amedai kuwashawishiwa kurejea Chama cha Mapinduzi (CCM).
Dk Mahanga alihama CCM Agosti 2,2015 baada ya kushindwa katika kura ya maoni kwa nafasi ya ubunge jimbo la Segerea.
Mbunge huyo wa zamani wa Segerea alijitoa CCM akisema ni kwa sababu utaratibu uliotumika haukuwa sahihi na uligubikwa na vitendo vya rushwa na njama zilizofanywa na viongozi wa kitaifa wa chama hicho tawala.
Akizungumza na MCL Digital leo Jumapili Desemba 3,2017 Dk Makongoro amesema mara kwa mara amekuwa akifuatwa na watu tofauti wakiwamo ndugu zake wakimshawishi arejee kwenye chama hicho tawala.
Amesema, “Nawaambia hivi sirudi huko. Huwa nina ishi kwa ninachokiamini  na hakuna kinachoweza kunishawishi kubadili imani na dhamira yangu ya Agosti 2 mwaka 2015.”
Awali, kupitia akaunti ya mtandao wa kijamii wa Facebook Dk Mahanga aliwataka wahusika kuacha kuwatuma rafiki zake na ndugu zake ili kumshawishi kurejea CCM.
“Imani yangu, utu wangu na msimamo wangu huwa hauna bei. Kamwe sitorudi CCM acheni kuhangaika,” amesema Dk Mahanga katika ukurasa huo.

No comments:

Post a Comment