Tuesday, October 24

FastJet yasababisha abiria kufanya vurugu Mwanza


Mwanza. Askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia(FFU) leo wamelazimika kuingilia kati kutuliza vurugu zilizoazishwa na abiria 75 waliokosa usafiri wa ndege ya kampuni ya FastJet kutoka Mwanza kwenda Dar es Salaam kutokana na hitilafu za kiufundi.
Abiria hao waliokaa uwanjani hapo kwa zaidi ya saa nne kuanzia saa 3:00 asubuhi walipotakiwa kusafiri hadi saa 7:00 mchana, walianzisha vurugu kushinikiza kupatiwa usafiri.
Wakizungumza na Mwananchi uwanjani hapo kwa nyakati tofauti, abiria Rukia Mohamed, Juma Kisombi na Mamad Mohamed wamesema walilazimika kuushinikiza uongozi wa kampuni hiyo kuwapa maelezo ya kutosha baada ya ahadi ya kutakiwa kusubiri kidogo kutotekelezwa kwa zaidi ya saa tatu waliyosubiri uwanjani hapo.
“Nimefika Jumapili iliyopita na leo, nilitakiwa kurejea jijini Dar es Salaam na nilifika uwanjani kwa muda uliotakiwa lakini hadi sasa hakuna ndege na uongozi hautoi maelezo ya kueleweka,” alilalamika Rukia.
Akizungumzia kadhia hiyo, Meneja wa FastJet Mkoa wa Mwanza, Ezekiel Manyiga amesema ndege iliyotakiwa kusafirisha abiria hao haikufika kutoka jijini Dar es Salaam kutokana na kupata hitilafu ya kiufundi.
“Hata abiria waliotakiwa kusafiri kutoka Dar es Salaam kuja Mwanza hawajafika hadi sasa; tunafanya kila lililo ndani ya uwezo wetu kutatua tatizo hili,” amesema Manyiga
Ilipofika saa 7:00 mchana jana, uongozi wa kampuni hiyo ulifikia uamuzi wa kuwarejeshea nauli abiria waliokuwa tayari kupokea fedha zao ili kutafuta usafiri mwingine pamoja na Sh30, 000 ya kujikimu kwa kila abiria aliyekosa usafiri.
“Watakaokuwa tayari kusubiri ndege yetu watalazimika kusafiri kesho (Jumatano)  kwa sababu ndege tayari imejaa,” amesema Manyiga

No comments:

Post a Comment