Sunday, September 10

Polisi Tanzania kuwasaka waliotaka kumuua Tundu Lissu

Mkuu wa Jeshi la Tanzania
Image captionMkuu wa Jeshi la Tanzania
Mkuu wa Jeshi la Polisi Simon Sirro amesema kuwa wametuma kikosi cha ziada polisi wa upelelezi mjini Dodoma kuchunguza na kuwatafuta wahalifu.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es salaam, Mkuu wa Jeshi la Polisi Simon Sirro amesema kuwa wametuma kikosi cha ziada polisi wa upelelezi mjini Dodoma kuchunguza na kuwatafuta wahalifu waliotekeleza shambulio la mwanasheria wa chama cha upinzani CHADEMA Tundu Lissu siku ya Alhamisi.
Kamanda Sirro amekanusha tetesi ya kuwa waliomshambulia mbunge huyo walikuwa wanahusika na polisi.
"Suala la sare za washukiwa kufanana na za jeshi la polisi" Kamanda Sirro amenukuliwa akisema "kinachofanya uhalifu sio sare, Kinachofanya uhalifu ni mtu anayetekeleza tukio. Nguo za jeshi la polisi Tanzania zinafanana na nguo nyingi za makampuni binafsi lakini siyo hoja kwamba polisi wetu wanahusika. Kwa hiyo jambo la msingi tunawatafuta waliotekeleza tukio hilo."
Hivi karibuni, mbunge Tundu Lissu kutoka chama cha upinzani cha CHADEMA, amekuwa akikamatwa mara kwa mara na jeshi la polisi akishutumiwa kufanya uchochezi.
Kamanda Sirro amelizungumzia suala hilo "Tunamkamata kamata Tundu Lissu kutokana na matendo yake na kutokana na sheria yenyewe."
Ikumbukwe kwamba Tundu Lissu alipigwa risasi na watu wasiojulikana Mjini Dodoma, katikati mwa Tanzania siku ya Alhamisi, na baadaye kupatiwa matibabu katika hospitali kuu ya Mkoa wa Dodoma na kisha kusafirishwa hadi mjini Nairobi, katika hospitali ya Nairobi kwa matibabu zaidi.

No comments:

Post a Comment