Monday, August 14

Makamba: Serikali haina nia ya kurudisha viroba


Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), January Makamba amesema Serikali haina nia ya kurudisha sokoni pombe zilizotengenezwa katika mifuko ya plastiki 'viroba'na kuwataka Watanzania kupuuza uzushi unaoenezwa kwamba pombe hizo zitarudi.
Makamba alitoa kauli hiyo leo, Jumatatu Agosti 14 alipotembelea eneo la Kimara Temboni lilipo ghala la kuhifadhi pombe mbalimbali ikiwamo viroba linalomilikiwa na Kampuni Thema.
Makamba alisisitiza kwamba Serikali uamuzi wake wa kuzuia pombe hizo upo palepale na haujabadilika hivyo watu waache kupotosha wenzao.
"Baada ya kupiga marufuku kuna kampuni zilikuja ofisi kuomba kuongezewa muda, lakini tuliwakatalia na kuwaambia waheshimu uamuzi uliotolewa sasa hizi tetesi ya kwamba vinarudi sokoni sijui zinatoka wapi," alisema Makamba.
Makamba ambaye pia ni Mbunge wa Bumbuli amesema  njia ya pekee kwa wafanyabiashara hao wa viroba wanaotakiwa kuifanya ili kupunguza hasara ni kubadilisha pombe hizo na kuziweka katika chupa zenye ujazo unaotakiwa.
Amesema kamwe Serikali haiwezi kurudi nyuma na kwamba mafanikio yameanza kuonekana kutokana na hatua hiyo.

No comments:

Post a Comment