Tuesday, March 22

Wawili wafariki Dar kwa dalili za ebola

Dar es Salaam. Watu wawili wamefariki dunia kwa maradhi ambayo dalili zake zinafanana na ugonjwa wa ebola.
Watu hao walifariki baada ya kufikishwa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) wakiwa wanatoka damu sehemu mbalimbali za miili yao ikiwamo kwenye ngozi, mdomoni, puani na matundu mengine ya mwili.
Mgonjwa wa kwanza alifariki dunia Machi 16 saa nane usiku na mwingine jana mchana. Wote walifariki ndani ya saa 12 baada ya kufikishwa hospitalini hapo.
Mkuu wa Kitengo cha Uchunguzi wa Magonjwa MNH, Dk Praxeda Ogweyo alisema wamewapokea wagonjwa hao wawili,  lakini vipimo havijaonyesha kama wana ebola.  “Ni kweli kuwa tumewapokea wagonjwa hao wawili na vipimo vya mgonjwa wa kwanza kinaonyesha hana ebola, lakini bado wanaendelea kufanya uchunguzi wa kina kujua ni ugonjwa gani,” alisema.
Dk Ogweyo alisema majibu ya mgonjwa wa pili aliyefariki jana bado hayajatoka.
Taarifa za awali zilizopatikana kutoka kwa ndugu wa marehemu zinaeleza kuwa wagonjwa hao wote walipita Mafinga, Iringa kabla ya kuja Dar es Salaam.
Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu alisema wizara yake imepokea taarifa hizo: “Tumepeleka sampuli kwenye maabara ya Taifa, majibu yote ni negative (hawana ebola). Hata hivyo, tumeamua kupeleka nje ya nchi kwa ajili ya kujiridhisha zaidi,” alisema.
Waziri Mwalimu alisema sampuli hizo mbili za damu zimepelekwa Taasisi ya Uchunguzi wa Magonjwa Kenya (KIMR).
Hata hivyo, alisema miili yao itazikwa na Serikali kupitia ofisi ya Mganga Mkuu wa Serikali na ndugu wa marehemu watapewa ushauri nasaha.
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Dk Grace Mganga alisema kutokwa na damu kunaweza kuwa na sababu nyingi, ikiwamo homa ya dengue, ebola na upungufu wa chembe ndogo za damu zinazouia damu kutoka kwa wingi.
Shemeji wa mmoja wa marehemu hao, Juma Seromba alisema ndugu yao alianguka akiwa kazini kama mgonjwa wa kifafa, akaanza kutokwa damu sehemu mbalimbali mwilini na baadaye walimpeleka MNH.

No comments:

Post a Comment