Tuesday, March 22

Siri ya madini Tanzanite kutoroshwa yabainika


Dar es Salaam. Udhaifu wa sheria zinazosimamia uchimbaji wa Tanzanite umetajwa kuwa chanzo cha madini hayo kuuzwa kwa wingi na nchi za Kenya, India na Afrika Kusini badala ya Tanzania yanakopatikana.
Hayo yalibainika wiki iliyopita katika ziara ya wahariri wa vyombo vya habari kwenye mgodi wa TanzaniteOne Mine Limited (TML), uliopo Mirerani Simanjiro mkoani Manyara.
Mkuu wa Usalama wa TML, George Kisambe alisema ingawa wameimarisha ulinzi kwa asilimia 90 kwa kushirikiana na Stamico chini ya Serikali, udhaifu kwenye sheria unatoa mwanya kwa hujuma dhidi ya Tanzanite na kampuni yao.
“Usimamizi wa sheria ndiyo unaosababisha Kenya na India zionekane kuongoza katika uuzaji Tanzanite inayochimbwa Tanzania pekee,” alisema Kisambe.
Hali hiyo inatajwa pia kudhoofisha usalama na kuwasukuma wawekezaji kuweka idadi kubwa ya walinzi kwenye migodi yao kudhibiti hali ya usalama kwa kuhofia uvamizi wa maeneo yao ya uchimbaji.
“Ili kurekebisha hali hiyo ni vyema Serikali ije na mkakati mbadala wa usimamizi wa madini haya, ikiwezekana iweke ukuta kama ilivyo kwa Israel na Palestina kuzitenganisha na kutambua maeneo yote ya uchimbaji,” alisema.
Alisema kitakwimu kampuni hiyo inachimba chini ya asilimia 30 ya madini yote ya Tanzanite na mapato yake yanajulikana na Serikali kwa kuwa na udhibiti huku ikilipa kodi.
Kaimu Mkurugenzi wa TML, Modest Apolinary alisema uvamizi wa wachimbaji wadogo katika mgodi huo ni changamoto inayopoteza kiwango kikubwa cha mapato na kuiomba Serikali kumaliza tatizo hilo.
“Serikali ina mamlaka ya kufanya uamuzi dhidi ya wachimbaji wavamizi ili TML iendelee kuchimba eneo lake, iongeze ajira kwa vijana na ichangie zaidi mapato ya Serikali kwa kulipa kodi inayotakiwa,” alisema Apolinary.

No comments:

Post a Comment