Wednesday, August 12

Daktari: Mbowe yuko salama


“Ninachoweza kuwaambia Watanzania, 
niko salama na hali yangu inaendelea vizuri, 
tatizo  nililonalo limetokana na kufanya kazi usiku na mchana bila kupumzika.” 
Freeman Mbowe. 

Dar es Salaam. Siku moja baada ya Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Freeman Mbowe kuugua ghafla akiwa kwenye maandaamano na kuwahishwa hospitali ya Taifa Muhimbili, imebainika kuwa hali hiyo imesababishwa na kufanya kazi kwa muda mrefu bila kupumzika.
Daktari bingwa wa Moyo Kitengo alicholazwa kiongozi huyo, Dk Tulizo Sanga alieleza kuwa baada ya jopo la madaktari wanane kumfanyia uchunguzi waligundua kwamba tatizo kubwa lililokuwa likimsumbua Mbowe ni uchovu ambalo kitaalam linaitwa ‘Fatigue’.
“Jopo la madaktari lilimfanyia vipimo na tumegundua kuwa tatizo kubwa linalomsumbua ni uchovu unaosababishwa na kusafiri na kufanya kazi kwa muda mrefu bila kupumzika.
“Uamuzi uliochukuliwa ni kumuweka mapumziko kwa ajili ya uangalizi zaidi ndani ya saa 48 lakini hali yake inaendelea vizuri anaweza kuruhusiwa muda wowote,” alisema Dk Sanga
Dk Sanga alieleza kuwa Mbowe alipokelewa hospitalini hapo kwenye kitengo cha magonjwa ya dharura akitokea katika hospitalia ya Doctors Plaza iliyopo Kinondoni.
Mwananchi lilishuhudia viongozi kadhaa wa upinzani wakiwasili katika Jengo la Moyo kumjulia hali kiongozi huyo.
Baadhi ya viongozi walioonekana ni Makamu wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad, Juma Duni Haji, Godbless Lema, Joshua Nassari na Mwenyekiti mwenza wa Ukawa, James Mbatia.
Kwa upande wake, Mbowe aliwatoa hofu watanzania na kuwahakikishia kwamba yupo salama na waondokane na hofu ambayo imeonekana kuenea kwenye mitandao na vyombo vya habari.
“Hakuna hali yoyote ya hofu na wasiwasi kama ambavyo imeshaanza kujengeka kwenye mitandao ya kijamii nipo hospitali kwa sababu za kitabibu na si vinginevyo.
“Ninachoweza kuwaambia Watanzania niko salama na hali yangu inaendelea vizuri, tatizo nililonalo limetokana na kufanya kazi usiku na mchana bila kupumzika,” alisema Mbowe.
Akizungumza na wanahabari Mbatia aliwata watanzania kuendelea kumuombea kiongozi huyo na kuwaunga mkono Ukawa ili waendeleze harakati zao katika kipindi hiki cha kuelekea kwenye Uchaguzi Mkuu.
“Suala la kuugua ni kawaida kwa kila binadamu ninachoweza kusema tuondelee kumuombea ili arejee kwenye mapambano na wazidi kutuunga mkono kwenye harakati zetu”alisema Mbatia
Kuhusiana na uwezekano wa ugonjwa wa Mbowe kusitisha ziara za Ukawa mikoani Mbatia alisema ratiba inaendelea kama kawaida na afya ya kiongozi huyo ikitengemaa ataungana na wenzake kwenye harakati hizo.
Mbowe aliugua ghafla juzi akiwa katika maandamano ya kumsindikiza mgombea urais kwa tiketi ya chama hicho, Edward Lowassa baada ya kuchukua fomu za kugombea urais katika Tume ya Taifa Uchaguzi (NEC).

No comments:

Post a Comment