Wednesday, August 12

CCM, Ukawa gumzo


Mikutano ya CCM (kushoto) na Chadema (kulia) 
iliyofanyika nchini hivi karibuni. 

Dar es Salaam. Mazungumzo kuhusu siasa na hasa Uchaguzi Mkuu, idadi ya watu waliojitokeza kujiandikisha kupiga kura na idadi kubwa ya watu wanaojitokeza kwenye mikutano ya hadhara ya wanasiasa ndiyo hali iliyoenea kila kona ya nchi kwa sasa, kitu ambacho wachambuzi waliohojiwa na gazeti hili wamekielezea kuwa ni kuongezeka kwa mwamko wa wananchi katika masuala ya siasa.
Wachambuzi hao, ambao waliohojiwa na Mwananchi kwa nyakati tofauti, wameeleza kuwa mwamko huo pia unatokana wananchi kutaka mabadiliko, uamuzi wa kada wa CCM, Edward Lowassa kuhamia Chadema na umoja wa vyama vya upinzani ambavyo vimeamua kuunganisha nguvu kwenye uchaguzi, kitu ambacho kimewafanya wananchi waone kunaweza kuwa na ushindani wa kweli safari hii.
Tangu mchakato wa uchaguzi uanze ndani ya vyama, mazungumzo ya wananchi wa kawaida kwenye mikusanyiko mbalimbali kama sokoni, maskani, kwenye vyombo vya usafiri na mitandao ya jamii imekuwa ikitawaliwa na siasa na hasa baada ya CCM kuanza kutafuta mgombea wake wa urais.
Ufuatiliaji huo wa habari za siasa uliongezeka zaidi baada ya kumteua Dk John Pombe Magufuli kuwania urais kwa tiketi ya chama hicho tawala na jina la Lowassa kutoingia tano bora, kitu kilichomfanya atangaze kujivua uanachama na kuhamia Chadema.
Wanasiasa hao wawili pia wamevuta maelfu ya watu kwenye mikutano yao ya kutambulishwa kwa wanachama, kutangaza kuhama chama na kuchukua fomu za kuwania urais, huku mbunge wa zamani wa Chadema, Zitto Kabwe akivuta mamia ya watu kwenye mikutano yake ya kukitangaza chama kipya cha ACT Wazalendo.
Idadi ya watu wanaotangaza kuhama chama kimoja na kwenda kingine imekuwa ikiibua mijadala mara kwa mara, huku bendera za vyama vikuu vya kisiasa—CCM, Chadema, CUF na NCCR Mageuzi—zikipepea maeneo mengi.
Wakati mwaka 2010 waliojiandikisha kupiga kura mwaka 2010 walikuwa milioni 11.5, mwaka huu idadi inaweza kuwa maradufu baada ya makisio ya watu waliotarajiwa kujitokeza kujiandikisha kuwa milioni 24 huku Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ikieleza kuwa imefikia idadi iliyotarajiwa au kupita malengo kwenye baadhi ya mikoa.
Pamoja na ukweli kwamba kipindi cha kuelekea Uchaguzi Mkuu uliopangwa kufanyika Oktoba 25 kinatakiwa kitawaliwe na habari na mijadala ya kisiasa, wachambuzi wanazungumzia mwamko wa mwaka huu kuwa ni mkubwa zaidi kulinganisha na chaguzi zilizopita.
Kauli za wasomi
Akizungumza na Mwananchi kuhusu hali hiyo ya siasa kushika nafasi kubwa katika mijadala mbalimbali, Profesa Gaudence Mpangala wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Ruaha (Ruco) alisema wananchi sasa wameamka na kutambua haki yao ya kupigakura, na hivyo wanataka kuitumia kudai mabadiliko waliyoyakosa kwa muda mrefu.
“Kuongezeka kwa umasikini, vijana kukosa ajira, ufisadi na kuongezeka kwa rushwa kumewaamsha wananchi kwa kiasi kikubwa na kuamka kwao kunatokana na kukua wa utandawazi,” alisema Profesa Mpangala.
“Ukiongea na wananchi wengi, wanakwambia kuwa wanataka mabadiliko. Wana matatizo mengi na wanaamini kuwa wakichagua kiongozi mzuri anaweza kuondoa matatizo yanayowakabili.”
Hata hivyo, Profesa Mpangala alisema tatizo lililopo ni wananchi kuamini kuwa mtu mmoja ataweza kuwaletea mabadiliko na kusahau kuwa mabadiliko watayaleta wenyewe, akieleza kuwa ili mabadiliko yatokee ni lazima kubadilisha mfumo wa utawala.
“Wanatakiwa kutazama mfumo maana chama kitakachoingia Ikulu kitaweza kuleta mabadiliko kama mfumo wa utawala utakuwa mzuri. Chama kinaweza kuwa na mgombea mzuri, lakini akashindwa kuleta kipya kwa sababu ya mfumo,” alisema.
Kauli ya Profesa Mpangala juu ya Watanzania kutaka mabadiliko inaungwa mkono na Richard Mbunda ambaye ni mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), ambaye alisema mwamko huo pia unatokana na ugumu wa maisha kwa watu wengi.
“Ninatembea maeneo mbalimbali ya nchi yetu na kuzungumza na watu. Nilichokibaini ni wananchi kuchoshwa na maisha wanayoishi. Wanahoji wazi iweje maisha yao yawe duni na ya wengine yawe ya juu. Watanzania sasa si watu wa kufuata upepo tu kama ilivyokuwa miaka ya nyuma,” alisema Mbunda.
“Wanaona tatizo kubwa tulilonalo ni la kimfumo na wanaamini kuwa wakichagua kiongozi wa aina fulani hali yao ya maisha itabadilika.”
Alisema kitendo cha Ukawa kumsimamisha Lowassa kimeibua changamoto mpya kwa sababu ni mgombea anayekubalika na watu wengi na wengi wanaamini kuwa akiwa rais ataweza kuwavusha.
“Hata Magufuli amefanya mengi ikiwa ni pamoja na kujenga barabara nyingi na wananchi wanamfahamu. Wagombea hawa wanaufanya uchaguzi wa mwaka huu kuwa wa kihistoria,” alisema.
Dk Benson Bana ambaye ni Mhadhiri wa Chuo Kikuu Dar es Salaam (UDSM) naye alimtaja Lowassa kama chachu inayowafanya Watanzania kujitokeza kwa wingi kushiriki uchaguzi.
“Mabadiliko ni hali ya kutoka katika hali uliyokuwa nayo kwenda katika hali nzuri zaidi. Watu hawajaanza kuyataka mabadiliko leo, wamekuwa wakiyataka kila uchaguzi. Wapo wanaomuonea huruma Lowassa na kuona kuwa dhamira yake ya kuhama CCM kwenda Chadema ni ya kweli na kuna jambo anataka kulifanya,” alisema.
Alisema CCM imekaa madarakani kwa muda mrefu na kufikia hatua ya kujisahau, jambo ambalo linawafanya wananchi kutaka mabadiliko.
“Binadamu siku zote hupenda mabadiliko. Hili suala la watoto wa viongozi nao kupewa uongozi, wananchi wanaliona na linawaudhi na wanaona CCM kama uwanja fulani hivi wa kubebana. Hawasemi tu ila wanayaona haya na wanayatafakari,” alisema.
“Mfumo wa CCM kujiendesha unatakiwa kutazamwa upya maana chama kineonekana kama cha (katibu mkuu wa CCM, Abdulrahman) Kinana na (katibu wa itikadi na uenezi wa CCM), Nape (Nnauye),” alisema na kusisitiza kuwa makamu mwenyekiti wa chama hicho, Philip Mangula amebaki kushughulikia masuala ya nidhamu. Hivi utapata kura kwa kushughulikia nidhamu?”
Alisema wanachotakiwa kukifanya Watanzania ni kuzichambua sera za CCM na vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kama zinaweza kutatua matatizo yanayowakabili, si kutazama sifa za mgombea mmoja mmoja.
“Wagombea wote wanakuja na lugha za kuwasaidia machinga, waendesha bodaboda, mamantilie na tatizo la ajira. Hizo ni lugha za kutafuta kura tu. Wanachotakiwa kutueleza wagombea wote ni mkakati watakaoutumia kumaliza matatozo hayo,” alisema.
Hoja za kuwapo mwamko pia zilitolewa na mchambuzi wa masuala ya siasa na utawala na mhadhiri wa Chuo Kikuu Huria (OUT), Hamad Salim.
“Watanzania wanataka mabadiliko na wapo wanaodhani watayapata kupitia CCM na wanaodhani watayapata nje ya CCM kutokana na kuyasubiri ndani ya chama hicho tawala kwa muda mrefu,” alisema Salim.
Alisema kitendo Lowassa kuhamia Ukawa kumeibua mihemko na ushindani mpya wa kisiasa nchini, na kwamba hilo limekuwa moja ya sababu ya wananchi wengi kujiandikisha.
“Ila si wote wanaojiandikisha kupigakura watapiga kura kuchagua viongozi, wapo watakaotumia shahada zao katika masuala yao binafsi,” alisema.
Profesa Damiani Gabagambi wa Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine(Sua) anaouona mwamko huo kwa vijana waliozaliwa mwishoni mwa miaka ya tisini na mwanzoni mwa miaka ya tisini, akisema wengi wanataka mabadiliko lakini hawajui yataletwaje.
“Miaka ya nyuma wananchi walikuwa hawapigi kura wakiamini kuwa nguvu ya upinzani ni ndogo, ila kitendo cha vyama vinne kuungana na kusimamisha mgombea mmoja kimewazindua  na sasa wanauona ushindani wa kweli. Ila wapo waliojiandikisha ili wapate shahada tu kwa matumizi mbalimbali,” alisema.
Katika uchaguzi wa mwaka huu, watu saba wamejitokeza kuwania urais kumrithi Rais Jakaya Kikwete ambaye amemaliza vipindi vyake viwili vya miaka mitano kila kimoja.
Wakati CCM imemsimamisha Dk Magufuli, vyama vinne vinavyounda Ukawa vimekubaliana kumsimamisha Lowassa, hali inayofanya uchaguzi wa mwaka huu uonekane kuwa ni vita vya kihistoria baina ya wawili hao.
Pia mwenyekiti wa DP, Mchungaji Christopher Mtikila amechukua fomu za kugombea urais sambamba na Chifu Lutayosa Yemba (ADC), Macmillan Lyimo (TLP), Hashimu Rungwe (Chauma) na Fahami Dovutwa (UPDP).
Mgombea wa nane anatarajiwa kutoka chama kipya cha ACT Wazalendo.

No comments:

Post a Comment