Wednesday, August 12

CCM yatengua matokeo majimbo ya vigogo

Nape Nnauye, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM 

Dodoma/Dar. Chama cha Mapinduzi (CCM) kimetengua matokeo ya kura za maoni na kuamuru kurudiwa kwa uchaguzi katika majimbo matano, baada ya kubaini kulikuwa na ukiukwaji wa kanuni.
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alisema jana kuwa Kamati ya Maadili iliyoketi juzi hadi usiku, iliamua majimbo ya Kilolo (Iringa), Makete (Njombe),  Rufiji (Pwani), Ukonga (Dar es Salaam) na Jimbo la Busega mkoani Simiyu yarudie uchaguzi.
“Siyo kwamba Kamati Kuu ilikuwa inapitia rufaa pekee bali tulikuwa tunaangalia mambo yote yaliyotokea na kuona namna bora ya kufanya, ndiyo maana tumekubaliana lazima uchaguzi huo urudiwe katika majimbo hayo Alhamisi (kesho) Agosti 13, mwaka huu,” alisema Nape.
Kilichotokea
Ingawa Nape alikataa kutaja kasoro zilizojitokeza katika majimbo hayo akisema hayo ni mambo ya ndani ya chama, kumekuwapo na  malalamiko ya vitendo vya rushwa katika majimbo mbalimbali nchini, hali iliyosababisha Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kuwakamata baadhi ya watuhumiwa.
Kilolo
Katika jimbo la Kilolo, kurudiwa kwa kura za maoni si jambo geni kwani hata mwaka 2010 uchaguzi huo ulirudiwa kati ya Profesa Peter Msolla na Venance Mwamoto aliyekuwa anamaliza kipindi chake wakati huo na Msolla kuibuka mshindi.
Jambo hilo limejirudia mwaka huu baina ya wagombea hao, baada ya Profesa Msolla anayemaliza muda wake kugomea kusaini matokeo ya uchaguzi, akidai kuwapo udanganyifu baada ya kuangushwa na Mwamoto.
Katika uchaguzi huo uliohusisha wagombea 15, Mwamoto alipata kura 11,200 wakati Profesa Msolla akipata kura 10,014. Kama ilivyokuwa katika majimbo mengine, tuhuma za rushwa na uvunjaji taratibu ziliripotiwa wakati wa mchakato huo.
Hata baada ya Profesa Msolla kugomea matokeo, Katibu wa CCM Mkoa wa Iringa, Hassan Mtenga alisisitiza kuwa kitendo hicho hakizuii vikao vya kamati ya CCM ngazi ya mkoa na wilaya kufanyika na kwamba matokeo hayawezi kubadilishwa wala uchaguzi kurudiwa.
Ukonga
Moja ya majimbo yaliyotawaliwa na madai ya rushwa na ukiukwaji wa taratibu lilikuwa Ukonga ambalo Meya wa Manispaa ya Ilala, Jerry Silaa alipata ushindi wa kura 10,000 dhidi ya mpinzani wake Ramesh Patel aliyepata kura 7,356 wakati Robert Masegesi aliambulia 548.
Hata baada ya ushindi huo wa Silaa, kuliibuka utata wa matokeo baada ya wagombea kutuhumiana kuchakachukua. Slaa alipoulizwa jana kuhusu uamuzi huo, alisema yeye si msemaji wa CCM, aulizwe Nape.
Makete
Licha ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira), Dk Binillith Mahenge kutangazwa mshindi wa kura za maoni jimbo la Makete, uliibuka utata juu ya matokeo hayo huku kukiwa na madai ya upande wa mshindani wake, kuwa Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Dk Norman Sigala ndiye mshindi.
Katika uchaguzi huo, Dk Mahenge alipata kura 8,534, Dk Sigala (8,211), Bonic Muhami (500), Fabianus Mkingwa (466) na Lufunyo Rafael aliyepata 226.
Busega
Kura za maoni za Jimbo la Busega nazo ziligubikwa na utata baada ya wagombea wawili, mbunge anayemaliza muda wake, Dk Titus Kamani na Dk Raphael Chegeni kujitangaza kwa nyakati tofauti kuwa washindi kabla ya matokeo rasmi.
Katika matokeo yaliyotangazwa baadaye, Dk Chegeni aliibuka mshindi kwa kupata kura 13,048 dhidi ya 11,829 za Dk Kamani.
Utata huo ulifanya hata kikao cha Kamati ya Siasa cha Wilaya ya Busega kilichokuwa kimehudhuriwa na watia nia sita kati ya saba, kuvunjika mbele ya Mkuu wa Wilaya hiyo, Paul Mzindakaya na Katibu wa CCM mkoa huo, Hilda Kapaya.
Vurugu ziliibuka katika eneo hilo na kusababisha baadhi ya wajumbe kurushiana makonde na karatasi za matokeo kuibwa mbele ya polisi na viongozi wa chama hicho.
Dk Kamani aliiambia gazeti hili hivi karibuni kuwa, amekata rufani kupinga matokeo hayo.
Rufiji
Katika Jimbo la Rufiji hali ilikuwa tofauti baada ya CCM wilayani humo kutoyatambua matokeo yaliyokuwa yametangazwa kuwa mbunge anayemaliza muda wake na Waziri wa Afya, Dk Seif Rashid alikuwa ameangushwa kwa kupata kura zaidi ya 3,000 dhidi ya mpinzani wake Mohammed Mchengelwa aliyepata kura zaidi ya 4,000.
Katibu Mwenezi wa CCM Wilaya hiyo, Musa Mng’eresa alisema kuwa kulikuwa na uvunjwaji wa kanuni ukiwamo ubadhirifu katika uchaguzi huo uliohusisha wagombea wanane, hivyo matokeo ya jimbo la Rufiji na Kibiti yalisitishwa.
Wizi wa kura
Alipotakiwa kujibu tuhuma kwamba CCM ni hodari wa kuiba kura nyakati za uchaguzi, zilitolewa juzi na mgombea urais wa Chadema na Ukawa, Edward Lowassa, Nape alisema, “tuzungumze haya (kurudia uchaguzi) kwanza tuachane na oil chafu, hayo siwezi kuyasemea nimeshawapa story, inatosha.”
Alisema baada ya kikao cha Kamati Kuu jana, leo inaweza kukutana Halmashauri Kuu ya Taifa kuidhinisha majina ya wagombea ili kuwaruhusu kuanza mchakato mwingine.
Kamati Kuu
Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete, akifungua kikao cha Kamati Kuu kilichohudhuriwa na wajumbe 25 badala ya 32, alisema, “Habari za toka tulipoachana, haya tufanye kazi iliyotuleta hapa, leo na kesho watu wanasubiri kwa hamu kubwa nani ni nani ili waweze kuimba iyena iyena, kikao kimefunguliwa waandishi mtupishe.”
Wakati waandishi wakitoka, Rais Kikwete alisikika akisema, “tunaanza kupitia majina na kila mmoja anatakiwa kuwa makini.


No comments:

Post a Comment