Tuesday, September 10

Taharuki kubwa yaibuka katika mpaka wa Rwanda na Tanzania.


Taharuki imeibuka katika mpaka wa Tanzania na Rwanda wakati madereva wa malori kutoka nchini wakihaha kuvuka kuingia Rwanda kabla ya kuanza kutumika kwa ushuru mpya wa barabara ambao unaanza kutumika tena leo kwa upande wa Rwanda ukilenga magari kutoka Tanzania tu.  

Rwanda iliongeza ushuru kwa zaidi asilimia 229 dhidi ya magari ya mizigo ya Tanzania tu kutoka viwango vya zamani vya Dola za Marekani 152 hadi Dola 500 kwa madai ya kutaka usawa na Tanzania. 
Ushuru huo ambao ulianza kutumika rasmi Septemba mosi mwaka huu kisha kusitishwa kwa muda, unatarajiwa kurejeshwa tena leo kulingana na tangazo la Rwanda mpakani Rusumo. 


Kadhia hiyo imesababisha msururu mrefu wa malori yanayoingia Rwanda kutoka Tanzania kuanzia jana ambayo ilikuwa siku ya mwisho kabla ushuri huo wa kutoka Dola za Marekani 152 hadi 500 kuanza kutozwa tena kuanzia leo. 


Kaimu Ofisa Mwandamizi wa Forodha wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) katika kituo cha Rusumo, Sure Mohamed, jana alilithibitisha NIPASHE kwamba wiki moja iliyopita serikali ya Rwanda iliweka ongezeko la ghafla la ushuru wa barabara kutoka Dola 152 hadi Dola 500 za Marekani. 
  
Alisema hali hiyo ilisababisha msururu mrefu wa magari umbali wa zaidi ya kilometa 20 kwa kuwa madereva wengi hawakuwa na taarifa za ongezeko hilo, hali iliyowalazimu kuwasiliana na waajiri wao ili wawatumie fedha za ziada. 

Hata hivyo, alisema ongezeko hilo la ushuru lililodumu kwa takribani wiki moja inakadiriwa magari zaidi ya 200 yalitozwa ushuru mpya wa Dola 500 kabla serikali ya Tanzania kufanya mazungumzo na serikali ya Rwanda na kufikia mwafaka wa kurejesha ushuru wa zamani wa Dola 152. 
 
Alisema ingawa serikali ya Rwanda ilikubali kurejesha ushuru wa zamani, lakini baadaye iliweka bango mpakani upande wake lililosema tozo hiyo ya zamani ingedumu hadi jana na baada ya hapo malori yatatakiwa kulipa Dola 500.“Ni kweli kulitokea ongezeko la ghafla la road toll (ushuru wa barabara) kwa upande wa wenzetu kutoka Dola 152 hadi Dola 500. 
 
Tulipouliza kwa nini wamefanya hivyo tena ghafla, walidai wanataka kuwa na kiwango sawa na cha kwetu,” alisema. 
Aliongeza kwamba kimsingi, madai hayo ya Rwanda kwamba wanataka kuwa na kiwango cha tozo sawa na cha Tanzania hayana ukweli wowote kwa sababu hapa nchini ushuru wa barabara unatozwa kulingana na umbali ambao gari linasafiri. 
 
“Sisi hapa nchini tunatoza ushuru wa barabara kwa kuangalia kilometa, hiyo Dola 500 wanayodai tunatoza ni umbali wa kutoka hapa Rusumo hadi Dar es Salaam ambao ni zaidi ya kilometa 1,800,” alisema Mohamed. 


Aliongeza kwamba kwa magari yanayoishia Isaka wilayani Kahama yanayotozwa Dola 110 tu, tofauti na Rwanda ambao wao kiwango chao ni kimoja hata kama gari litasafiri umbali wa nusu kilometa. 


DC NGARA ANENA
  Mkuu wa Wilaya ya Ngara, Constantine Kanyasu, alithibitisha serikali ya Rwanda kuongeza ushuru wa barabara kutoka Dola 152 hadi Dola 500 na kwamba baada ya mazungumzo na serikali ya Tanzania walikubali kurejesha kiwango cha zamani, lakini kwa muda tu. 
 
“Baada ya kufanya nao mazungumzo kuhusu uamuzi wao wa kupandisha ushuru wa barabara, walikubali kurejesha kiwango cha zamani, lakini wakasema wanafanya hivyo kwa muda tu ili kuruhusu magari yaliyokuwa tayari yamepakia mizigo Dar es Salaam hadi Septemba 9, hivyo tunasubiri kuona hiyo kesho (leo) kama watarejesha tozo mpya au wataendelea na tozo ya zamani,” alisema. 

Hata hivyo, Kanyasu alisema Tanzania ina mtandao mrefu wa barabara wa karibu kilometa 2,000 na ndiyo sababu tozo inafikia hadi Dola 500, lakini Rwanda ina mtandao wa barabara usiozidi kilometa 300, hivyo madai yao ya kupandisha ushuru wa barabara hauna maelezo ya kuridhisha. 
  
KAULI ZA MADEREVA  
Baadhi ya madereva wa malori ya mizigo waliozungumza na NIPASHE wakati wakisubiri kuvuka kuingia Rwanda walisema ingawa hawana uwezo wa kuzuia ongezeko la ushuru, lakini pia hawaoni kama lina tija hususani kwa wananchi wa Rwanda. 
  
Kassim Salum anayeendesha lori la mizigo la kampuni ya Bhanji Logistics ya jijini Dar es Salaam, alisema ameshangazwa na ongezeko hilo kwa upande wa Rwanda kwa sababu kwa upande wa Burundi kiwango ni kile kile cha Dola 152. 
 
“Kimsingi, hakuna tofauti kubwa ya kijiografia kati ya Rwanda na Burundi, lakini tumeshangaa kusikia kwamba Rwanda wanakusudia kupandisha ushuru kutoka Dola 152 hadi Dola 500 wakati wenzao wa Burundi kiwango ni kile kile na hakuna usumbufu wowote,” alisema. 
 
Aliongeza kwamba kama Rwanda wataendelea na msimamo wao ni wazi watakaoathirika ni wananchi wake kwa sababu wenye magari wataongeza gharama za usafirishaji na wafanyabiashara wataongeza bei ya bidhaa, hivyo atakayeathirika ni mlaji wa mwisho ambaye ni mwananchi wa Rwanda. 
  
John Nzigila, anayeendesha lori la Kampuni ya Mafuta ya Eafco, alisema alifika katika mpaka wa Rusumo juzi na kukuta foleni kubwa. 
  
Alisema pengine foleni hiyo ilitokana na malori mengi kutaka kuwahi kuvuka kuingia Rwanda kabla ya jana ambayo ilikuwa siku ya mwisho ya kutozwa kiwango cha zamani cha ushuru. 
  
“Mimi nimeingia hapa jana (juzi) na nililazimika kulipia hiyo hiyo jana (juzi) ili kuepuka kulipa tozo mpya ambayo tuliambiwa inaanza kesho,” alisema Nzigila. 
 
Naye Zuberi Denya anayeendesha lori la mizigo la Kampuni ya Kleb ya jijini Dar es Salaam, alisema serikali ya Rwanda ina uhuru wa kuongeza ushuru kadri itakavyoona inafaa, lakini haoni kama kulikuwa na sababu yoyote ya msingi ya kufanya hivyo hivi sasa. 
 
“Unajua katika siku za karibuni kumekuwapo na mgongano wa kisiasa kati ya Tanzania na Rwanda, hivyo hatuwezi kuhusisha moja kwa moja ongezeko la ushuru na mgongano huo, lakini tunajiuliza kwa nini wafanye hivyo sasa hivi baada ya Tanzania kuwataka wahamiaji haramu kurejea kwao?” 
 
NIPASHE ambalo limefika eneo la Rusumo kwenye mpaka wa Tanzania na Rwanda jana lilishuhudia msururu mrefu wa malori yakisubiri kuvuka mpaka huku baadhi ya madereva wakijaribu kuvunja utaratibu na kuchepuka foleni kwa lengo la kutaka kuwahi. 
  
KAULI YA WAZIRI MGIMWA  
Waziri wa Fedha, Dk. William Mgimwa, jana aliliambia NIPASHE kuwa amesikia habari hizo, lakini alisema mazungumzo kuhusiana na suala hilo kati ya Tanzania na Rwanda yanaendelea. 
 
Dk. Mgimwa alisema kesho atakutana na waziri mwenzake wa Fedha wa Rwanda jijini Kampala, Uganda kuzungumzia suala hilo. 
  
Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, hakupatikana jana kuzungumzia suala hilo kwani simu zake zilikuwa zimefungwa. 

  
Hata hivyo, Naibu wake, Dk. Charles Tizeba, alipoulizwa jana, alisema asingeweza kulizungumzia suala hilo kwa kuwa alikuwa katika ziara ya Rais Jakaya Kikwete mkoani Mwanza na kushauri aulizwe Waziri Mwakyembe. 
  
TATOA YATANGAZA MSIMAMO  
Naye Msemaji wa Chama cha Wamiliki wa Malori Tanzania (Tatoa), Elias Lukumay, alisema msimamo wao uko pale pale kwamba hawatakuwa tayari kulipa nyongeza ya ushuru. 

Lukumay alisema wataendelea kusimamisha magari mpakani mpaka pale mawaziri wawili wa fedha watakapokutana na kufikia mwafaka. 
  
Septemba 3, mwaka huu, Serikali ya Tanzania ilisema mgogoro wa ushuru mpakani kati ya wafanyabiashara wa Tanzania na Rwanda kwa sasa umemalizika. 


Hayo yalisemwa na Naibu Waziri wa Uchukuzi, Dk. Charles Tzeba, na kusema kuwa wafanyabiashara wa Kitanzania walisumbuliwa baada ya kulazimika kulipa Dola 500 za Marekani ili kuingiza mizigo yao Rwanda. 
  
Alisema baada ya kutokea tatizo hilo, alimpigia simu Waziri wa Uchukuzi wa Rwanda, Profesa Silas Lwakabamba, ambaye alisema hana taarifa juu ya taarifa hizo na kuwasiliana na Waziri wa Fedha wa Rwanda ambaye alimpa taarifa kuhusiana na suala hilo. 
  
Hata hivyo, Tzeba alikanusha madai ya kupandishwa ushuru huo kutokana na mgogoro wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Rwanda. 


Alisema walipata taarifa zisizo rasmi kuwa Rwanda ingepandisha gharama za ushuru kuanzia mwanzoni mwa mwezi huu na kwamba walikuwa wakisubiri taarifa rasmi. 

Hata hivyo, alisema taarifa hizo zilikuwa na ukweli kwani Septemba Mosi, mwaka huu alipigiwa simu kutoka mpakani kuwa magari ya Tanzania yamezuiwa eneo la Rusumo na wanatakiwa walipe Dola 500. 
 
Tzeba alisema baada ya kuwasiliana na Profesa Lwakatamba walikubaliana kuwa suala hilo litafanyiwa kazi na mawaziri wa fedha wa nchi hizo mbili.

- Nipashe.

Ndugai ataja sababu zake zilizomfanya amtimue Freeman Mbowe Bungeni

NAIBU Spika, Job Ndugai ametetea uamuzi wake wa kuagiza kutolewa ndani ya ukumbi wa Bunge, Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe akisema alikuwa sahihi.

Mabishano hayo ambayo yalisababisha kuibuka kwa vurugu bungeni yalitokea mwishoni mwa wiki, muda mfupi baada ya kipindi cha maswali na majibu, ambapo kiongozi huyo wa Bunge aliruhusu mjadala kuhusu Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba uendelee.

Kutokana na hali hiyo, Mbowe alisimama kutaka kutoa ufafanuzi juu ya mjadala huo, lakini Ndugai alimzima na kumtaka kukaa chini, jambo ambalo halikumfurahisha Mbowe na kumfanya agomee agizo lake.

Akizungumza na MTANZANIA jana kwa njia ya simu, Ndugai alitumia muda mwingi kutetea uamuzi wake na kukosoa hoja za watu wanaompinga juu ya uamuzi wake huo.

Ndugai alisema katika kikao hicho, Mbowe alifanya jeuri kubishana na kiti na kueleza kuwa kanuni za Bunge zinasema hakuna mbunge yeyote atakayesimama kuzungumza bila kuruhusiwa na kwamba uamuzi wa kiti ndiyo wa mwisho.

Ndugai alisema wanaomtuhumu kwamba hakutenda haki kumuamuru Mbowe akae chini, wanafanya hivyo kwa vile hawajui kanuni za Bunge.

Ndugai alisema kwa mujibu wa kanuni, ni Rais wa Jamhuri pekee ndiye anayeruhusiwa kulihutubia Bunge kwa wakati anaoona yeye unafaa, lakini si mbunge.

“Hata rais mwenyewe ni lazima amwandikie barua spika, huu ndiyo utaratibu lakini si mbunge au waziri anayeruhusiwa kusimama kwa wakati anaoutaka yeye kuzungumza akaruhusiwa, ni lazima ataomba ruhusa kwa Spika na kama ipo nafasi ya kufanya hivyo Spika atamruhusu, kama haipo hataruhusiwa.

Alipoulizwa kwamba haoni kama alivunja kanuni kwa kumzuia Kiongozi wa Upinzani bungeni wakati kanuni za mabunge ya Jumuiya ya Madola zinatoa upendeleo kwa kiongozi huyo na waziri mkuu ndani ya Bunge, Ndugai alisema:

“Katika vikao vya Bunge, uamuzi wowote wa Spika unakuwa wa mwisho na hauwezi kupingwa na mbunge au waziri yeyote.

“Mbowe nilimuomba kwa heshima sana atupishe kwanza, nilimuelekeza karibu mara tatu…lakini mtu mzima anavunja utaratibu.

“Huyu Mbowe amejivunjia heshima mwenyewe, hata kanisani anayeendesha ibada ni mtu mmoja tu, na wengine wanapaswa kufuata utaratibu.

“Kwanza Mbowe alijitoa mwenyewe kwenye orodha kwa maandishi na ninayo hapa.... yeye na Halima Mdee, sasa alisimama kufanya nini kama sio ujeuri?

“Kanuni anazijua mimi ningemruhusu tu, lakini kwa ujeuri hakufanya hivyo. Kuna taratibu za bunge, mbunge anakaa chini pale Spika anaposimama na wasome kanuni, sasa hapo mjeuri ni nani?

“Tujifunze kanuni haiwezekani mtu yeyote asimame saa yoyote, kila mmoja hawezi kufanya anavyotaka, kuna taratibu zake, kiti kikimuona atapewa nafasi kama ipo na iwapo kiti kikiridhika,” alisema Naibu Spika.

Awatetea askari wa Bunge

Akizungumzia hatua ya kuwaamuru askari wa bunge kuingia ndani ya ukumbi wa Bunge na kumtoa Kiongozi wa Upinzani, iwapo kama amevunja kanuni, Ndugai alisema hakuvunja kanuni na kufafanua kila askari aliye kwenye viunga vya bunge yuko chini ya himaya ya kiti.

“Kila askari aliye kwenye eneo la bunge au viunga vya bunge kuanzia polisi, usalama wa taifa na wengine wote siwezi kuwataja hapa, hao wote wako chini ya bunge ni Sajent at Arms.

“Askari polisi wote unaowaona bungeni wanaletwa na RPC Dodoma na wanakuwa chini yetu, hakuna askari aliyetoka nje siku ile…. Ni uongo na hawajui kanuni.

“Uamuzi wa kuita wanausalama ndani ya ukumbi ulikuwa ni uamuzi sahihi, hakuna askari aliyetoka nje ya bunge,” alisisitiza Ndugai.

Msekwa amuunga mkono Ndugai

Naye Spika Mstaafu aliyeongoza Bunge la nane, Pius Msekwa alimtetea Ndugai akisema kuwa haoni kosa lolote lililofanywa na kiongozi huyo wa Bunge.

Msekwa ambaye alipata kuwa Makamu Mwenyekiti wa CCM (Tanzania Bara), alisema ni jambo la kawaida ndani ya Bunge, Spika kumuamuru mbunge au waziri kukaa chini pale anapoona inafaa.

“Spika ni sawa na mwenyekiti wa kikao chochote, anayo madaraka ya kuruhusu nani aseme, nani asiseme.

“Tuje bungeni sasa, Ndugai ndiye anayeamua nani aseme, ni sahihi ndiye mwenye mamlaka hayo na ni jambo la kawaida kabisa,” alisema Msekwa.

Akitoa uzoefu wake wa bunge alilokuwa akilisimamia, Msekwa alisema matukio yanayotokea bungeni sasa yamegubikwa na hisia za ujana zaidi na kusisitiza wazee walio nje ya bunge wanatafakari cha kufanya kabla hali haijaharibika.

“Sisi yetu macho… lakini kila zama na kitabu chake, hizi ndio zama za vijana, wakati wetu haya hayakuwapo…lakini ikifikia hatua ya kutaka kuliteketeza bunge lazima tutachukua hatua… lakini dalili sio nzuri,” alisema Msekwa.


-Mtanzania 

Monday, September 9

CUF: Ndugai anahujumu

Dar es Salaam. Chama cha Wananchi (Cuf), kimesema kitendo cha Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai kukataa kumpa nafasi Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe na kuamuru askari wa Bunge wamtoe nje ya ukumbi huo ni kumhujumu Rais Kikwete kwenye azma yake ya kupata Katiba Mpya.
Pia, chama hicho kimesema kinafanya juhudi za kuwasiliana na viongozi wa vyama vingine ili kuweka mkakati wa pamoja wa kukabiliana na hujuma dhidi ya mchakato wa kupata Katiba Mpya na kuimarisha umoja wa kitaifa  kwenye kipindi hiki cha kukabiliana na changamoto za nchi jirani.
Akizungumza Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa chama hicho, Profesa Ibrahimu Lipumba alisema, Cuf inalaani vitendo vya kuwanyanyasa na kuwadhalilisha wabunge wa upinzani akiwamo Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni na kudai kuwa inaonyesha wazi CCM wanampango wa kutengeneza katiba ya upande mmoja.
“Kwa mfumo wa mabunge ya Jumuiya ya Madola, kwa Tanzania Waziri Mkuu na kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni ndiyo wanawakilisha pande mbili ndani ya Bunge, hivyo kumnyima Mbowe fursa ya kuzungumza ni unyanyasaji na udhalilishaji na kwamba kitendo hicho hakikubaliki,” alisema.
Profesa Lipumba alisisitiza muswada uliokuwa unajadiliwa  ulikuwa na utata, Serikali imeubadili kwa nguvu na kuondoa maoni muhimu ya wadau.


Tutatumia nguvu ya umma kukwamisha Katiba

Dodoma. Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema kitatumia nguvu ya umma kuikataa Katiba Mpya endapo CCM na Serikali yake: “vitaendeleza hila na ubabe katika mchakato unaoendelea.”
Pia chama hicho kikuu cha upinzani nchini, kimeitaka Serikali kuboresha Daftari la Kudumu la Wapigakura kabla ya upigaji wa kura ya maoni ya Katiba Mpya huku kikisema kinyume chake suala hilo litaibua mgogoro mkubwa.
Kauli hizo zimetolewa kwa nyakati tofauti na Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na Mkurugenzi wa Mawasiliano wa chama hicho, John Mnyika katika mahojiano yaliyofanyika Mjini Dodoma mwishoni mwa wiki.
Mnyika alisema baada ya CCM kuhodhi muswada wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba na hivyo kulifanya Bunge la Katiba liwe ni hodhi ya chama hicho tawala karata pekee waliyobakiwa nayo ni kura ya maoni... “Rais Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM, ndiye atakayeteua wajumbe 166 kutoka taasisi na makundi na kufanya Bunge zima la Katiba kuwa na wajumbe zaidi ya 600.”
Alisema kwa sasa, Tanzania Bara hakuna utaratibu wa kikatiba wa namna ya kuendesha kura ya maoni na kuongeza.
“Wenzetu Zanzibar katika Katiba yao wanao mfumo wa kura ya maoni, sisi haupo ni lazima tutengeneze sheria ya kura ya maoni ya Katiba Mpya na Sheria ya kura ya maoni ya Muungano,” alisema Mnyika.
Mnyika alisema Kamati ya Bunge la Katiba, Sheria na Utawala inapaswa kuanza kukutana kwa dharura kupata maoni ya wadau kuhusu kura ya maoni na ianze na Zanzibar ambayo haikushirikishwa.
“Kamati ianze sasa, isisubiri Bunge la Oktoba 29 maana kati ya mambo yaliyoifanya Serikali kuondoa muswada wa Sheria ya Kura ya Maoni ni mgongano wa kikatiba kati ya Zanzibar na Muungano,” alisema.
Alisema pia Tanzania inahitaji kuwa na Katiba ya mpito ambayo itaweka chombo huru kitakachosimamia upigaji wa kura ya maoni badala ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).
Mbowe alisema Serikali ya CCM inatumia hila na ubabe kuhakikisha inapatikana Katiba Mpya itakayobeba masilahi ya chama hicho kwa gharama yoyote.
 “Endapo CCM itaendelea na hila zake hizi niwaambie Chadema tumejipanga… Tutatumia teknolojia ya kisasa kuwafikia Watanzania hata ikibidi kutumia helikopta nne ili waikatae wakati wa kupiga kura ya maoni,” alisema Mbowe na kuongeza: “Hila yoyote itakayotokea kwenye Katiba tutahamasisha Watanzania kuikataa, wasifikiri wanachokifanya ni salama kwao… Wanageuza mchakato kuwa wa kichama badala wa wananchi.”
Alisema msimamo wa CCM kukataa mapendekezo ya muundo wa Serikali tatu si wa wanachama wake wa kawaida, bali matakwa ya viongozi wake wa juu.

“Tunapozungumzia kumdhibiti Rais, wao (CCM) wanafikiri tunamzungumzia Rais Kikwete (Jakaya)… Tunataka kudhibiti madaraka ya Rais yeyote ajaye awe wa  Chadema, CCM au NCCR”.
Alisema mapendekezo ya wananchi kuhusu Serikali tatu yalianzia wakati wa Rais wa Zanzibar, Aboud Jumbe mwaka 1984 na baadaye mwaka 1991 wakati wa Tume ya Jaji Mkuu Francis Nyalali.
Alisema pamoja na kutotekelezwa kwa mapendekezo hayo ya wananchi, bado wabunge wa G55 walianzisha vuguvugu hilo lakini likazimwa kwa kutumia nguvu kubwa.
“Tume ya Jaji Robert Kisanga nayo ilikuja na mapendekezo hayohayo na sasa Tume ya Jaji Joseph Warioba na bado CCM haitaki kuamini ni ya wananchi,” alisema.
Mbowe alisema ndiyo maana Chadema sasa kimeamua kujitoa mhanga kuwahamasisha hadi wanachama wa CCM kuikataa Katiba Mpya endapo itapatikana nje ya matakwa ya Watanzania... “ Nia tunayo, sababu tunayo na uwezo tunao.”
Alisema matumizi ya polisi hayatalipatia taifa Katiba Mpya na nzuri. “Wajue kuwa wako Watanzania wenye busara kwa mamilioni walioko nje ya Bunge ambao wana sauti katika Katiba yao na CCM wasifikiri wao ni alfa na omega (mwanzo na mwisho),” alisema Mbowe.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia amesema hata kama Tanzania haitapata Katiba Mpya hadi ifikapo 2015, bado ya sasa haitafaa kutumika.
“Hata kama tutashindwa kupata Katiba Mpya hatuwezi kwenda kwenye uchaguzi na katiba hii ya sasa kwa sababu katiba mpya ya Zanzibar imejiingiza katika mgogoro na Katiba ya Muungano,” alisema.
Alisema kama dalili za kutopatikana kwa Katiba Mpya zimeanza kuonekana, ni vyema ikatumika busara na hekima katika kuvuka kikwazo hicho na njia pekee ni meza ya mazungumzo.
“Sisi siyo tutakaoifanya Tanzania isitawalike, bali CCM…  Tunafanya haya kwa nia njema kabisa, hatutaki damu ya Watanzania imwagike kwa jambo linaloepukika,” alisema.

Friday, September 6

‘Marekebisho yanazungumzika bungeni’




Dodoma. Waziri Mkuu, Mizengo Pinda amesema Serikali haitauondoa Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba kwa sababu mambo ambayo Kambi ya Upinzani Bungeni inayadai, yanazungumzika na yanaweza kubadilishwa kwa mamlaka ya wabunge.
Pinda alikuwa akijibu swali la nyongeza la Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe katika kipindi cha Maswali ya Kwa Waziri Mkuu Bungeni, Dodoma jana.
Mbowe ambaye pia ni Mbunge wa Hai (Chadema), alisema yapo matukio ya kibabe, kejeli, matusi na ya dharau ambayo yamekuwa yakifanya kuchelewa kwa utaratibu mzima wa utungaji wa sheria... “Pamoja na rai mliyoiondoa, sisi tunasema yapo maeneo mengi yasiyo na tija ambayo yanafanya msingi wa marekebisho ya sheria mlioleta jana (juzi), kuwa hayana tija kwa mchakato huu.”
Akijibu swali hilo, Pinda alisema: “Hivi kweli Mbowe una ngoja hadi muswada unafika ngazi ya Bunge, ndipo unakuja na hoja hiyo wakati tulikuwa na fursa kubwa?”
Alisema kwa mambo ambayo alielezwa kuwa ndiyo yaliyosababisha wabunge wa kambi ya upinzani kutoka nje ya Ukumbi wa Bunge juzi, hakuna atakayeona umuhimu wa kuondoa muswada huo.
“Kwa sababu ni vitu ambavyo ndani ya Bunge hili vinazungumzika na vinaweza kubadilishwa kulingana na mamlaka mliyopewa,” alisema.
Katika swali la msingi, Mbowe alisema mchakato wa Katiba Mpya unahitaji ustahimilivu, ushirikiano, uwazi, dhamira njema na kwamba wabunge wanapaswa kutambua kuwa wapo wadau nje ya Bunge wanahitaji ushirikiano.
Pinda alisema: “Mategemeo ni wabunge tulio ndani tutaujadili muswada huu kikamilifu na maeneo yote ambayo yanadhaniwa yanaweza yasiwe na tija, neema kwa nchi yetu, ni jukumu letu kujadili kwa uwazi, uaminifu na kiukweli.
Mbunge wa Kuteuliwa, James Mbatia (NCCR –Mageuzi), alihoji kama Serikali haioni ni busara mazungumzo ya kisiasa kufanyika kwanza kisha yakafuatiwa na sheria ambayo itasaidia kuunda dhana ya dola. Alisema kumekuwa na ukiukwaji mkubwa wa Katiba kwa kuruhusu mabadiliko ya Katiba ya Zanzibar.
Kuhusu hilo, Pinda alisema kulikuwa na mashauriano makubwa kati ya vyama, taasisi na pande mbili za Muungano kabla muswada huo kufikishwa bungeni na kwamba Katiba Mpya itameza yote yaliyomo katika katiba hiyo ya zamani na kuja na mawazo mapya ambayo itaongoza Taifa.

Mheshimiwa SUGU anasakwa na polisi kwa kosa la kuwakashifu walinzi wa Bunge

Taarifa kutoka Dodoma zinadai kuwa kuna Askari mmoja ambaye ni miongoni mwa walinzi wa Bunge ameenda kufungua faili Polisi Dodoma na kusema kuwa ametishiwa kupigwa na Mbunge Sugu...
Baada ya kufungua Jalada hilo polisi wamechukua Difenda 6 na wameingia mitaani kumtafuta ili awekwe ndani mpaka kesho ndio afikishwe mahakamani asubuhi.

"Mbowe ni Mjinga na Mpuuzi"...Hii ni kauli ya Kigwangalla bungeni

Mbunge wa Nzega Dr. Kigwangalla, ametumia muda wake karibu wote wa kuchangia Muswada wa Katiba kwa kumshambulia Mwenyekiti wa CHADEMA, Mhe. Mbowe kuwa ni Mjinga, Mpuuzi, ametia aibu aibu 
Kigwangalla  amempongeza  Naibu  Spika  kwa  kumtimua  Mbowe  bungeni  na  kusema  kuwa  kitendo  hicho  kimemshikisha  adabu...
Aidha, mbunge  huyo  wa  Nzega amedai kuwa Mbowe sio Mchaga bali ni mhuni fulani  aliyejivika  sura  ya  Uchaga  kwa  masilahi  yake  binafsi !.
Kigwangalla  alihitimisha  mchango wake  kwa  kudai  kuwa wapinzani wana akili za shetani  zisizovumilika!

Wananchi walilaani Bunge la Tanzania kutokana na vurugu zinazoendelea

Baada ya kuibuka mvutano mkali bungeni jana, kati ya Naibu Spika, Job Ndugai na wabunge wa Kambi ya Upinzani, wasomi, wanaharakati, Chama cha Madaktari Tanzania (Mat), Chama cha Walimu Tanzania (CWT) na Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (Tucta), vimesema kinachoendelea sasa ndani ya Bunge ni masilahi ya vyama vya siasa siyo taifa.
 

Walitoa kauli hiyo muda mfupi baada ya Naibu Spika, Job Ndugai kuwataka askari kumtoa nje ya Ukumbi wa Bunge, Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe.
 

Mbowe aligoma kukaa chini na kuungwa mkono na wabunge wa upinzani, akishinikiza kuahirishwa kujadiliwa kwa Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, hadi hapo Zanzibar itakaposhirikishwa, muda mfupi baada ya wabunge kupiga kura na 156 kutaka ujadiliwe na 56 wakitaka uondolewe.
 

Wabunge hao wa upinzani kutoka vyama vya Chadema, CUF na NCCR- Mageuzi, juzi walitoka nje ya Ukumbi wa Bunge wakishinikiza kuahirishwa kujadiliwa kwa muswada huo. 
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Bashiru Ally alisema mvutano huo umejaa masilahi ya wanasiasa kwa kila upande kujaribu kuvutia kwake.
 

“Mvutano ule hauzungumzi kabisa mwafaka wa Bunge la Katiba, binafsi nadhani Bunge la Katiba linatakiwa kuwa na wabunge wapya kabisa na wasiotoka katika chama chochote cha siasa,” alisema
 

Katibu Mkuu wa Tucta, Nicolaus Mgaya alisema: “Marekebisho hayo yanafanyika kwa ajili ya mustakabali wa Muungano wetu, kama Zanzibar hawakushirikishwa, uwekwe utaratibu wa jambo hilo kufanyika ili kipatikane kitu bora, siyo bora Katiba.”
 

Alisema nchi zilizoendelea zimepata mafanikio kwa kuwa zina Katiba nzuri ambazo zinaweza kudumu kwa miaka 100 kabla ya kufanyiwa marekebisho..

Ripoti maalumu ya gazeti la MWANANCHI kuhusu vurugu zilizotokea jana bungeni


Jana, Bingwa wa Dunia wa uzani wa kati (super middle), unaotambuliwa na Shirikisho la Ngumi Duniani (WBF), Francis Cheka alitembelea Bunge baada ya kutwaa taji hilo karibuni na jana hiyohiyo, Bunge hilo lilishuhudia ngumi kavukavu katika vurugu kubwa pengine kuliko zote zilizowahi kutokea katika ukumbi wake. 

Katika masumbwi hayo yasiyo rasmi, Mbunge wa Mbeya Mjini (Chadema), Joseph Mbilinyi ‘Sugu’ anadaiwa kumpiga kichwa Askari wa Bunge na kumchania sare na kung’oa kipaza sauti.
 

Mbilinyi jana alisema alikuwa anatafutwa na polisi huku akisema hilo limemshangaza akidai kwamba yeye ndiye aliyeshambuliwa na askari huyo.
 

Vurugu hizo zilitokea baada ya Naibu Spika, Job Ndugai kuamuru kutolewa nje kwa Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe.
 

Katika vurugu hizo Mbilinyi alibebwa juujuu na polisi hadi nje ya ukumbi huku akiwa hana viatu.
 

Pamoja na tafrani hiyo, Ndugai alisema wakati akihitimisha kikao cha Bunge kipindi cha asubuhi kuwa amewasamehe wabunge wote waliohusika na kosa hilo la utovu wa nidhamu na kuwaruhusu kurejea kipindi cha jioni kuendelea na Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba. 

Hata hivyo, wabunge wote CUF, NCCR-Mageuzi na Chadema ambao baada ya tukio hilo walitoka nje ya ukumbi, hawakurejea na baadaye walitoa msimamo wa pamoja wakisema hawatashiriki katika mjadala huo.
 

Msimamo huo ulitolewa na Mbowe ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chadema, Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia na Mbunge wa CUF, Habib Mnyaa.
 

Mbowe alisema wameamua kususia majadiliano hayo kuonyesha msimamo wao wa kupinga kupitisha mambo yasiyo na masilahi kwa nchi.
  
“Hatuko tayari kushiriki katika uchakachuaji wa Katiba... Matumizi ya nguvu ya polisi kamwe hayatatupatia Katiba nzuri,” alisema. Alisema kambi rasmi ya upinzani inalaani vikali kitendo cha Ndugai kuruhusu Bunge kunajisiwa kwa kuruhusu polisi kuingia ndani kinyume na kanuni.
 

Mnyaa alisema kitendo cha wadau wa Zanzibar kutoshirikishwa katika kutoa maoni yao katika muswada huo wa marekebisho ni dharau kubwa.
 

Mbatia alisema Tanzania haiwezi kuingia Uchaguzi Mkuu wa 2015 kwa kutumia Katiba ya sasa kwa sababu tayari kuna mgongano wa kikatiba kati ya Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
 

Mnadhimu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Tundu Lissu alimtaka Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Kuu, (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi kutoa ushahidi kama Rais aliteua wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba kulingana na mapendekezo ya taasisi zao.

Kuanza kwa tafrani
Sakata hilo lilianza saa 6:45 mchana muda mfupi baada ya kukamilika kwa kura kuamua kama Bunge liahirishwe au la kutokana na hoja iliyotolewa na Mbunge wa Mkoani (CUF), Ali Hamisi Seif (CUF). Waliotaka liahirishwe walipata kura 59 na waliokataa 159.

Baada ya Ndugai kutangaza matokeo hayo na kutaka shughuli za Bunge ziendelee, Mbowe aliposimama na kusema ana hoja Naibu Spika alimwamuru akae chini.

Baada ya Mbowe kusisitiza ana hoja na kumwomba Spika amsikilize ndipo Ndugai alipomwamuru atoke nje na alipokaidi alisema:” Naomba askari wote waliopo katika mazingira haya (ya Bunge) waingie ndani ya ukumbi wa Bunge”.

Baada ya kitambo kifupi, Mbowe akiwa bado amesimama alitoa maagizo atolewe nje: “Kiongozi wa upinzani atolewe nje.”

Polisi waliingia ndani ya Ukumbi wa Bunge lakini Wabunge wa Kambi ya Upinzani kwa umoja wao, walimzinga Mbowe asifikiwe na askari hao.

Baada ya kuona polisi wanaelekea kushindwa, Ndugai alitoa maagizo mengine: “Askari hamjaletwa humu ndani kufanya majadiliano mnatakiwa kuhakikisha kiongozi wa upinzani anatolewa nje”.

Alisema yeye ndiye anayeendesha kikao hicho hivyo lazima Mbowe atolewe nje.

Hapo ndipo wabunge hao wa upinzani walipoanza kuimba: “Hatutaki kuburuzwa hatutaki kuburuzwa… hatutaki kuonewa,” huku wakiendelea kumzinga Mbowe.

“Askari wote mliopo humu ndani naomba mnisikilize… Sasa naagiza kwa mara ya mwisho... nasema kiongozi wa upinzani atolewe nje.”

Ngumi zarushwa
Baada ya kauli hiyo ya Ndugai, ndipo polisi walipotumia nguvu hasa kwa Mbilinyi na Mbunge wa Maswa Mashariki (Chadema), Silvester Kasulumbai.

Katika patashika hiyo, inadaiwa kwamba Mbunge wa Kasulu Mjini (NCCR-Mageuzi), Moses Machali alipigwa ngumi ambayo ilimfanya apepesuke hadi sakafuni.

Kilichomponza Mbilinyi ni hatua yake ya kusogelea Siwa. Polisi waliokuwa karibu, walimbeba juujuu hadi nje ya ukumbi.

Wakati akitolewa nje ya ukumbi, alijaribu kujizuia kwa kushika kipaza sauti kinachotumiwa na upande wa upinzani hadi kikang’oka.

Mbunge wa Viti Maalumu (CUF), Mozza Abeid, alivuliwa hijabu katika vurumai hizo wakati polisi walipokuwa wakitumia nguvu ili kumfikia Mbowe.

Baada ya kuona hali inazidi kuwa mbaya, Mbowe aliamua kutoka nje huku akisindikizwa na polisi pamoja na wabunge wa vyama hivyo na alipofika nje ya ukumbi alipokewa na polisi wa kawaida waliomweka chini ya ulinzi kabla ya kumwachia baada ya ombi la Mbunge wa Rombo (Chadema), Joseph Selasini.

Kutokana na hali ya mambo kuwa tete, askari wa Bunge waliwaondoa wageni waliokuwa wamekaa katika kumbi za wageni wakiwamo wanafunzi wa shule mbalimbali za sekondari huku baadhi ya wabunge wa CCM waliokuwa na simu za kisasa za mkononi na kompyuta mpakato (Ipad) wakichukua picha za tukio zima.

Inadaiwa kwamba baada ya kutoka nje ya ukumbi, Mbilinyi alimtwanga ngumi mmoja wa askari waliomtoa kwa nguvu kabla ya kuamuliwa na wabunge na polisi.
Wakati wote huo, wafanyakazi wa Bunge na wageni walionekana wakiwa wamejikusanya katika makundi wakitafakari na kushangaa yaliyokuwa yakitokea.

Balaa lilivyoanza
Akitumia Kanuni ya 69(1), Mbunge wa Mkoani (CUF), Ali Hamisi Seif, alitaka kuahirishwa kwa mjadala wa Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba wa mwaka 2013 kutokana na ukweli kuwa Kamati ya Sheria, Katiba na Utawala ya Bunge ilipaswa kukusanya maoni ya wadau mbalimbali nchini ikiwamo upande wa Zanzibar jambo ambalo halikufanyika wakati wa maandalizi ya muswada huo.

“Ilipaswa sheria hii inapotaka kufanyiwa marekebisho iende tena kulekule Zanzibar lakini jambo la kusikitisha kamati inayohusika na masuala ya Katiba haikwenda. Mimi ni mjumbe wa kamati na tuliitwa Dar lakini ratiba waliyotupa haikuonyesha kama tungekwenda Zanzibar,” alisema. 

Mkosamali naye aliomba mwongozo kwa Spika, akisema kwa kuzingatia matakwa ya kiapo cha Spika au Naibu alipaswa kuendesha Bunge kwa haki bila upendeleo.

“Kanuni inasema Spika ama Naibu Spika ama Mwenyekiti ataendesha shughuli za Bunge kwa haki, uadilifu, bila chuki wala upendeleo wowote kwa kuongozwa na Katiba ya nchi,” alisema na kuongeza: “Kwa kuwa sisi tumekuweka hapo ili uendeshe Bunge kwa uadilifu, usiburuzwe na chama chako na uzingatie miongozo yote kwa wakati. Kwa nini usitumie mamlaka yako kuondoa muswada huu”?

Mbunge wa Peramiho (CCM), Jenister Mhagama aliomba mwongozo kwamba kwa kuwa bado kuna malalamiko basi waipe Serikali nafasi ya kuthibitisha kwamba majadiliano ya kamati yalikamilika.

Lissu katika kuomba mwongozo wake, alisema Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Sheria, Katiba na Utawala, Pindi Chana alilidanganya Bunge alipowasilisha maoni ya kamati kwamba wadau wa muswada huo walishirikishwa jambo ambalo alisema si kweli.

Lissu alisema hakuna Mzanzibari aliyefika mbele ya kamati hiyo kutoa maoni kuhusu muswada wowote.

Hata hivyo, Chana alijibu akisema wadau wa Zanzibar walitoa maoni yao na kukabidhi nyaraka mbalimbali kwa Spika kuthibitisha kauli yake hiyo. Alivitaja vyama vya Jahazi Asilia na ADC kuwa vilihojiwa.

Kwa upande wake, Lukuvi alimshambulia Lissu kwa kauli yake ya juzi kwamba uteuzi wa Wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba uliofanywa na Rais Jakaya Kikwete ulikuwa na walakini. “Lissu alisema jana (juzi) kwamba wapo wadau ambao walisema ijapokuwa waliandikiwa barua ya kuwasilisha majina matatu kila moja ili Rais ateue mmoja lakini hakuna mjumbe aliyeteuliwa”.

Alitaja majina ya walioteuliwa kuwa ni Maria Kashonda (Tec), Jesca Mkuchu (CCT), Humphrey Polepole (Civil Society) na Profesa Palamagamba Kabudi (Kundi la Wasomi).

Lukuvi aliwataja wengine waliopendekezwa na taasisi zao na Rais kuwateua kuwa ni Mwamtumu Malale (Bakwata) na Dk Sengondo Mvungi (NCCR) na Profesa Mwesiga Baregu wa Chadema.

Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Fredrick Werema alisema katika mchakato wa muswada huo, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) iliwasilisha maoni yake mbele ya kamati.

Alisema Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi aliwasilisha kwa kamati mapendekezo ya SMZ, Mei mwaka huu na mapendekezo hayo ikiwamo uteuzi wa wajumbe 166 yalizingatiwa.


Waacha muswada, wapiga vijembe
Baada ya kurejea katika kikao cha Bunge cha jioni jana, wabunge wa CCM waliopewa fursa ya kuchangia mjadala wa muswada huo walitumia muda mwingi kuwajadili wabunge wa kambi ya upinzani.

Thursday, September 5

Rais Kikwete na Paul Kagame wakutanishwa na Rais wa Uganda

Rais wa Uganda, Yoweri Museveni ameitisha mkutano wa dharura wa marais wa nchi za Maziwa Makuu (ICGLR), kujadili hali ya usalama Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. 

Rais Jakaya Kikwete ni miongoni mwa waalikwa kwenye mkutano huo ambao pia unatarajiwa kuhudhuriwa na Rais wa Rwanda, Paul Kagame.
 

Wakati hali ya usalama Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ikidhoofika, katika siku za karibuni, uhusiano wa Tanzania na Rwanda umekuwa wa shaka hasa baada ya Rais Kikwete kuishauri Serikali ya Rwanda kukaa na wapinzani ili kumaliza mzozo uliolikumba eneo la Maziwa Makuu.
 

Rais Kikwete alitoa ushauri huo wakati akiwa katika sherehe za maadhimisho ya miaka 50 ya Umoja wa Afrika (AU), zilizofanyika mjini Addis Ababa, Ethiopia. Mkutano wa leo utafanyika kwenye Ukumbi wa Commonwealth Resort, Munyonyo katikati ya Jiji la Kampala.
 

Kwa mujibu wa taarifa Rais Museveni ameitisha mkutano huo hasa kuzungumzia hatua ya Umoja wa Mataifa kupambana na Kundi la Waasi wa M23.
 

Mbali na viongozi hao wa Tanzania na Rwanda, viongozi wengine wanaotarajiwa kuhudhuria mkutano huo wanatoka Angola, Burundi, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Jamhuri ya Kongo, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Kenya, Sudan, na Zambia.

Kesi ya waziri mkuu Mizengo Pinda kutajwa septemba 16 mwaka huu...DPP adai kuwa hiyo ni kesi FEKI

KESI ya kikatiba iliyofunguliwa dhidi ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda kutokana na kauli yake ya kuruhusu wanaokaidi maagizo ya Dola wapigwe, itatajwa Septemba 16 mwaka huu katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.

Kesi hiyo ilifunguliwa Agosti mosi mwaka huu na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), dhidi ya Waziri Pinda na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), wakipinga kauli hiyo iliyotolewa bungeni.

Itasikilizwa na jopo la majaji watatu wa Mahakama Kuu, likiongozwa na Jaji Kiongozi Fakhi Jundu wengine ni Jaji Augustine Mwarija na Dk Fauz Twaib.

Inadaiwa Mei 20 mwaka huu, Pinda akiwa bungeni katika nafasi yake ya Waziri Mkuu, kinyume na Katiba ya Nchi alitoa kauli ya kuruhusu askari wa Jeshi la Polisi kuwapiga raia ambao hawatatii amri yao kunapokuwa na vurugu.

“Sasa kama wewe umekaidi, hutaki, unaona kwamba ni imara zaidi, wewe ndio jeuri zaidi watakupiga tuu na mimi nasema muwapige tu kwa sababu hakuna namna nyingine, eeh maana tumechoka sasa,” sehemu ya hati ya mashitaka iliyonukuu kauli ya Waziri Pinda.

Katika hati hiyo inadaiwa kwa mujibu wa utekelezaji wa Sheria za Jinai, kauli inayotolewa na kiongozi wa nafasi ya Waziri Mkuu, inaonekana kama amri inayopaswa kutekelezwa na vyombo vya Dola kama Polisi, hivyo itachukuliwa kama amri halali na kusababisha waendelee kuwatesa na kuwapiga wananchi wasio na hatia.

Aidha inadaiwa Pinda alivunja ibara ya 100 ya Katiba inayompa kinga mbunge anapotoa jambo lolote bungeni, kwa kuwa yeye hakuzungumza bungeni kama mbunge, bali alikuwa anatoa msimamo wa Serikali yake.

Akizungumza hivi karibuni, Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) alisema hakuna uhalali wa mashitaka hayo kwa sababu kauli ya Pinda kuwa pigeni haikuwa piga ua, alichosema ni kupiga wale wasiotaka kutekeleza amri halali na kuna sheria inayoruhusu wananchi kupigwa pindi wanapokaidi amri.