Tuesday, April 10

Trump aapa ''kutumia nguvu'' kujibu shambulio ''la kemikali'' Syria

Rais wa Marekani Donald Trump
Image captionRais Donald Trump amesema Marekani inapata ''msaada mzuri" juu ya nani aliyehusika na shambulio la Douma Jumamosi.
Rais wa Marekani Donald Trump ameahidi " kutumia nguvu " kujibu madai ya shambulio la kemikali nchini Syria, huku mataifa ya magharibi yakitafakari hatua watakayoichukua.
"Tuna njia nyingi za kijeshi,"aliwambia waandishi wa habari.
Aliongeza kuwa hatua ya kujibu shambulio hilo itaamuliwa katika kipindi cha "muda mfupi".
Bwana Trump alisema kuwa Marekani inapata ''msaada mzuri" juu ya nani aliyehusika na shambulio la Douma Jumamosi.
Duru za kitabibu zinasema makumi kadhaa ya watu waliawa katika shambulio hilo, lakini idadi kamili haijathibitishwa.
Bw Trump pia alijadili tukio hilo la rais wa Ufaransa Emmanuel Macron Jumatatu jioni, na viongozi wote walielezea utashi wao wa "kujibu kikamilifu".
Nikki Haley mjumbe wa Marekani katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa
Image captionMjumbe wa Marekani Nikki Haley alisema kuwa-wanaounga mkono jeshi la Syrian - wana "damu ya watoto wa Syria " mikononi mwao
Waziri Mkuu wa Uingereza Theresa May amesema kuwa "analaani vikali" kitendo cha "ukatili" kinachodaiwa kuwa ni shambulio la kemikali na akatoa wito kwa wanaomuunga mkono rais Bashar al-Assad kuwajibishwa.
Kauli za viongozi wa kimagharibi za kulaani shambulio hilo zimefuatia kikao cha malumbano katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ambapo Marekani na Urusi walitupia na maneno makali kuhusiana na tukio la Douma.
Muwakilishi wa Urusi kwenye baraza hilo Vassily Nebenzia alisema shambulio linalodaiwa lilipangwa na akaonya kwamba hatua za kijeshi za Marekani zinazolenga kujibu tukio hilo "litakuwa na athari mbaya".
Mjumbe wa Marekani Nikki Haley alisema kuwa-wanaounga mkono jeshi la Syrian - wana "damu ya watoto wa Syria " mikononi mwao na akambandika jina rais Assad kama "zimwi ".
Muwakilishi wa Urusi kwenye baraza hilo Vassily Nebenzia
Image captionMuwakilishi wa Urusi kwenye baraza hilo Vassily Nebenzia alisema linalodaiwa kuwa la kemikali dhidi ya Douma lilipangwa
Bi Haley alitoa wito wa kupigwa kura juu ya muswada wa maazimio ya kubuniwa kwa tume ya uchunguzi juu ya matumizi ya silaha za kemiikali nchini Syria siku ya Jumanne.
Lakini Urusi inasema haiwezi kuunga mkono pendekezo hilo kwasababu lina "vipengele visivyokubalika''.

Ni kipi kilichotokea Jumamosi?.

Shirika la matibabu la Marekani na Syria linasema kuwa watu zaidi ya 500 waliletwa kwenye kituo cha matibabu katika mji wa Douma, uliopo katika jimbo la mashariki la Ghouta , karibu na mji mkuu Damascus, wakiwa na dalili "zinazoonesha kuwa walishambuliwa na kemikali".
Shirika hilo linasema dalili walizaokuwa nazo ni pamoja na ugumu wa kupumua, ngozi ya samawati , kutokwa na povu mdomoni , kuungua kwa mboni na "walikuwa na harufu kama ya kemikali ya chlorine".
Idadi kamili ya vifo ya na ni nini hasa kilichotokea haviwezi kuthibitishwa kwasababu eneo hilo halina mawasiliano.
Makadirio ya idadi ya watu waliouawa katika shambulio linaloshukiwa kuwa la kemikali ni kuanzia watu 42 hadi zaidi 60, lakini makundi ya kitabibu yanasema idadi hiyo inaweza kuongezeka baada ya wahudumu wa uokoaji kuweza kufika kwenye sehemu za chini za majengo ambako mamia ya familia walikuwa wamekimbilia kuepuka mashambulio ya mabomu.
Muwakilishi wa Ufaransa katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa amesema gesi ya sumu ilitumiwa kwa makusudi kwasababu inaweza kusambaa hadi sehemu za chini za majengo hadi.
Marekani ,ufaransa na Uingereza wameongoza kampeni ya kimataifa ya kulaani shambulio hilo linalodaiwa kuwa la kemikali, huku serikali ya Syria na waungaji mkono wao Urusi wakikana kuwajibika kwao kokote na tukio hilo.

No comments:

Post a Comment