Friday, April 27

TPDC yawataka wananchi kujiunga makundi kuomba kuunganishwa bomba la gesi asilia


Dar es Salaam. takriban nyumba 70 na viwanda viwili vinatarajiwa kunufaika na awamu ya kwanza ya usambazaji gesi asilia, huku watu wengine wakishauriwa kutuma maombi baada ya kujiunga kwa pamoja ili kupata huduma hiyo kwa gharama nafuu zaidi.
Hayo yalibainishwa juzi na kaimu mkurugenzi mtendaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Kapuulya Musomba, wakati wa uzinduzi wa kituo cha kupunguza mgandamizo wa gesi na maungano ya bomba linalokwenda katika makazi ya watu.
Musomba alisema awamu ya kwanza viwanda viwili vya Mikocheni vitaunganishwa (CocaCola na Bidco), lakini itawanufaisha zaidi wakazi wa maeneo ambayo bomba hilo linapita ya Ubungo Kibo, Shekilango, Sinza Sarvey na Mikocheni na maeneo mengine ya karibu na hapo.
“Changamoto ya usambazaji wa huduma ya gesi ni gharama kuanzia vifaa vyake, awamu hii tumetumia kuanzia Sh4 bilioni hadi Sh5 bilioni... ni rahisi zaidi watu wengi wanaokaa sehemu moja wakiungana wakaomba kwa pamoja,” alisema.
Alisema gharama hiyo itazingatia zaidi umbali wa nyumba na mazingira yaliyopo kulifikia bomba kuu na kwamba, mabomba yanayotumika kuunganisha katika nyumba yanazalishwa nchini ila tatizo ni vifaa hivyo vingine ambavyo lazima viagizwe nje ya nchi.
Naye naibu meneja wa Kampuni ya Sinoma East Africa, Lu Xiaoqiang ambao ndiyo wanatekeleza awamu hiyo, alisema wanatarajia kukamilisha kazi hiyo kwa ubora na muda uliopangwa lakini zaidi watajikita kuwajengea uwezo wazawa ambao ndiyo watashirikiana.

No comments:

Post a Comment