Tuesday, April 10

Sakata la kufungiwa nyimbo laibuka bungeni

Dodoma. Sakata la kufungiwa nyimbo za wasanii limeibuka bungeni na kusababisha kelele za wabunge pande zote.
Hata hivyo Serikali imeendeleza msimamo wake kuwa itaendelea kuzifungia nyimbo hizo ili  kulinda maadili ya nchi huku Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Dk Harrison Mwakyembe akiwatuhumu wabunge kushabikia mambo ilihali wabunge wa mataifa mengine hawafanyi hivyo.
Mbunge wa Viti Maalumu Catherine Magige aliibua sakata hilo wakati akiuliza swali la nyongeza ambapo ametaka kujua ni kwa nini Serikali imekuwa ikiwafungia wasanii na kama kamati ya maudhui imeshindwa kazi yake kwanini inasubiri hadi nyimbo zitoke.
Waziri Mwakyembe amesema Serikali haina vita na wasanii bali kinachofanyika ni kulinda utamaduni wa Mtanzania ili taifa lisiwe kokoro la kila mmoja.
Amesema baadhi ya mataifa yanafanya kazi kwa umakini katika kuangalia kazi za wasanii wao na baadhi wanafungiwa.

Dk Mwakyembe ametolea mfano wa wasanii kutoka Nigeria na Marekani pamoja na mkongwe Koffi Olomide ambao hivi karibuni baadhi ya nyimbo zao zilifungiwa.
Nyimbo ambazo zilifungiwa ni pamoja na Pale kati Patamu na Maku Makuz zilizoimbwa na Ney wa Mitego, kibamia wa Roma Mkatoliki,
Wimbo wa Amani Hamisi maarufu kama Manifango wa Hainaga Ushemeji pia umefungiwa, sawa na I am Sorry JK wake Nikki Mbishi.
Nyimbo nyingine ni Tema mate tumchape (Hamad Ali maarufu Madee), Uzuri Wako (Juma Mussa Mpolopoto maarufu Jux), Nampa Papa (Gift Stanford maarufu Gigy Money) na Nampaga (Barnaba Elias maarufu Barnaba).
Nyimbo za Diamond, ambaye jina lake halisi ni Nasib Abdul, zilizofungiwa ni Hallelujah (aliomshirikisha Morgan Heritage ) na Waka Waka (aliomshirikisha Rick Ross).

No comments:

Post a Comment