Saturday, March 3

Watoto wanne waliofariki kwa kuungua ndani ya nyumba, wazikwa

Sengerema. Mamia ya wakazi wa mji wa Sengerema jana wamejitokeza kwa wingi kushiriki mazishi ya watoto wanne wa familia moja waliofariki dunia kwa kuungua kwa moto.
Akizungumza wakati wa mazishi hayo leo Machi, 3 Diwani wa Kata ya Nyatukala, Salehe Msaba amesema tukio hilo limeleta simanzi na majonzi kwa familia na jamii nzima hivyo ni vema jamii kushikama pamoja na kuisaidia familia hiyo.
“Tunapaswa kumshukuru Mungu kwa mapenzi yake kwani kila jambo hupangwa na yeye, lakini pia tunapaswa kuwa wamoja na kuondoa makundi yanayoweza kutugawa,” amesema Msaba.
Amesema kutokana na tatizo hilo, mbunge wa jimbo la Sengerema, William Ngeleja ametuma rambirambi ya Sh100, 000 kwa familia iliyopatwa na msiba huo.
Mkazi wa Kata ya Nyatukala, Juma Kalunde amesema wazazi wote tunapaswa kuwa makini katika kutumia nishati yoyote na wakati wa kulala tunapaswa kuzima kila kitu kisha kupumzika.
Amesema vifo vya watoto hawa vimetokea kwa uzembe uliofanywa na dada yao aliyewafungia mlango kwa nje kuondoka na baada ya hapo mshumaa ulishika kwenye neti na kusababisha moto huo.
Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Sengerema, Marco Makoye amezitaka jamii kuwa makini wakati wakitumia nishati  yoyote ya umeme au kuni .
Tukio hilo lilitokea Februari 28, Saa 5:00 usiku, watoto wanne Lydia Elias (10), Modesta Elias (9), Steven Deogratias (9) na Kizengele Elias (8) waliungulia ndani na wamezikwa katika makaburi ya Twitange wilayani Sengerema.

No comments:

Post a Comment