Monday, March 12

Mazungumzo kati ya Serikali, Airtel yaanza

Dar es Salaam. Mazungumzo kati Serikali na kampuni ya Bharti Airtel inayomiliki hisa katika kampuni ya simu za mkononi ya Airtel Tanzania yameanza leo Machi 12, 2018.
Mazungumzo hayo yanalenga kutafuta suluhu ya mmiliki halali wa kampuni ya Airtel ambayo ni ya tatu kwa ukubwa nchini.
Katika mazungumzo hayo yanayofanyika jijini Dar es Salaam, Serikali inawakilishwa na mwenyekiti wa kamati maalumu iliyoundwa na Rais John Magufuli ambaye pia ni Waziri wa Katiba na Sheria, Profesa Palamagamba Kabudi.
Upande wa Bharti Airtel unawakilishwa na mwanasheria mkuu wake, Mukesh Bhavnani.
Taarifa iliyotolewa na Naibu Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Jaffar Haniu leo Machi 12, 2018 imesema mazungumzo hayo yana lengo la kufikia makubaliano yatakayokuwa na tija kwa pande zote mbili na kuimarisha sekta ya mawasiliano Tanzania. 
Desemba mwaka jana uliibuka utata kuhusu mmiliki halali wa Airtel, Serikali ikisema ndiyo mmiliki halali kwa sababu ubinafsishwaji wa kampuni hiyo haukufuata utaratibu madai ambayo yalikanushwa na Bharti Airtel.

No comments:

Post a Comment