Friday, December 1

Ajira 200,000 kutolewa


Arusha. Shirika lisilokua la Kiserikali  la Hand in Hand Eastern Afrika  linatarajia kutengeneza ajira 200,000 kwa miaka mitano katika kipindi cha mwaka 2018 hadi 2022 kwa kuwezesha vikundi vya uzalishaji kufungua biashara mpya pamoja na kuziendeleza zilizopo .
Mpango huo utafanyika kwa kushirikisha wadau mbalimbali ikiwemo serikali na taasisi binafsi kwa kuhakikisha kuwa vikundi vya uzalishaji vinawezeshwa na kupatiwa mikopo ili kupanua wigo  utakaosababisha ongezeko la ajira nchini.
Ofisa Mkuu wa Shirika hilo Afrika Mashariki, Albert Wambugu amesema leo Desemba mosi  kuwa wamekua wakitoa mafunzo katika vikundi vya uzalishaji juu ya kuanzisha biashara mpya ,kuboresha ambazo tayari zimeanzishwa pamoja na jinsi ya kujiwekea akiba na kuwekeza.
Ofisa Maendeleo ya Jamii mkoa wa Arusha, Blandina Nkini amesema kuwa serikali imekua ikitoa mikopo kwa wanawake na vijana ili kupunguza tatizo la ajira kwa kuhamasisha watu kujikita katika shughuli za uzalishaji mali na kujiajiri.
“Taasisi binafsi zinapaswa kushirikiana  na serikali kuangalia ni jinsi gani tunaweza kuondoa umasikini miongoni mwa vijana wengi kwa kuwapa stadi za kazi na kuwaongezea mitaji kwenye biashara ambazo zimeshaanzishwa sanjari na kuwawezesha kupata masoko” amesema Nkini
Amesema wakati nchi  inaelekea kwenye uchumi wa viwanda ,wanawake na vijana wanapaswa kuwa mstari wa mbele katika kuzalisha mali ghafi za viwanda pamoja na wao wenyewe kuanzisha viwanda.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Kenyatta ambaye pia ni Katibu Mtendaji wa Shirika hilo, Catherine Ndungo amesema malengo ya kuanzishwa shirika  hilo ni kuwasaidia watu wenye kipato cha chini ya dola moja kwa siku ambayo ni sawa na Sh2,000 kupatiwa kuwapatia mbinu za kuwawezesha kujikwamua kiuchumi.

No comments:

Post a Comment