Friday, November 17

Wakurugenzi wawili ndugu walivyopoteza maisha ajali ya ndege Ngorongoro

Maofisa wa vyombo vya usalama wakikagua mabaki
Maofisa wa vyombo vya usalama wakikagua mabaki ya Ndege iliyoanguka juzi eneo la Empakai ndani ya Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro mkoani Arusha. Picha na Mussa Juma 
Ngorongoro. Ajali ya ndege ya kampuni ya Coastal Aviation iliyotokea juzi na kuua watu 11, imepoteza maisha ya wakurugenzi wawili wa kampuni maarufu ya utalii mkoani Arusha, Masai Wandering, Nassibu Mfinanga na Shatri Mfinanga.
Ndege hiyo yenye namba 5H-EGG aina ya Cessna Grand Caravan ilianguka baada ya kugonga kingo za Kreta ya Empakai umbali wa mita 3,250 kutoka usawa wa bahari ikitoka mkoani Kilimanjaro kwenda Hifadhi ya Serengeti kutokana na ukungu uliokuwa umetanda katika eneo hilo.
Wakurugenzi hao pamoja na mkuu wa idara ya kompyuta wa kampuni hiyo, Gift Lema walikuwa wakielekea Hifadhi ya Serengeti ambapo wanamiliki kambi za watalii kwa ajili ya kupiga picha ili kuboresha mtandao intaneti wa kampuni hiyo.
Wengine waliofariki ni pamoja na Joyce Mkama mfanyakazi wa Hoteli ya Serena, Simion Kombe ambaye ni mfanyakazi wa kampuni ya Mount Kilimanjaro na Moses Maina aliyekuwa mfanyakazi wa Hoteli ya Andbeyond.
Waliofariki wengine ni Mfalala Siyabonga aliyekuwa akifanyakazi Hoteli ya Bilila Serengeti na watalii Steinert Alexis, Lickttgen Katharina, Kauser Anita na Beranek Hubert.
Walifanya sherehe kabla
Akizungumza katika eneo la ajali, mpwa wa Nassibu, Rick Thomas alisema kabla ya safari hiyo Novemba 11, wakurugenzi hao walifanya sherehe maalumu ya kila mwaka na wafanyakazi wote na wageni iliyokwenda sambamba na kuchangia vituo vya watoto yatima jijini Arusha. Thomas alisema kampuni ya Masai Wondering inavilea vituo vya watoto yatima zaidi ya 10 katika mikoa ya Arusha na Manyara ambapo katika sherehe hiyo iliyopewa jina la ‘Asante Afrika’ kila tiketi iliuzwa Sh100,000.
Mfanyakazi mwingine wa kampuni hiyo, Mubarak Mkwepu alisema katika sherehe hiyo zaidi ya Sh15 milioni zilipatikana.
Alisema kuwa Nassibu ameacha mke na watoto wawili.
Ajali ilivyotokea
Kabla ya kuanguka ndege hiyo ilizunguka juu na kumwaga mafuta.
Mashuhuda waliozungumza na gazeti hili walisema kabla ya kuanguka ilizunguka angani kwa zaidi ya nusu saa katika eneo la milima ya bonde la Empakai ndani ya Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro. Lunda Mollel na Lengio Kilembi ambao ni wakazi wa Kijiji cha Sendiu walisema wakiwa machungani waliiona ndege hiyo ikizunguka juu na baadaye kuanguka.
Hata hivyo, walisema walianza kutilia shaka baada ya kuona inachukua muda mrefu na baadaye kurejea eneo la Kreta ya Empakai kwa kasi na kisha kugonga mlima na kuanguka.
Kilembi alisema wakati ndege hiyo ikiwa juu inazunguka waliona ikimwaga mafuta, jambo ambalo liliwashangaza. “Nadhani yule rubani alishindwa kutoka katikati ya milima kutokana na ukungu na ndipo alishindwa kuidhibiti ndege na kuanguka,” alisema Mollel.
Hata hivyo, alisema washindwa kwenda katika eneo hilo kutokana na umbali, lakini majira ya saa 10 jioni ndipo walianza kuona magari yakienda na wao walikwenda na kukuta watu 11 wakiwa wamefariki dunia. Kamanda wa polisi Mkoa wa Arusha, Charles Mkumbo alisema jeshi hilo kwa kushirikiana na mamlaka nyingine ikiwamo ya anga wanaendelea na uchunguzi wa ajali hiyo.
“Uchunguzi umeanza kujua chanzo na tayari kisanduku maalumu cha mawasiliano kimechukuliwa na wataalamu waliofika mara tu baada ya ajali,” alisema.
Hiyo ni ajali ya pili kutokea ikihusisha ndege za Coastal Aviation kwani wiki mbili zilizopita ndege nyingine ya kampuni hiyo iliangika katika eneo la Lobo Serengeti na kujeruhi watu wanne.

No comments:

Post a Comment