Friday, November 17

Duce walia na deni la Sh700 milioni

Mwenyekiti wa Bodi ya Usimamizi Duce, Profesa
Mwenyekiti wa Bodi ya Usimamizi Duce, Profesa Rwekaza Mukandala 
Dar es Salaam. Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam (Duce) kinakabiliwa na deni la Sh700 milioni, lililotokana na mkopo uliotolewa na Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HESLB) ikiwa ni gharama za kusomesha wanataaluma.
Rais wa chuo hicho, Profesa William Anangisye alisema hayo kwenye mahafali ya kumi ya Duce jijini Dar es Salaam.
Alisema ili kukabiliana na madeni kutoka bodi hiyo, chuo kimeanzisha utaratibu wa kuwachuja wanataaluma wanaoomba kusomeshwa na bodi.
“Tumeanzisha uhusiano na vyuo rafiki nje ya nchi ili vitusaidie kusomesha wanataaluma hawa,” alisema.
Anangisye alifafanua kuwa huu ni wakati wa wanataaluma kutafuta ufadhili kutoka taasisi nyingine za kimataifa zinazotoa ufadhili ili wasomeshwe.
Alisema wanatumia fedha nyingi kuwalipa wahadhiri wa muda chuoni hasa katika masomo ya Fizikia, Hisabati, na Infomatiki.
“Hii ni changamoto kwetu, hata hivyo tumeanzisha utaratibu wa kuandaa mpango wa usomeshaji wa wafanyakazi uitwao Staff Training Plan utaowezesha chuo kutathmini mahitaji ya usomeshaji,” alisema.
Pia, alifafanua kuwa chuo kinakabiliwa na uhaba wa mabweni na kwamba wanafunzi 4,888 kati ya 5,300 wamekosa nafasi za mabweni na kuishi katika vyumba vya kupanga.
Mwenyekiti wa Bodi ya Usimamizi Duce, Profesa Rwekaza Mukandala aliwataka wahitimu kuacha kujenga mazoea ya kuajiriwa na badala yake watengeneze mazingira ya kujiajiri wenyewe ili kukabiliana na changamoto ya mrundikano wa wahitimu wasio na kazi mtaani.
“Mimi nasisitiza tu kuwa ni vizuri kwa wahitimu kufikiria kuajiriwa nje ya Serikali au sekta rasmi pekee,” alisema.
Alisema tatizo la wahitimu kutegemea ajira lipo katika nchi nyingi za Afrika na dunia kwa jumla, hivyo chuo kimeona ipo haja ya kuongeza mkazo katika elimu ya ujasiriamali ili kuwajengea uwezo wa kujiajiri.
“Kwa idadi hii, leo tunategemea mtafanya kazi kwa bidii na nidhamu, na kwa wale watakaoenda kuwa wajasiriamali mna mchango pia katika jitihada za kuwezesha mikakati ya kitaifa ya kuleta maendeleo ya viwanda na uchumi wa kati,” alisema.
Mkuu wa chuo hicho, Jakaya Kikwete aliwatunuku wahitimu 1,443 shahada za fani mbalimbali.

No comments:

Post a Comment