Wednesday, October 11

UN yafichuwa mkakati wa majeshi ya Myanmar kufuta athari za Waislam wa Rohingya

Mtoto anapewa chanjo katika kambi ya wakimbizi ya Waislam wa Rohingya
Umoja wa Mataifa imesema kuwa uvunjifu wa amani unaoendelea magharibi ya Jimbo la Rakhine, Myanmar ni sehemu ya kampeni iliyoandaliwa na kuratibiwa na majeshi ya serikali ili kuhakikisha inawaondosha kabisa Waislam wa Rohingya katika eneo hilo.
Ripoti iliyotolewa Jumatano huko Geneva na ofisi ya haki za binadamu ya UNimewatuhumu wanajeshi wa Myanmar, wakisaidiwa na makundi ya wanajeshi wakibudha wenye silaha, kwamba siyo tu wameshambulia majumba ya Waislam wa Rohingya na vijiji vyao lakini pia wamekuwa wakijaribu “kuondoa kabisa alama na kumbukumbu zote za watu hao katika ardhi yao” huko eneo la Rohingya ili kufanya watu hao wasiweze kuwepo kabisa katika nchi hiyo.

Zaidi ya wakimbizi nusu milioni wamekimbia Myanmar kuelekea eneo la Bangladesh Cox Bazar tangu Agosti 25, wakati mashambulizi katika vituo vya usalama yalipofanywa na wapiganajiwa Rohingya na kusababisha majeshi ya Myanmar kutumia nguvu kupita kiasi kupambana nao. Lakini ripoti ya UN iliyokuwa imejikita katika mahojiano 65 iliyofanya na mamia ya wakimbizi, imesema kuwa operesheni ya kuwaondosha Waislam wa Rohingya huko eneo la Rakhine ilianza mapema kwa mwezi moja takriban.
Wakimbizi wamewaambia wachunguzi wa UN kwamba hata kabla ya mashambulizi na baada yake, vyombo vya usalama vilitumia vipaza sauti kuwashinikiza Waislam kukimbia eneo hilo na kutafuta hifadhi huko Bangladesh, la sivyo “tutachoma nyumba zenu na kuwaua.” Pia Waislam wa Rohingya wameeleza visa vilivyofanywa na vyombo vya usalama ikiwemo kuwapiga risasi wanavijiji na ubakaji wa makundi kwa wasichana wadogo chini ya miaka mitano yaliofanywa na askari wasio na magwanda.
Mkuu wa haki za binadamu UN Zeid Ra’ad al-Hussein siku za nyuma ameelezea vitendo viovu dhidi ya watu wa Rohingyas“ni somo la mfano wa mauaji ya halaiki.”
Maafisa wa Myanmar hawakuwa na maelezo mara moja dhidi ya ripoti hiyo mpya ya UN.
Watu wa Rohingya wasiokuwa na utaifa kwa muda mrefu wamenyimwa haki zao za msingi katika nchi ya Myanmar yenye mabudhaa walio wengi, ambao wanawachukulia kama wahamiaji kutoka Bangladesh, pamoja na kuwepo ushahidi kuwa familia nyingi za Waislam hao wameishi katika nchi hiyo kwa vizazi vingi.

No comments:

Post a Comment