Sunday, October 1

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII, RAMO MAKANI AFUNGUA KONGAMANO LA MAONESHO YA UTALII YA KARIBU KUSINI.


Baadhi ya Wanafunzi wa Chuo cha Walimu cha Kleruu wakifuatilia maada inayowasilishwa kuhusiana na Mradi wa SPANEST jinsi inavyoshirikisha wananchi katika masuala ya uhifadhi mara baada ya kufunguliwa kwa kongamano la maonesho ya utalii ya Karibu Kusini yanayofanyika kwa mara ya pili mjini Iringa. 
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Eng. Ramo Makani, (katikati) wa pili kulia ni Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Jamhuri David, wa pili kushoto ni Mkuu wa wilaya ya Iringa Richard Kasesela akiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi mara baada ya kufungua kongamano la maonesho ya utalii ya Karibu Kusini yanayofanyika kwa mara ya pili mjini Iringa. (Picha na Lusungu Helela- MNRT)
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Eng. Ramo Makani, (katikati) wa pili kulia ni Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Jamhuri David, wa pili kushoto ni Mkuu wa wilaya ya Iringa Richard Kasesela wakiwa kwenye picha ya pamoja na Sekretarieti ya Waandaji wa kongamano mara baada ya kufungua kongamano la maonesho ya utalii ya Karibu Kusini yanayofanyika kwa mara ya pili mjini Iringa (Picha na Lusungu Helela- MNRT).




Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Eng. Ramo Makani, amefungua kongamano la maonesho ya utalii ya Karibu Kusini yanayofanyika kwa mara ya pili mjini Iringa.

Kongamano hilo limefanyika kwa muda wa siku moja katika Ukumbi wa Chuo cha Walimu wa Kleruu likiwakutanisha wasomi na wahadhiri kutoka vyuo vikuu nchini, wanafunzi pamoja na wadau wa utalii wanaofanya shughuli za kiutalii likiwa na lengo la kutathmini na kuangalia namna mikoa ya Nyanda za Juu Kusini inavyoweza kunufaika kutokana na utajiri wa vivutio vya utalii vilivyopo.

Sambamba na kongamano hilo, maonesho hayo yanaendelea kufanyika hadi Oktoba 2 katika viwanja katika viwanja vya Kichangani yakiwa yamewakutanisha Wajasiriamali wadogo 350 kutoka kona zote za mikoa hiyo.Akizindua Kongamano hilo Naibu Waziri Makani amewataka wananchi kuanza kuutupia macho utalii wa nje ya hifadhi kwa kuwa watalii wengi kwa sasa hawaji kuangalii wanyamapori pekee.

Amesema watalii wa siku hizi wamechoka kuangalia wanyamapori wanataka kujifunza kuhusu utamaduni wetu pamoja na vyakula vyetu vya kiasili.Mbali na kuwa na utajiri wa makabila tofauti tofauti, Makani alisema Nyanda za juu Kusini imejaliwa kuwa na vivutio vya Malikale ambayo bado havijatangazwa vya kutosha.

Naye, Mkurugenzi wa Idara ya Utalii, Philip Chitaunga alisema Iringa inasifika kwa kuzalisha wataalamu wa tasnia ya utalii kutokana na uwepo wa chuo Kikuu cha Tumaini kuwa ndo chuo cha kwanza kutoa shahada ya Utalii lakini imekuwa nyuma kiutalii akitolea mfano wa hoteli zinazojengwa ni za chini ya kiwango licha ya watalaam kuwepo.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Iringa, David Jamhuri alisema mkoa umejipanga kuhakikisha kuwa fursa za utalii kwa mikoa ya Nyanda za juu Kusini zinafunguka kwa kuhakikisha kuwa wananchi wanakuwa wa kwanza kunufaika kutokana namipango waliyojiwekea

Pia aliwataka viongozi wa Kiserikali kila wanapopata nafasi ya kuzungumza na wananchi watumie fursa hiyo kutoa elimu kuhusu umuhimu wa kutembelea vivutio vya utalii vilivyopo nchini.

Muongoza watalii wa Kampuni ya Chabo Tours, Serafino Liduino aliitaka Serikali kuanza kuona umuhimu wa kutoa mafunzo mashukeni ili kutengeneza kizazi kinachojua thamani ya kuhifadhi mazingira ili vivutio asilia viendelee kuwepo kutokana na tishio la mabadiliko ya tabia ya nchi yanajitokeza kwa sasa.

No comments:

Post a Comment