Monday, October 2

Makinda ajipa malengo makubwa NHIF


Mwenyekiti wa Bodi ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), Anne Makinda amesema katika uongozi wake anamuomba Mungu kufikisha asilimia 80 ya Watanzania waliojiunga na bima ya afya itakayowasaidia kupata unafuu wa matibabu.
Makinda, ambaye ni Spika mstaafu wa Bunge la Kumi, alitoa kauli hiyo juzi wakati mahafali ya tano ya kidato cha nne ya Sekondari ya Wasichana Luther iliyopo Mapinga Wilaya ya Bagamoyo, mkoani Pwani.
NHIF imepanga kuwafikia asilimia 85 ya Watanzania ifikapo mwaka 2020.
Alisema bima ndiyo msemo wa mjini kwa sababu hospitali kwa sasa kitu cha kwanza utakachoulizwa ni bima ya afya.
“Suala la bima sasa hivi si la kujifikiria ndugu zangu. Katika hali ya kawaida unasema hauna fedha lakini fedha ni nini katika kifo, Zipo bima za afya za aina nyingi naomba mjiunge,” alisema Makinda aliyeteuliwa na Rais John Magufuli kuongoza bodi hiyo Mei mwaka jana.
Makinda alisema suala la bima ni tatizo kila hospitali; za Serikali au binafsi na kwamba ingawa hali siyo nzuri, ni bora kila mtu awe na bima ili kujihakikishia kupata huduma za afya wakati wote.
Awali, Mkuu wa shule hiyo, Salvatory Mworia alisema wanafunzi 24 wanatarajia kuhitimu kidato cha nne na kwamba, shule imekuwa na historia ya kufanya vizuri katika mitihani ya Taifa.
“Changamoto kubwa tuliokuwa nayo ni ubovu wa barabara unaosababishwa na malori yanayokwenda kubeba chumvi. Hali hii inasababisha usumbufu kwa wapita njia hasa nyakati za mvua,” alisema Mworia.

No comments:

Post a Comment