Saturday, October 28

Mvua yaua wengine wawili


Kibaha. Miili ya watu wawili akiwemo mgambo imeopolewa  baada ya kuzama maji kufuatia mvua zinazoendelea kunyesha  maeneo mbalimbali.
Miili hiyo imeopolewa  saa  saba mchana  Oktoba 27 mjini Kibaha  kwenye mto Kiluvya na imetambulika ni ya Issa Ally (28) askari mgambo na Saimon Ramadhani (27).
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoani Pwani Blasilus Chatanda amesema leo kwamba mgambo huyo alikuwa  akijaribu kumuokoa mtoto  aliyetaka kusombwa na maji kutokana na mvua hiyo.
Amesema mgambo huyo amejitahidi kadri ya uwezo wake kuokoa maisha ya mtoto huyo ambaye hata hivyo hajaonekana mpaka leo.
Kamanda Chatanda amesema kwamba mwili wa mgambo huyo umeonekana baada ya maji kupungua.
Kamanda Chatanda amesema kwamba Ramadhani ambaye ni mkazi wa Muheza kata ya Pangani mjini Kibaha na alisombwa na maji wakati akijaribu kuvuka mto Mpiji. 
"Kama mnavyojua mvua imeendelea kunyesha sehemu mbalimbali mito imejaa maji, sasa inaonekana huyu naye aliyapuuza maji hayana kasi kubwa akawa anavuka yakamshinda nguvu yakamsomba na kusababisha kifo"amesema Chatanda.
Kaimu Kamanda huyo ameongeza kuwa miili hiyo imepelekwa kuhifadhiwa katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Pwani Tumbi kusubiri uchunguzi wa daktari.

No comments:

Post a Comment