Friday, October 13

Mkuu wa Mkoa Akemea vikao kudorora

MKUU WA MKOA WA RUKWA, ZELOTE STEVEN.

MKUU wa Mkoa wa Rukwa, Zelote Steven ameagiza kuanza kufanyika vikao vya kamati za maendeleo za wilaya (DCC) kwa kuwa vimekuwa havifanyiki kwa muda mrefu hali inayonyima fursa ya kupata ushuru mzuri kutoka ngazi ya wilaya.

Akifungua kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Rukwa (RCC) alisema kwa muda mrefu vikao hivyo havijafanyika kwa kisingizio cha kutokuwa na posho, kitu ambacho si sahihi.

Zelothe alisema kwa ngazi ya mkoa, kikao hicho kimekuwa kikifanyika bila posho, lakini cha kushangaza kwa ngazi ya wilaya vikao kama hivyo havifanyiki.

"Naagiza kuanzia sasa ni lazima vikao hivyo vifanyike. Posho ya kikao isiwe kigezo mbona vikao vya RCC vinafanyika na kama hakuna posho, tunalipa pindi zinapopatikana. Sitaki kusikia kuwa hamfanyi vikao vya DCC kwa madai kakuna posho," alisema.

Aliwasihi watumishi wa umma kuongeza kasi katika kuwatumikia wananchi kwa sababu dunia hivi sasa imebadilika hivyo “lazima tukimbie kwa sababu mkoa wa Rukwa unahitaji maendeleo kwa kasi kubwa”.

Katika kikao hicho, mmoja wa wajumbe waalikwa, Zeno Nkoswe, alipendekeza kuwa umefika wakati sheria iliyoanzisha vikao hivyo itazamwe upya, ili uwakilishi uongezwe kwa kuwa wajumbe halali ni 28 ambao wanawakilisha zaidi ya wakazi milioni moja wa mkoa huo.

Nkoswe alisema kutokana na zama za sasa, ni vyema idadi ya wajumbe wa kikao hicho ikaongezeka kwa uwakilishi, tofauti na sasa kwa sababu walio wengi ni waalikwa na iko siku wanaweza wasihudhurie kwa vile hawabanwi na sheria.

No comments:

Post a Comment