Monday, October 2

Jimbo la Sugu ‘lawapasua’ kichwa CCM Mbeya


Mbeya. Chama cha Mapinduzi (CCM) Mbeya Mjini kimesema safu ya viongozi wa jumuiya za chama hicho zilizofanyika mwishoni mwa mwezi uliopita zitawasaidia kurudisha jimbo la Mbeya Mjini na halmashauri mikononi mwake katika Uchaguzi Mkuu wa 2020.
Katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, CCM Mbeya Mjini ilishindwa kumng’oa mbunge wa jimbo hilo,   Joseph Mbilinyi 'Sugu’ (Chadema) lakini ilijikuta ikipoteza viti vingi vya udiwani jambo lililofanya Chadema kunyakuwa na halmashauri ya jiji hilo baada ya Chadema kuwa na viti 26 vya udiwani na CCM kumi.
Kwa nyakati tofauti viongozi waandamizi wa CCM Mbeya Mjini wamesema   mfumo wa uchaguziulioanzishwa sasa na chama hicho unaondoa msuguano na makundi yanayojenga fitina, majungu na usaliti tofauti na hapo awali.
Katibu wa Umoja wa Wazazi-CCM Wilaya ya Mbeya, Sadick Kadulo amesema   kwa sasa CCM ipo makini katika chaguzi zake lengo ni kuona inakuwa na viongozi wenye uwezo wa kukisaidia chama kukomboa jimbo na halmashauri.
“Mapinduzi haya ya kimuundo ndani ya chama chetu yana tija sana tofuati na huko nyuma kwani wakati ule ilikuwa rahisi sana wagombea kucheza rafu  ndani na nje ya chama, na hii ndio iliyotufanya tupoteze jimbo kwa mara ya pili lakini kubwa zaidi tukapoteza halmashauri,”

“Lakini naamini hii safu tuliyoipata katika jumuiya zote za CCM ni makini na imara kutokana na mfumo wake, hivyo katika chaguzi za Serikali za Mitaa mwaka 2019 tutashinda kwa kishindo lakini pia 2020 tutakomboa jimbo na halmashauri pia,” amesema Kadulo.
Akiwa wilayani Mbarali, Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Mbeya, Dk Mary Mwanjelwa amewaambia wafuasi wa CCM kwamba chuki, ubinafsi, usaliti na fitina ndizo zinazokiumiza chama chake Mbeya Mjini na kusababisha kuanguka katika chaguzi zake tofauti na wilaya nyingine za mkoa huo.
“Mimi ni Mbunge wa Viti Maalumu mkoa mzima wa Mbeya, nina wilaya sita, lakini sijaona mbunge kama mbunge wa Mbarali (Haroon Pirmohamed) na hili nalizingumza bila kumung’unya maneno, Mbarali tumepata mbunge ambaye ni lulu tumtumie’.
Hata hivyo amesema jimbo la Mbeya Mjini ndio kioo cha mkoa mzima wa Mbeya hivyo ni aibu kuona upinzani ndio unaotawala kuanzia ubunge hadi halmashauri, hivyo anaamini katika safu za viongozi wapya waliopatikana hawataendekeza makundi ambayo huwa yanawagharimu siku za uchaguzi, badala yake watakuwa kitu kimoja.

No comments:

Post a Comment