Friday, September 22

Raia wa kigeni aeleza pasipoti yake ilivyochanwa na polisi

Dar es Salaam. Raia wa Uholanzi, Monique Amanzi (28) amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na shtaka la kuishi nchini bila kuwa na viza, huku yeye akidai pasipoti yake ilichanwa na askari aliyekuwa na uhusiano naye kimapenzi.
Mwendesha Mashtaka wa Uhamiaji, Novatus Mlay amedai mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Victoria Nongwa kuwa Septemba 11 katika ofisi ya makao makuu ya Uhamiaji, Kurasini wilayani Temeke alibainika kuishi nchini bila kuwa na viza kinyume cha sheria.
Baada ya kusomewa mashtaka leo Ijumaa, mshtakiwa amedai rafiki yake wa kiume ambaye ni polisi wa kitengo cha usalama barabarani, Letiko Kurwa alichana hati yake ya kusafiria.
Baada ya hati yake kuchanwa, ameeleza aliripoti polisi Kinondoni miaka miwili iliyopita lakini alipoteza namba ya taarifa ya polisi (RB).
Mshtakiwa ameeleza alipoingia nchini alikuja na mtoto mmoja Ibrahimu Abas na kwamba, alizaa mtoto mmoja na askari huyo ambaye alifariki dunia.
Ameeleza kwamba wametengana na askari huyo na kwamba, alishawahi kwenda uhamiaji lakini hakupata mafanikio.
Baada ya kutoa maelezo hayo, mshtakiwa alitakiwa kuwa na wadhamini wawili raia wa Tanzania, ambao kila mmoja atasaini bondi ya Sh1 milioni.
Upande wa mashtaka umedai upelelezi haujakamilika na Hakimu Nongwa aliahirisha kesi hiyo hadi Septemba 27 kwa ajili ya kutajwa.

No comments:

Post a Comment