Thursday, August 3

Uhamiaji wamsafisha mgombea TFF

Msemaji Mkuu Idara ya Uhamiaji, Ally Mtanda

Msemaji Mkuu Idara ya Uhamiaji, Ally Mtanda akifafanua swala hilo mbele ya wanahabari mapema leo Jijini Dar es salaam 
Idara ya Uhamiaji imetoa ufafanuzi kuhusu uraia wa mgombea wa urais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Wallace Karia na kuthibitisha kuwa ni MTanzania.
Karia aliwekewa pingamizi na mmoja wa wagombea wa nafasi hiyo kwa hoja ya kutilia shaka uraia wake.
Msemaji Mkuu wa Idara ya Uhamiaji, Ally Mtanda amesema ofisi yake imechunguza na kuthibitisha kuwa Karia alizaliwa nchini na mama yake ni Mtanzania.
Hata hivyo, Mtanda amesema kuwa ni kweli kuwa Karia baba yake ni msomali na alikuwa pia na uraia wa Somalia lakini alishaukana.
"Kwa msingi huo, Karia ni raia wa Tanzania kwa kuzaliwa chini ya kifungu cha 5(1) na (2) cha sheria ya uraia. Na wakati huo huo akiwa raia wa Somalia wa kurithi.
"Ni hitaji la kisheria chini ya kifungu cha 7(1), pale mtu anapokuwa na uraia wa nchi mbili kuukana uraia mmoja pale anapofikisha miaka 18, hatua ambayo Karia alitekeleza na kuthibitishwa," amesema Mtanda.

No comments:

Post a Comment