Sunday, August 13

Uchaguzi Kenya: Kofi Annan amtaka Odinga kutumia njia za kisheria

Kofi Annan

Image captionKofi Annan alikuwa mpatanishi mkuu mzozo wa baada ya uchaguzi Kenya mwaka 2007
Katibu mkuu wa zamani wa Umoja wa Mataifa Kofi Annan, ambaye alikuwa mpatanishi mkuu baada ya mzozo wa kisiasa nchini Kenya miaka kumi iliyopita, ametoa wito kwa walioshindwa kutumia mifumo ya kisheria kutafuta haki.
Bw Annan alikuwa mpatanishi mkuu baada ya ghasia kuzuka baada ya uchaguzi mkuu wa 2007 uliokumbwa na utata.
Bw Mwai Kibaki alitangazwa mshindi wakati huo lakini Bw Raila Odinga na chama chake cha ODM wakapinga matokeo hayo.
Katibu mkuu huyo wa zamani wa UN amempongeza Bw Kenyatta kwa ushindi wake na pia akamsifu Bw Odinga kwa kuendesha kampeni yake kwa njia ya amani.
"Namshukuru kiongozi wa upinzani Raila Odinga kwa kampeni ya uchaguzi ya amani aliyoiendesha. Amekuwa mtetezi jasiri wa demokrasia," amesema Dkt Annan kupitia taarifa.
"Kwa hivyo, namhimiza sasa afuatilie malalamiko yake kupitia mifumo ya kisheria iliyowekwa na aweke maslahi ya taifa mbele, kama alivyofanya kwa uzalendo mara nyingi awali."
Upinzani umekuwa ukidai mitambo ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (IEBC) ilidukuliwa na matokeo kuchakachuliwa kumfaa Rais Kenyatta.
Alhamisi, muungano wa upinzani National Super Alliance (NASA) ulidai Bw Odinga ndiye aliyeshinda uchaguzi huo na kuitaka tume hiyo kumtangaza kuwa mshindi.
Rais Kenyatta alipata kura 8, 203, 290 ambayo ni asilimia 54.27 naye mpinzani wake mkuu, mgombea wa muungano wa upinzani wa National Super Alliance Raila Odinga akapata kura milioni 6,762,224 ambayo ni asilimia 44.74.
Maajenti wakuu wa NASA waliondoka ghafla kikao cha tume hiyo cha kuafikiana kuhusu matokeo hayo kabla ya kutangazwa kwa Bw Kenyatta kuwa mshindi wa uchaguzi huo Ijumaa usiku.
Naibu ajenti mkuu wa muungano huo James Orengo, amesema muungano huo hautaenda kortini. Amesema hawana imani na idara ya mahakama kwamba itashughulikia malalamiko yao kwa njia ya haki bila mapendeleo.
Bw Annan pia ametoa wito kwa Rais Kenyatta, ambaye alitangazwa mshindi wa urais Ijumaa afanye juhudi kuunganisha tena taifa.
Kiongozi huyo amesikitishwa na mauaji ambayo yametokea kwenye makabiliano kati ya waandamanaji waliokuwa wanapinga matokeo na polisi.
Amesema anatumai hakutatokea mauaji zaidi.
"Amani, uthabiti na ustawi vinategemea viongozi wa kisiasa Kenya. Wanafaa kuwa makini sana katika mambo wanayosema na vitendo vyao katika hali hii ya sasa. Nawaomba wawajibike."
Naibu rais na mwakilishi mkuu wa Umoja wa Ulaya Federica Mogherini pia ameutaka upinzani kutumia njia za kisheria kufuatilia malalamiko yao kuhusu uchaguzi.
Uhuru Kenyatta kushoto) na Mpinzani wake Raila Odinga (kulia)
Image captionUhuru Kenyatta kushoto) na Mpinzani wake Raila Odinga (kulia)
"Sawa na ulivyofanya Umoja wa Afrika, Umoja wa Ulaya unatarajia upinzani uheshimu matokeo na ktuumia njia za kisheria zilizopo kukata rufaa na kuwasilisha malalamiko," amesema kupitia taarifa.
Polisi walikabiliana na wafuasi wa upinzani katika mitaa ya Mathare na Kibera jijini Nairobi, katika katika maeneo ya Homa Bay, Migori na Kisumu ambayo ni ngome ya Bw Odinga magharibi mwa Kenya.
Mwanamke akijikinga KiberaHaki miliki ya pichaREUTERS
Image captionGhasia zilitokea pia mtaa wa Kibera, Nairobi
Mashirika ya kutetea haki yanasema watu kadha wameuawa kwa kupigwa risasi na wengine wengi wanauguza majeraha hospitalini.
MathareHaki miliki ya pichaEPA
Image captionWafuasi wa upinzani wamekuwa wakikabiliana na polisi mtaa wa Mathare na Kibera jijini Nairobi na eneo la Kisumu
Tume ya Kitaifa la Haki za Kibinadamu ilisema idadi ya waliokuwa wameuawa kufikia Jumamosi jioni ilikuwa imefikia 24, ingawa idadi hiyo haijathibitishwa na shirika jingine.
Kamishna wa eneo la Nyanza Wilson Njenga Jumamosi alithibitisha kwamba mtu mmoja alifariki eneo la Maseno kilomita takriban 20 kutoka mji wa Kisumu.
Jumamosi, msichana wa miaka 10 pia alifariki baada ya kupigwa risasi wakati wa makabiliano kati ya waandamanaji na polisi katika mtaa wa Mathare Kaskazini jijini Nairobi.
Serikali imesema hakuna mwandamanaji aliyeuawa na maafisa wa polisi na kwamba polisi hawajatumia risasi halisi kuwakabili waandamanaji.
Mwaka 2007, watu zaidi ya 1,000 walifariki na wengine 600,000 wakafurushwa makwao wakati wa ghasia za kikabila zilizozuka baada ya matokeo ya uchaguzi kutangazwa.

No comments:

Post a Comment