Wednesday, August 30

MBUNGE ULANGA ATOA FEDHA KWA WAHANGA WA AJALI YA BASI


Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Ulanga Mh. Amina Seif na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri Ndg. Yusuf Semuguruka wakimsikiliza mmoja wa majeruhi wa ajali ya basi la Mfundo iliyotokea katika Mlima Ndororo hivi karibuni.
Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Ulanga Mh. Amina Seif akimkabidhi Mganga Mkuu wa Wilaya fedha zilizochangwa na Waheshimiwa Madiwani wa kamati ya Fedha, Utawala na Mipango na Wakuu wa Idara kwa ajili ya kulipia gharama za matibabu yaliyotolewa kwa majeruhi wa ajali ya basi la Mfundo.

Na Sekela Mwasubila – Afisa Habari

Mbunge wa Ulanga Mh. Goodluck Mlinga ametoa kiasi cha shilingi milioni tano na laki tano kwa ajili ya kuwafariji majeruhi  na wafiwa wa ajali ya basi la Mfundo iliyotokea hivi karibuni katika mlima Ndororo.

Fedha hizo zilikabidhiwa kwa Mkuu wa Wilaya ya Ulanga Jacob Kassema ambaye ni mwenyekiti wa kamati ya maafa wilaya ili awasilishe kwa walengwa ikiwa kwa ajili ya kuwapa pole familia za waliopoteza maisha na majeruhi  wa ajali hiyo.

Akipikea fedha hizo Mkuu wa Wilaya Ndugu Kassema alimshukuru mbunge kwa msaada alioutoa kwani utawasaidia sana wafiwa na majeruhi na kuwafariji kutokana na kupoteza mali zao katika eneo la ajali.

Wakati huo huo madiwani wa kamati ya fedha, Utawala na Mipango na Idara nao walitoa mkono wa pole kwa wafiwa na majeruhi ambapo mchango huo ulikabidhiwa kwa Mganga Mkuu na Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya Ulanga Mh. Amina Seif na kusema kuwa fedha hiyo imetolewa kwaajili ya kugharamia matibabu ya majeruhi waliopo wodini na waliotibiwa na kuruhusiwa.

Aliongeza kuwa waheshimiwa madiwani wameguswa sana na ajali hiyo na kuona kuwa kuna haja ya kuwasaidia kuwalipia matibabu kwani wengi wao wamepoteza vitu sehemu ya ajali hivyo ingewahuia ugumu wa kulipia matibabu na kuamua kuwachangisha madiwani wa kamati ya fedha na wakuu wa Idara na kufanikiwa kukusanya kiasi cha Tshs. 327,000.

Akipokea fedha hizo Mganga Mkuu wa Hospitali ya Wilaya Dkt. Rajabu Risasi amewashukuru waheshimiwa madiwani kwa msaada huo na kueleza kuwa fedha hiyo itawasaidia katika kufidia madawa yaliyotumika siku ya ajari kwani majeruhi wote walitibiwa bila kujali kama wana fedha za matibabu.

Basi la Mfundo lilipata ajali siku ya alhamisi katika mlima Ndororo na kujeruhi watu thelathini na tatu na kusababisha vifo vya watu saba.

No comments:

Post a Comment