Saturday, March 19

‘Namuunga mkono Mpungwe kuhusu Z’bar’


Dar es Salaam. Ikiwa imebaki siku moja kabla ya Uchaguzi wa Marudio kufanyika Zanzibar, mfanyabiashara maarufu nchini, Hashim Ismail amesema Taifa haliwezi kujidanganya kwamba kila kitu ni shwari visiwani humo.
Alisema hayo jana akiunga mkono kauli ya Balozi Ami Mpungwe aliyoitoa katika mahojiano na gazeti hili wiki hii akisema, Taifa halipaswi kujidanganya kwamba Zanzibar hakuna tatizo. Alisema: “Mtanzania yeyote aliyesoma yale aliyozungumza Ami (Mpungwe) hana budi kumuunga mkono. Pia, mimi nakubaliana naye; kuna shida, hatari kubwa na ufisadi mkubwa wa kisiasa. Na kama alivyosema hatuwezi “ku-pretend everything in the garden is rosy (hatuwezi kujidanganya kwamba kila kitu kilichopo katika bustani ni waridi).
“Lakini kama ilivyo kawaida yetu ya uchwara, woga na kujikomba, yale aliyozungumzia Ami yalienda na gazeti la jana (juzi) na kubaki karatasi tu ya kufungia vitumbua.
“Jambo hili si la ZEC (Tume ya Uchaguzi Zanzibar), CCM na CUF tu, ni suala la haki za binadamu. Linatuhusu sote.”
Mzee Ismail alisema Balozi Mpungwe alipendekeza kurudi kwenye meza ya mazungumzo akisisitiza kwamba ni jambo sahihi kabisa lakini akahoji:
“Uchaguzi unaorudiwa Machi 20 (kesho) chini ya ulinzi mkali wa vyombo vya dola... Unaosusiwa na vyama vingine vya siasa, utakuwa umeshamalizika. Sasa itakuwaje?
Hoja ni kuufuta kwanza kisha turudi katika meza.” Katika mahojiano maalumu na Mwananchi, Mpungwe ambaye ni balozi wa zamani wa Afrika Kusini alihadharisha kuhusu hali ya kisiasa Zanzibar akisema “tusijidanganye kuwa hakuna matatizo” kwenye visiwa hivyo na kutaka ufumbuzi utafutwe kabla haujasababisha madhara.    

No comments:

Post a Comment