Thursday, July 2

Kilio bei mpya ya petroli kila kona.


Zikiwa ni siku mbili zimepita tangu Mamlaka ya Usimamizi wa Nishati na Maji (Ewura), itangaze kuongezeka kwa bei elekezi ya mafuta ya petroli, dizeli na mafuta ya taa, wananachi wengi wameingiwa hofu kwa kuamini kuwa uamuzi huo utawaongezea makali ya maisha maradufu.
 
Juzi mamlaka hiyo ilitangaza ongezeko la bei elekezi ya mafuta na kuonyesha kuwa bei ya petroli imeongezeka kwa Sh. 232 kwa lita, dizeli Sh. 261 na mafuta ya taa Sh. 369. Katika soko la dunia, bei ya mafuta imekuwa ikishuka. Hata hivyo, taarifa ya Ewura ilitaja sababu za kupanda kwa bei ya nishati hiyo nchini kaunzia jana kuwa ni kuporomoka kwa thamani ya Shilingi na pia kuanza kutumika kwa tozo mpya za mafuta zilizopitishwa na bunge la bajeti kwa mwaka wa fedha 2015/2016.
 
Kufuatia mabadiliko hayo, bei ya petroli kwa sasa jijini Dar es Salaam ni Sh. 2,198, dizeli Sh. 2,043 na mafuta ya taa ni Sh.1, 993; Arusha petroli Sh. 2, 282, dizeli Sh. 2, 127, mafuta ya taa Sh. 2, 077 huku maeneo mengine kama Bukoba bei ikiwa juu zaidi kwa petroli kuuzwa Sh. 2,413, dizeli Sh. 2, 258 na mafuta ya taa Sh. 2, 208.
 
TUCTA: BEI HII INAUMIZA WAFANYAKAZI 
Akizungumza na NIPASHE kwa njia ya simu jana,  Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (Tucta), Gratian Mukoba, alisema, wafanyakazi wataumia zaidi kutokana na ongezeko hilo la bei ya mafuta kwani wanahitaji kutumia usafiri kwenda kazini huku wakiwa hawana marupurupu ya usafiri.
 
Mukoba aliongeza kuwa, ongezeko hilo pia litamuathiri mkulima kwa bei ya mazao kupanda kutokana na gharama za usafiri.
 
“Maoni yetu ni kwamba ukiongeza bei ya mafuta, unaongeza matumizi kwa mafanyakazi katika usafiri na chakula. Ni mzigo kwa mfanyakazi ukizingatia hawana ‘allowance ya commuter’ bajeti  ya usafiri,” alisema rais huyo. 
Alisema, serikali ilitakiwa kuangalia kitu kingine ambacho wangeongeza bei kisingeweza kuathiri  moja kwa moja.
 
CHAMATA: ONGEZEKO LIMETUATHIRI MNO
Kwa upande wake, Chama cha Madereva Tanzania, kimesema kuwa ongezeko hilo la bei ni kubwa na hivyo litaahiri madereva na kuwaneemesha wamiliki wa magari yao.
 
Akizungumza na NIPASHE kwa njia ya simu jana, Katibu Mkuu wa chama hicho, Rashid Salehe, alisema, bei hiyo ni kubwa kwani inawaumiza Watanzania wote kwani ndiyo wanaotumia usafiri wa pamoja.
 
“Athari ni kubwa… juzi tu ilikuwa Sh. 1, 900, sasa Sh. 2, 200. Tunaoathirika ni sisi tunaotumia usafiri wa pamoja,” alisema Salehe na kuongeza.
 
Hamad Mohamed, dereva wa daladala inayofanya safari zake kati ya Makumbusho na Posta, jijini Dar es Salaam, alisema, kupanda kwa bei ya mafuta ya petroli kumewaathiri katika biashara hiyo ya usafiri kwani mabosi wao hawaguswi na hilo.
 
DARCOBOA: TUPENI MWEZI MMOJA
Umoja wa Wamiliki wa Mabasi ya Daladala Dar es Salaam (Darcoboa), umesema kwa sasa unasubiri hali itakuwaje baada ya mwezi mmoja kabla ya kutoa maoni yao rasmi kuhusiana na  ongezeko hilo la bei ya mafuta.
 
Mwenyekiti wa umoja huo, Sabri Mabrouk, alisema, athari ni kubwa kwani bei imepanda kwa kishindo tofauti na kipindi cha nyuma ambacho ilikuwa ikipanda kati ya Sh. 50 na Sh. 60.
 
“Tumeshauriana na viongozi wenzangu, tuvumilie mwezi mmoja maana Ewura wana utaratibu wa kutangaza bei elekezi kila mwezi ili baada ya hapo tutoe madai yetu,” alisema mwenyekiti huyo.
 
TRAWU: HALI YA MFANYAKAZI KUWA MBAYA ZAIDI
Kaimu  Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Reli (Trawu) Kanda ya Dar es Salaam, Yasin Mleke, alisema kupanda kwa bei ya mafuta nchini kutaendelea kusababisha maisha ya wafanyakazi na wananchi kwa ujumla kuwa magumu kwa kuwa gharama ya usafiri itaongezeka na  bei ya bidhaa kuwa juu.
 
Aliishauri serikali kudhibiti mfumuko wa bei ili kuboresha maisha ya wafanyakazi na wananchi kwa ujumla.

No comments:

Post a Comment