Tuesday, June 9

KUTANA NA MWANAMKE ALIYETANGAZA NIA



MKURUGENZI Mkuu wa Taasisi ya Taifa ya Utafiti Magonjwa ya Binadamu 
Dk Mwele Malecela 

MKURUGENZI Mkuu wa Taasisi ya Taifa ya Utafiti Magonjwa ya Binadamu Dk Mwele Malecela mtoto wa Makamu wa zamani wa CCM John Malecela ni miongoni mwa wana CCM ambao wamejitosa kugombea urais kupitia CCM. Dk Mwele kesho amepangiwa na CCM kuchukua fomu za kuomba kugombea urais. Ratiba ya CCM iliyotolewa jana Makao Makuu ya chama hicho mjini hapa inaonesha kuwa licha ya Dk Mwele, mwingine ambaye atachukua fomu hiyo kesho ni Nicholaus Mtenda ambaye pia amejitokeza kuomba 
kugombea urais kupitia CCM. Dk Mwele katika maisha yake mengi kwa zaidi ya miaka 20 amekuwa mtumishi katika Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) ambako alianza kazi akiwa kijana na akapanda hadi kuwa mtafiti mkuu na baadaye akateuliwa kuwa Mkurugenzi Mkuu. Licha ya kukulia katika familia ya mwanasiasa maarufu nchini, lakini Dk Mwele hajawahi kujitokeza hadharani kushiriki kwenye masuala ya siasa. Kama akichukua fomu hiyo kesho, atakuwa ni mwanamke wa pili kuomba kuteuliwa na CCM kugombea urais kumrithi Rais Jakaya Kikwete. Mwanamke mwingine ni Balozi Amina Salum Ali wa Zanzibar. Jana Waziri wa Malisili na Utalii, Lazaro Nyalandu na wanachama wengine wawili wa CCM walichukua fomu za kuwania urais. Nyalandu alikuwa wa kwanza kufika katika ofisi za CCM kuchukua fomu akiwa amefuatana na familia yake na wafuasi wake kadhaa. Baadaye alifuatiwa na mwanachama mwingine wa CCM, Peter Nyalali, ambaye ni Ofisa mstaafu wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) na kufuatiwa na mwanachama wa chama hicho kutoka wilaya ya Muleba, Leonce Mulenda. Akizungumza mara baada ya kuchukua fomu, Nyalandu alisema hatua hiyo ni ishara ya yeye kuanza safari ya ndoto yake ya kuchukua majukumu ya urais kwa lengo la maendeleo ya nchi hii chini ya misingi aliyoianzisha Baba wa Taifa, hayati, Mwalimu Julius Nyerere. Kwa upande wa Nyalali, alisema atalenga katika kuimarisha uchumi kwa kuzingatia Katiba ya nchi na ya chama na kuleta mabadiliko chanya ndani ya CCM na kwa Watanzania ambao wamekuwa hawanufaiki na fursa zilizopo nchini. Kwa upande wa Leonce Mulenda, alisema atahakikisha Katiba ya Chama na maamuzi yanatekelezwa kama inavyotakiwa na kuwa chama imara kitakachosaidia serikali isiwe legelege.

No comments:

Post a Comment